Mapacha wa Ecuador watua Arsenal, ishu ya kucheza ipo hivi
Muktasari:
- Ndugu hao, Edwin na Holger Quintero, watahamia rasmi London Kaskazini Agosti 2027 wakitokea Independiente del Valle ya nchini kwao Ecuador, klabu ambayo Moises Caicedo wa Chelsea alitokea kabla ya kuhamia Brighton mwaka 2021.
Arsenal imetangaza kuwasajili wachezaji mapacha wenye vipaji kutoka Ecuador, lakini mashabiki wa The Gunners duniani kote watapaswa kusubiri miaka miwili ili kuona wakiingia kwenye kikosi cha wakubwa, kwani lazima wacheze baada ya kufikisha miaka 18.
Ndugu hao, Edwin na Holger Quintero, watahamia rasmi London Kaskazini Agosti 2027 wakitokea Independiente del Valle ya nchini kwao Ecuador, klabu ambayo Moises Caicedo wa Chelsea alitokea kabla ya kuhamia Brighton mwaka 2021.
Taarifa ya Arsenal imeeleza: “Edwin na Holger wanatambulika kwa vipaji vyao vya soka vinavyosisimua zaidi katika ukanda wa Amerika Kusini, wakionyesha utendaji thabiti na wa kuvutia katika timu za vijana kwa klabu na taifa. Wote wameshajumuishwa katika timu ya taifa ya U17 ya Ecuador.
“Edwin anatumia mguu wa kushoto, mwepesi na mchezaji mwenye ujuzi wa kunyumbulika, anacheza kama kiungo wa kushoto na kulia, anapenda kumkabili mpinzani na ana mbinu nyingi za kipekee.
“Holger anatumia mguu wa kulia, ni kiungo mshambuliaji mwenye ujuzi na ufundi, anajua kupambana kwa maono ya kuisaidia timu na pia ana uwezo wa kuwakabili wapinzani kwa haraka.”
Mapacha hao walipiga picha wakiwa wamevaa jezi za Arsenal na kusaini mkataba wakiwa karibu na mkurugenzi wa michezo wa klabu hiyo, Andrea Berta.
Arsenal itafuatilia maendeleo ya mapacha hao kwa miaka miwili ijayo wakiwa na klabu ya Independiente del Valle.
Taarifa ya Arsenal imeongoza: “Kila mtu hapa Arsenal ana furaha kubwa kuwakaribisha mapacha wa Quintero kwa ajili ya kuisaidia klabu yetu siku za usoni.”