Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Neymar kuwafuata Messi, Suarez

NEYMAR Pict

Muktasari:

  • Mkataba wa Neymar na Santos unamalizika Desemba 31, 2026, huku hadi sasa kukiwa hakuna uamuzi rasmi kuhusu kama ataendelea kubaki kwenye klabu hiyo ya Brazil.

MIAMI, MAREKANI: Nyota wa Brazil, Neymar, 34, anaweza kuachana na Santos mwishoni mwa mwaka huu na kuhamia Inter Miami, ambako anaweza kuungana tena na mastaa wenzake wa zamani wa Barcelona, Lionel Messi na Luis Suarez.

Mkataba wa Neymar na Santos unamalizika Desemba 31, 2026, huku hadi sasa kukiwa hakuna uamuzi rasmi kuhusu kama ataendelea kubaki kwenye klabu hiyo ya Brazil.

Mustakabali wa Neymar umeendelea kuibua maswali baada ya tukio lililotokea kufuatia sare ya mabao 2-2 dhidi ya Chapecoense.

Kwa mujibu wa taarifa, Neymar alifika katika kituo cha mazoezi cha Santos, akakaa kwa muda mfupi kabla ya kuondoka bila ruhusa, huku akikosa kushiriki katika mazoezi ya kurejesha nguvu yaliyopangwa kwa wachezaji walioanza mchezo huo.

Tukio hilo lilizua sintofahamu ndani ya klabu, lakini Santos iliamua kutomchukulia hatua za kinidhamu, huku mchezaji huyo akirejea kwenye mazoezi yaliyofuata.

NEY 01

Neymar bado hajafunga mlango wa kuendelea na soka, huku uwezekano wa kubaki Santos, kutafuta klabu nyingine au hata kustaafu ukiwa wazi.

Katika mazingira hayo, Inter Miami imeanza kuonekana kama moja ya vituo vinavyoweza kumvutia, hasa kutokana na uwepo wa Messi na Suarez.

Neymar, Messi na Suarez waliunda moja ya safu hatari zaidi za ushambuliaji duniani walipokuwa Barcelona kati ya mwaka 2014 na 2017.

Katika kipindi hicho, watatu hao walishinda mataji tisa, yakiwamo Ligi ya Mabingwa Ulaya, mataji mawili ya La Liga, Copa del Rey mara tatu, Super Cup ya Hispania, UEFA Super Cup na Kombe la Dunia la Klabu.

NEY 02

Katika msimu wao wa kwanza pamoja, walikuwa sehemu muhimu ya Barcelona iliyotwaa mataji matatu na kufunga jumla ya mabao 122 katika mashindano yote; Messi akifunga 58, Neymar 39 na Suarez 25.

Sasa, uwezekano wa MSN—Messi, Suarez na Neymar,kuungana tena Miami umeanza kupewa uzito, ingawa bado hakuna makubaliano yaliyofikiwa kati ya Neymar na Inter Miami.


SWALI LA AFYA

Pamoja na mvuto mkubwa wa kibiashara na kimichezo wa kuwakutanisha tena mastaa hao, suala kubwa linaloweza kuamua hatma ya Neymar ni utimamu wake wa mwili.

Akiwa na umri wa miaka 34, sehemu kubwa ya miaka ya hivi karibuni ya Neymar imekuwa ikigubikwa na majeraha na kukosa mwendelezo wa kucheza.

NEY 03

Hata hivyo, kipaji chake bado kinatambulika na kama ataweza kubaki fiti, uwepo wake pamoja na Messi na Suarez unaweza kuwa kivutio kikubwa katika soka la Marekani.

Kwa sasa, Santos bado inamsubiri Neymar afanye uamuzi kuhusu mustakabali wake, huku Inter Miami ikiwa na Messi na Suarez na dirisha la uhamisho likitoa uwezekano wa kutokea kwa muungano mwingine wa kihistoria.