Mshkaji wa Messi ahusishwa kuondoka kwa kocha
MIAMI, MAREKANI: KUONDOKA ghafla kwa kocha Javier Mascherano katikati ya msimu kwenye kikosi cha Inter Miami kwa kile kilichoelezwa kuwa “sababu binafsi” kumeacha maswali kwani hakutoa maelezo ya kina wakati wa kuaga wiki iliyopita, lakini zigo la lawama linaelekezwa kwa mastaa wawili ambao ni washkaji zake supastaa wa timu hiyo, Lionel Messi.
Mwanzoni ilionekana kuwa sababu za kuondoka kwake zilihusiana zaidi na masuala ya kiuchezaji kuliko vinginevyo, ukiwamo pia mwanzo mbaya wa msimu na hasa kuondolewa kwenye kinyang’anyiro cha ubingwa wa Shirikisho la Soka la Amerika Kaskazini, Kati na Karibea (CONCACAF), mashindano yaliyokuwa lengo la klabu kufika mbali zaidi. Hata hivyo taarifa mpya zimeibuka zikielekeza lawama kwa wachezaji wawili muhimu.
Mwandishi maarufu wa michezo na habari za uchunguzi wa Argentina, Toti Pasman amedai kuwa wachezaji wenzake na Lionel Messi walikuwa chanzo cha mgogoro na uhusiano kati ya Mascherano na Rodrigo De Paul haukuwa mzuri.
Inadaiwa Mascherano hakumtaka De Paul aletwe kwenye kikosi, huku kiungo huyo akiwa na ushawishi mkubwa ndani ya vyumba vya kubadilishia nguo, jambo lililosababisha hali ya kutokuelewana. De Paul alitua wakati wa usajili wa dirisha dogo la Januari akitokea Atletico Madrid ya Hispania.
Pasman alimtaja pia mchezaji mwingine kuwa ni Luis Suarez, akisema uhusiano wake na Mascherano uliharibika, na kocha huyo akaamua kumpiga katika mojawapo wa mechi kutokana na kutokuwa fiti kimwili, lakini mshambuliaji huyo alikuja kufunga bao katika mechi iliyofuata na kuibua hisia mbalimbali ikiashiria mvutano baina yao.
Kwa sasa, Guillermo Hoyos amechukua jukumu la kuinoa timu hiyo kwa muda wakati ikisaka ufumbuzi wa suala la benchi la ufundi. Hata hivyo Messi bado hajazungumzia suala hilo hadharani, licha ya kuwa alikuwa mmoja wa waliounga mkono ujio wa Mascherano alipomrithi Tata Martino, ambaye naye pia aliondoka kwa sababu zilizotajwa kuwa binafsi.