Madrid yapanga kuanza kubonga na Vinicius Jr
Muktasari:
- Taarifa kutoka Hispania zinaeleza uongozi wa klabu unataka kumlinda staa huyo asiondoke baada ya upepo uliopita hivi karibuni kati yake na kocha Xabi Alonso.
REAL Madrid inatarajiwa kuanza upya mazungumzo ya mkataba mpya na mshambuliaji wa kimataifa wa Brazil, Vinicius Jr, 25, ambaye ameweka wazi kuwa ana nia ya kuendelea kubaki Santiago Bernabeu baada ya kufanya mazungumzo na benchi la ufundi.
Taarifa kutoka Hispania zinaeleza uongozi wa klabu unataka kumlinda staa huyo asiondoke baada ya upepo uliopita hivi karibuni kati yake na kocha Xabi Alonso.
Vinicius anahitaji mshahara wa takribani Pauni 600,000 ambazo ni sawa na mshahara wa sasa wa Kylian Mbappe. Haijajulikana ikiwa Madrid itakuwa tayari kumpa mshahara huo, lakini kwa sasa wanaendelea kufanya mazungumzo na wawakilishi wake ili kufikia mwafaka.
Mkataba wa sasa wa Vinicius unatarajiwa kumalizika 2027 na mwishoni mwa mwaka jana aliripotiwa huenda angeondoka.
Manuel Akanji
BAADA ya kucheza kwa takribani nusu msimu Inter Milan inapanga kubadilisha dili la mkopo la beki wa Manchester City na timu ya taifa ya Uswisi, Manuel Akanji, 30, kuwa la kudumu.
Inaelezwa kwamba Akanji amewavutia viongozi wa Inter Milan kutokana na uzoefu na uwezo mkubwa aliouonyesha tangu ajiunge mwaka jana.
Klabu hiyo iko tayari kuanza mazungumzo rasmi na Manchester City kuhusu uhamisho wa jumla.
Raheem Sterling
WEST Ham United imeonyesha nia ya kumsajili kiungo mshambuliaji wa Chelsea na timu ya taifa ya England, Raheem Sterling, 31, ambaye kwa sasa hapati nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza.
Awali, taarifa zilieleza Sterling amechoshwa kutocheza na angependa kuondoka, lakini anaweza kusitisha suala hilo kwa sasa baada ya kocha Enzo Maresca kusepa zake.
Leon Goretzka
BAYERN Munich iko tayari kumuuza kiungo wa kimataifa wa Ujerumani, Leon Goretzka, 30, katika dirisha hili.
Inadaiwa kwamba klabu hiyo ya Ujerumani haina pingamizi la kumuachia ikiwa itapokea ofa inayoridhisha na hadi sasa Tottenham Hotspur, Arsenal na Manchester United zimeonyesha nia ya kumsajili.
Goretzka anawindwa na vigogo hao kwa sababu hapati nafasi kikosi cha kwanza.
Bruno Fernandes
MANCHESTER United inaripotiwa kuwa tayari kumuuza kiungo wake na nahodha wa timu hiyo, Bruno Fernandes, 31, katika dirisha hili la usajili.
Inaelezwa kwamba uongozi wa klabu unatazama upya mwelekeo wa kikosi na uko tayari kusikiliza ofa zitakazowasilishwa katika dirisha hili au lijalo.
Hata hivyo, Mashetani Wekundu hawatamlazimisha kuondoka badala yake watamuuza ikiwa tu yeye mwenyewe atataka kuondoka.
Adama Traore
WEST Ham United inaendelea na jitihada za kumsajili winga wa Fulham na timu ya taifa ya Hispania, Adama Traore, 29, lakini dili hilo linaonekana kukwama kutokana na madai makubwa ya mshahara.
Taarifa zinaeleza West Ham inaamini Traore ataongeza kitu katika safu ya ushambuliaji na imepanga kumpa mshahara wa Pauni 70,000 kwa wiki lakini mwenyewe anataka kuanzia Pauni 100,000 kwa wiki. Mazungumzo bado yanaendelea
Mo Salah
AS Roma imeonyesha nia ya kutaka kumsajili tena winga wa Liverpool na timu ya taifa ya Misri, Mohamed Salah, 33, baada ya kuona timu za Saudi Arabia zimejiondoa katika katika dirisha hili.
Taarifa za Italia zinaeleza kuwa Roma inamwona Salah kama staa mwenye uzoefu mkubwa ambaye anaweza kuiongezea nguvu safu ya ushambuliaji.
Hata hivyo, masuala ya kifedha na mshahara mkubwa ambao anauhitaji inaonekana kuwa changamoto kubwa inayoweza kukwamisha dili hilo.
Jean-Philippe Mateta
MANCHESTER United imeanza harakati za kuimarisha kikosi kwa kuwafuatilia mshambuliaji na beki kutoka Ufaransa.
Wa kwanza inayempa kipaumbele zaidi cha kumsajili ni staa wa Crystal Palace, Jean-Philippe Mateta, 28, na beki wa Rennes, Jeremy Jacquet, 20.
Mkataba wa sasa wa Mateta unatarajiwa kumalizika ifikapo 2027 na anadaiwa kwamba keshagoma kusaini mkataba mwingine akisisitiza kwamba anataka kuondoka mwisho wa msimu huu.