Man United yamgeukia Tchouameni
Muktasari:
- United imekuwa ikisaka kiungo wa kiwango cha juu wa kuongeza nguvu katikati ya uwanja, huku Tchouameni akitajwa kuwa mmoja wa wachezaji wanaopewa kipaumbele na benchi la ufundi kuelekea msimu mpya.
MANCHESTER United inaweza kupata nafasi kubwa ya kumsajili kiungo Aurelien Tchouameni ikiwa Real Madrid itafanikiwa kukamilisha usajili wa Rodri kutoka Manchester City.
Kwa mujibu wa gazeti la AS la Hispania, Real Madrid ina imani kubwa ya kufanikisha dili la Rodri kwa ada inayokadiriwa kufikia Pauni43 milioni, licha ya kiungo huyo kufanyiwa upasuaji mdogo wa mgongo mwanzoni mwa wiki hii.
Taarifa hizo zinaeleza kuwa iwapo Rodri atatua Santiago Bernabeu, Real Madrid itakuwa tayari kumruhusu Tchouameni kuondoka, hatua itakayofungua mlango kwa Manchester United kuwasilisha ofa ya takribani Pauni68 milioni kwa ajili ya nyota huyo wa kimataifa wa Ufaransa.
United imekuwa ikisaka kiungo wa kiwango cha juu wa kuongeza nguvu katikati ya uwanja, huku Tchouameni akitajwa kuwa mmoja wa wachezaji wanaopewa kipaumbele na benchi la ufundi kuelekea msimu mpya.
Wakati huo huo, Manchester City bado ilikuwa na matumaini ya kumbakiza Rodri kwa kumpa mkataba mpya, lakini dalili zinaonyesha kiungo huyo anatamani kurejea nyumbani Hispania na kuvaa jezi ya Real Madrid.
Ikiwa dili hilo litakamilika, linaweza kuwa mwanzo wa mabadiliko makubwa katika safu za kiungo za vigogo hao wawili, huku United ikisubiri kwa hamu kuona kama ndoto yake ya kumpata Tchouameni itageuka kuwa uhalisia.
Ousmane Diomande
KOCHA wa Nottingham Forest, Oliver Glasner, ameanza kuunda kikosi chake kwa msimu mpya baada ya kuweka wazi maeneo manne anayohitaji kuimarisha haraka ili kuongeza ushindani wa timu hiyo kwenye Ligi Kuu England. Kipaumbele ni kuimarisha safu ya ulinzi, ambapo Forest ipo mbioni kumsajili beki wa Sporting Lisbon, Ousmane Diomande, mwenye umri wa miaka 22.
John Stones
BEKI wa kimataifa wa England, John Stones, yupo hatua moja tu kujiunga na Inter Milan baada ya kufikia makubaliano ya awali ya mkataba, huku akitarajiwa kufanyiwa vipimo vya afya kabla ya kutambulishwa rasmi na mabingwa hao wa Italia. Stones, ambaye aliachana na Manchester City mwishoni mwa msimu uliopita, sasa anakaribia kuanza ukurasa mpya wa maisha yake ya soka nchini Italia.
Yan Diomande
KIJANA anayetikisa soka la dunia, Yan Diomande, yupo hatua moja tu kutimiza ndoto yake ya kujiunga na Real Madrid baada ya vigogo hao wa Hispania kukubali kuvunja benki ili kuinasa saini yake katika moja ya usajili mkubwa zaidi kuwahi kutokea. Real Madrid inadaiwa kukubali kulipa zaidi ya Pauni100 milioni kwa ajili ya nyota huyo mwenye umri wa miaka 19, ada itakayomfanya kuwa usajili ghali.
Liam Delap
LIAM Delap anaweza kupewa nafasi ya kuokoa maisha yake ya soka baada ya kushindwa kung’ara Chelsea, huku Nottingham Forest ikifufua mpango wa kumsajili mshambuliaji huyo katika dirisha hili la usajili. Kwa mujibu wa The Telegraph, Forest haijakata tamaa kwa Delap licha ya kushindwa kumpata msimu uliopita alipohamia Chelsea. Klabu hiyo bado inaamini nyota huyo atawasaidia.
Illia Zabarnyi
LIVERPOOL imeingia kwenye mbio za kumsajili beki wa Paris Saint-Germain, Illia Zabarnyi, baada ya nyota huyo wa Ukraine kuripotiwa kutoridhishwa na hali yake ndani ya kikosi cha mabingwa hao wa Ufaransa. Kocha wa Liverpool, Andoni Iraola, amemuweka Zabarnyi kwenye orodha ya vipaumbele vyake kutokana na kufahamu vizuri uwezo wake tangu walipowahi kufanya kazi pamoja.
Josh Acheampong
CRYSTAL Palace imeonyesha nia ya kumnasa beki chipukizi wa Chelsea, Josh Acheampong, kwa mkopo, lakini vigogo hao wa Stamford Bridge hawana mpango wa kumwachia kirahisi kutokana na kumchukulia kuwa sehemu ya mustakabali wa klabu. Kwa mujibu wa BBC, Palace inaamini inaweza kumshawishi Chelsea kumruhusu Acheampong kuondoka kwa mkopo ili apate nafasi ya kucheza zaidi.
Harry Amass
MANCHESTER United ipo hatarini kurudia kosa kubwa la usajili baada ya kuweka kwenye mstari wa kumuacha beki chipukizi Harry Amass kwa ada ndogo, hatua inayoweza kuigharimu baadaye kama ilivyotokea kwa Alvaro Carreras. Uamuzi wa kumuachia Amass mwenye umri wa miaka 19 kwa kiasi kinachokadiriwa kuwa Pauni6 milioni umeibua maswali ndani ya mashabiki wa United.
Cesar Palacios
FULHAM imeanza mazungumzo ya kumsajili kiungo wa Real Madrid, Cesar Palacios, huku kocha wa zamani wa vijana wa klabu hiyo, Alvaro Arbeloa, akitajwa kuwa chanzo kikubwa cha kuvutiwa kwa washambuliaji wa Los Blancos. Palacios, mwenye umri wa miaka 21, ameibuka kuwa mmoja wa walengwa wakuu wa Fulham katika dirisha hili la usajili, huku Arbeloa akiwa na uhusiano mzuri naye.
Savinho
WINGA wa Manchester City, Savinho, ameweka wazi nia yake ya kuondoka Etihad na kujiunga na Tottenham, huku akiweka presha kwa mabosi wa klabu hiyo kukubali dili la uhamisho linalokadiriwa kufikia Pauni60 milioni. Kwa mujibu wa taarifa kutoka England, Tottenham imerejea kwenye mazungumzo ya kumsajili nyota huyo wa Brazil, ambaye tayari amewaeleza viongozi wa City kuwa anataka changamoto mpya.