Shearer, Arteta watoa neno kwa Gyokeres
Muktasari:
- Mchezaji huyo raia wa Sweden alijiunga na Arsenal katika dirisha lililopita la majira ya kiangazi kwa ada ya Pauni 67 milioni kukiwa na matumaini ya kumaliza shida ya nafasi ya namba tisa, lakini ameshindwa kufikia matarajio na tangu msimu uanze amefunga mabao matatu tu.
LONDON, ENGLAND: STAA wa zamani wa Newcastle United, Alan Shearer anaamini straika wa Arsenal Viktor Gyokeres ataisaidia sana timu hiyo kwa kufunga mabao msimu huu, lakini hatoweza kufikia hata kidogo idadi ya mabao aliyoyafunga akiwa Sporting Lisbon.
Mchezaji huyo raia wa Sweden alijiunga na Arsenal katika dirisha lililopita la majira ya kiangazi kwa ada ya Pauni 67 milioni kukiwa na matumaini ya kumaliza shida ya nafasi ya namba tisa, lakini ameshindwa kufikia matarajio na tangu msimu uanze amefunga mabao matatu tu.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 hajafunga katika mechi zake saba za mwisho za michuano yote akiwa na Arsenal na alikosa nafasi nyingi wikiendi iliyopita wakati timu yake ikishinda bao 1-0 dhidi ya Fulham.
Shearer amesisitiza kwamba bado staa huyu hafikii katika viwango vya wachezaji kama Harry Kane, Erling Haaland au Kylian Mbappe, ingawa anaweza kutoa mchango mkubwa katika kikosi cha washika mitutu.
"Sio mchezaji wa levo za dunia, lakini naona analeta utofauti katika safu ya ushambuliaji ya Arsenal, jambo muhimu ni anatakiwa kuboresha uchezaji wake katika eneo la mwisho pamoja na kuwa makini na mtulivu. Moja ya vitu ambavyo navipenda kutoka kwake ni jinsi anavyokimbia nyuma ya safu ya ulinzi ya timu pinzani jambo linalowapa wachezaji wengine nafasi ya kucheza. Katika hili amesaidia sana Arsenal, ingawa hafungi,"amesema Shearer.
"Nina matumaini kwamba atafunga mabao siku za usoni, ingawa hayatoweza kufikia yale aliyofunga msimu uliopita."
Baada ya mechi dhidi ya Fulham, kocha wa Arsenal, Mikel Arteta kwa upande wake naye amesema:" Alikuwa karibu sana kufunga leo ni kama mara mbili au tatu. Sote tulikuwa tukimwombea afunge. Anafanya kazi kubwa sana na sisi tunaendelea kumsapoti na tunaamini mabao yatakuja."