Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Salah ang'ara, Misri yatinga 16 Bora

MISRI Pict

Muktasari:

  • Australia ilianza mchezo kwa kasi na ilikaribia kupata bao mapema katika dakika ya tano kupitia Cristian Volpato, ambaye shuti lake la mbali liligonga mwamba.

DALLAS, TEXAS: Timu ya Taifa ya Misri imeandika historia kwa kufuzu hatua ya 16 Bora ya Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza baada ya kuiondoa Australia kwa ushindi wa penalti 4-2, kufuatia sare ya bao 1-1 iliyodumu hadi baada ya dakika 120.

Australia ilianza mchezo kwa kasi na ilikaribia kupata bao mapema katika dakika ya tano kupitia Cristian Volpato, ambaye shuti lake la mbali liligonga mwamba.

Dakika chache baadaye, Jordan Bos naye alikaribia kuifungia timu yake, lakini juhudi zake zilizimwa na beki Rami Rabia akiwa katika nafasi nzuri ya kufunga.

Licha ya Australia kuonyesha ubora katika dakika za mwanzo, Misri ilitumia vyema nafasi yake ya kwanza iliyolenga lango na kufungua ukurasa wa mabao katika dakika ya 13. Emam Ashour alimalizia kwa kichwa krosi ya Karim Hafez na kuiandikia The Pharaohs bao la kuongoza.

Baada ya bao hilo, Australia iliongeza kasi na kutawala umiliki wa mpira, lakini ilishindwa kuzalisha nafasi nyingi za wazi. Aziz Behich alijaribu kusawazisha kwa shuti kali, lakini kipa Mostafa Shobeir aliokoa kwa ustadi. Wakati huo huo, Misri iliendelea kuwa tishio kwenye mashambulizi ya kushtukiza, ingawa nyota wake Mohamed Salah hakupata nafasi nyingi za kung'ara kipindi cha kwanza.

Kipindi cha pili kilianza kwa Misri kukosa nafasi ya kuongeza bao kupitia Omar Marmoush, kabla Australia haijapata bao la kusawazisha kupitia kujifunga kwa Mohamed Hany, aliyeelekeza wavuni mpira uliotokana na mpira wa adhabu.

Baada ya bao hilo, timu zote zilicheza kwa tahadhari huku kila upande ukitafuta bao la ushindi. Kipa wa Australia, Patrick Beach, aliokoa kwa ustadi kichwa cha Rami Rabia, huku Harry Souttar akiokoa shuti la Haissem Hassan karibu na mstari wa goli na kuufanya mchezo uingie dakika 30 za nyongeza.

Katika muda wa nyongeza, Salah alipata nafasi nzuri ya kuipa Misri ushindi, lakini shuti lake lilipaa juu ya lango. Dakika mbili kabla ya filimbi ya mwisho, Australia ilimwingiza kipa mkongwe Mathew Ryan mahsusi kwa ajili ya mikwaju ya penalti.

Katika hatua ya penalti, Harry Souttar alikosa mkwaju wa kwanza wa Australia na kuipa Misri mwanzo mzuri. Salah alionyesha utulivu na uzoefu mkubwa kwa kufunga penalti yake kwa mtindo wa Panenka, huku chipukizi wa Australia mwenye umri wa miaka 18, Lucas Herrington, naye akishindwa kufunga mkwaju wake.

Hossam Abdelmaguid aliifungia Misri penalti ya ushindi na kuihakikishia timu hiyo ushindi wa penalti 4-2 pamoja na tiketi ya kihistoria ya kutinga hatua ya 16 Bora ya Kombe la Dunia.

Kwa ushindi huo, Misri sasa itakutana na Argentina katika hatua ya 16 Bora, katika mchezo unaotarajiwa kuwa wa ushindani mkubwa.

Nahodha wa Misri, Mohamed Salah, alichaguliwa kuwa mchezaji bora wa mechi kutokana na mchango wake mkubwa, uongozi aliouonyesha uwanjani na utulivu wake wakati wa mikwaju ya penalti ulioisaidia timu yake kuandika historia.