Mtoto wa tajiri aibuka Man United
Muktasari:
- Licha ya familia hiyo kukosolewa sana na mashabiki kutokana na kuingiza klabu kwenye madeni tangu walipoinunua 2005, imeendelea umiliki wake kwa kuwa na hisa nyingi na kugoma kuziuza.
MANCHESTER, ENGLAND: EDWARD Glazer, mmoja wa ndugu watano wenye hisa nyingi kwenye umiliki wa klabu ya Manchester United, amebainisha juu ya mpango wa familia hiyo ya Kimarekani juu ya kutathmini mustakabali wa klabu hiyo ya Old Trafford.
Licha ya familia hiyo kukosolewa sana na mashabiki kutokana na kuingiza klabu kwenye madeni tangu walipoinunua 2005, imeendelea umiliki wake kwa kuwa na hisa nyingi na kugoma kuziuza.
Mwaka 2024, bilionea wa Uingereza, Sir Jim Ratcliffe alikamilisha dili la kununua asilimia 27.7 ya hisa za klabu hiyo kwa thamani ya Pauni 1.25 bilioni. Na katika makubaliano yao, tajiri Ratcliffe atasimamia masuala yote ya kisoka katika klabu hiyo, akisaidiana na wakurugenzi Jason Wilcox na Omar Berrada. Edward ni mmoja wa watoto wa tajiri wa Man United, Malcolm Glazer, aliyefariki dunia 2014.
Mapema msimu huu, kuliibuka uvumi kwamba huenda klabu hiyo ikanunuliwa na tajiri mpya, wakati Turki Al-Sheikh alipoposti kwenye mtandao wa kijamii kwamba Man United ipo kwenye hatua za mwisho kabisa za mazungumzo ya timu hiyo kuuzwa kwa mwekezaji mpya.
Kwenye X, Al-Sheikh aliandika: “Habari njema nilizosikia hii leo ni kwamba Manchester United ipo kwenye hatua za juu kabisa za kukamilisha mazungumzo ya kuuzwa kwa mwekezaji mpya...nadhani atakuwa mwekezaji bora kuliko waliopita.”
Kisha aliposti tena: “Posti yangu iliyopita kuhusu uwezekano wa Man United kuuzwa nilikuwa na maana moja, klabu ipo kwenye mazungumzo ya mwekezaji mpya.
“Kuelezea zaidi, mimi sio mwekezaji, wala hatokei kwenye nchi yangu. Nimeposti hiyo kama shabiki tu anayetaka dili hilo litokee, licha kwamba inaweza isiwe lazima kutokea.”
Kwa kipindi hicho, maofisa wakuu wa Man United walibainisha kwamba taarifa hizo za Al-Sheikh hata kwao ni mpya pia, hawazifahamu. Hata hivyo, uamuzi wa familia ya Glazer kama itaamua kuiuza jumla klabu hiyo, bilionea Ratcliffe hatakuwa na nguvu ya kuzuia.