Vigogo Ulaya wapewa mchongo kumpata Donnarumma
Muktasari:
- Donnarumma ambaye alijiunga na PSG mwaka 2021 akitokea AC Milan na ameshinda mataji ya Ligue 1 mara tatu mfululizo.
Paris Saint-Germain inatarajia kupokea ofa kutoka Chelsea, Manchester United au Inter Milan kwa kipa wa timu ya taifa ya Italia, Gianluigi Donnarumma, 26, ambaye ameomba kuondoka dirisha hili.
Donnarumma ambaye alijiunga na PSG mwaka 2021 akitokea AC Milan na ameshinda mataji ya Ligue 1 mara tatu mfululizo.
Hata hivyo, PSG ilijaribu kufanya naye mazungumzo ya kumsainisha mkataba mpya lakini ilishindikana.
Katika kuhakikisha inamruhusu kuondoka, PSG tayari imemsajili kipa wa Lille, Lucas Chevalier, kwa mkataba wa miaka mitano kwa ada ya Euro 40 milioni.
Vyanzo vinasema PSG haitaki kuendelea tena na kipa huyo wa kimataifa wa Italia, ambaye mkataba wake wa sasa unamalizika mwisho wa msimu ujao.
Donnarumma, ambaye tayari ni miongoni mwa wachezaji wanaolipwa zaidi PSG akiwa anakunja Euro 850,000 kwa mwezi, alitaka ongezeko la mshahara jambo halikufikiwa mwafaka.
Yoane Wissa
NEWCASTLE United inajiandaa kutoa ofa mpya ya Pauni 30 milioni kwenda Brentford ili kuipata saini ya mshambuliaji wa klabu hiyo, Yoane Wissa, 28. Wissa amekuwa kwenye kiwango bora msimu uliopita akifunga mabao 12 na kutoa asisti sita Ligi Kuu England, akisaidia Brentford kuwa moja kati ya timu shindani msimu uliopita. Newcastle inamwona kama mbadala wa Callum Wilson ambaye ametimkia West Ham.
Randal Kolo Muani
NEWCASTLE imeanzisha mazungumzo na PSG kujadili uwezekano wa kuipata huduma ya mshambuliaji wa klabu hiyo, Randal Kolo Muani, 26, ambaye msimu uliopita alifunga mabao tisa na kutoa asisti nne kwenye Ligue 1. Mbali ya Muani, Newcastle pia inamfukuzia kijana wa Porto na timu ya taifa ya Hispania, Samu Aghehowa 21, aliyefunga mabao 14 msimu wa 2024/25 Ligi Kuu Ureno. Mkataba wake unamalizika mwaka 2028.
Nicolas Jackson
MSHAMBULIAJI wa Chelsea, Nicolas Jackson 24, anataka kuendelea kucheza Ligi Kuu England ikiwa ataondoka katika kikosi hicho dirisha hili. Hivi karibuni Bayern Munich ilitajwa inamwinda sana na ilikuwa tayari kutoa ofa inayohitajika ili kumpata lakini suala hilo sasa linaonekana kuwa gumu. AC Milan na Juventus pia ni miongoni mwa timu zinazomhitaji. Katika msimu uliopita Jackson alifunga mabao 14 kwenye michuano yote.
Kingsley Coman
Al-Nassr ya Saudi Arabia imewasilisha ofa kwenda Bayern Munich ili kuipata saini ya winga wao, Kingsley Coman, 29, dirisha hili. Inaelezwa Bayern imekubali ofa hiyo lakini inasubiri maamuzi ya Coman ikiwa atakuwa tayari kwenda nchini humo au laa. Coman ambaye ameshinda Bundesliga mara nane tangu ajiunge na Bayern mwaka 2015, mkataba wake unatarajiwa kumalizika mwaka 2027.
Joao Neves
BAADA ya kufanikisha usajili wa mshambuliaji wa kimataifa wa Slovenia, Benjamin Sesko, 22, kutoka RB Leipzig, Manchester United sasa inataka kusajili kiungo wa kuzuia na kipa mpya. Mashetani hao wekundu wanahusishwa na majina kama Joao Neves wa Benfica na kipa Diogo Costa wa FC Porto. Man United imepanga kuboresha kikosi chao kuhakikisha inafanya vizuri msimu ujao baada ya kuwa katika kiwango kibovu msimu uliopita.
Jean-Philippe Mateta
MSHAMBULIAJI wa Crystal Palace, Jean-Philippe Mateta, 28, anatajwa ndio kipaumbele cha usajili wa Atalanta dirisha hili na ipo tayari kutoa hadi Euro 40 milioni ili kuipata huduma yake. Mateta anawindwa ili kwenda kuziba pengo la Ademola Lookman ambaye kuna uwezekano mkubwa akaondoka dirisha hili.
Tyler Dibling
SOUTHAMPTON imeendelea kusisitiza inahitaji walau Pauni 50 milioni kutoka kwa timu yoyote itakayohitaji saini ya winga wao, Tyler Dibling, 19, dirisha hili. Ripoti zinaeleza Everton wanavutiwa sana na fundi huyu ambaye anaichezea timu ya taifa ya England kwa vijana wenye umri chini ya miaka 21. Mkataba wake wa sasa unatarajiwa kumalizika mwaka 2027.