Jamie Carragher aukubali mziki wa Arsenal
Muktasari:
- Carragher ametoa kauli hiyo baada ya kushuhudia ushindi wa Manchester City wa mabao 3–0 dhidi ya Liverpool jana Jumapili, Novemba 9, 2025. Ushindi huo uliiwezesha timu ya Pep Guardiola kupanda hadi nafasi ya pili, ikiishusha Chelsea, na kwa sasa iko nyuma ya Arsenal kwa pointi nne.
Gwiji wa Liverpool, Jamie Carragher, ameitaja Arsenal kuwa timu bora zaidi katika Ligi ya EPL msimu huu.
Carragher ametoa kauli hiyo baada ya kushuhudia ushindi wa Manchester City wa mabao 3–0 dhidi ya Liverpool jana Jumapili, Novemba 9, 2025. Ushindi huo uliiwezesha timu ya Pep Guardiola kupanda hadi nafasi ya pili, ikiishusha Chelsea, na kwa sasa iko nyuma ya Arsenal kwa pointi nne.
Licha ya kiwango bora kilichoonyeshwa na Manchester City, Carragher amesema hana shaka kwamba kikosi cha Mikel Arteta ndicho bora zaidi nchini England kwa sasa.
Beki huyo wa zamani wa England amekiri kuwa Manchester City itaendelea kuiweka Arsenal chini ya shinikizo katika mbio za ubingwa, hasa ikizingatiwa kwamba Arsenal imewahi kupoteza mara mbili dhidi ya kikosi cha Guardiola katika misimu iliyopita.
Carragher ameambia Sky Sports: “Mara mbili katika miaka mitatu iliyopita, wamekuja kutoka nyuma na kuipiku Arsenal. Liverpool ndio mabingwa, lakini City imewazidi. Wanaweza kuwa wanapata kumbukumbu za mara zilizopita walipokuwa na nafasi ya kuchukuwa ubingwa.
“Bado ninaamini Arsenal ndiyo timu bora zaidi niliyoshuhudia katika Ligi ya EPL msimu huu, bila shaka.”
Kwa sasa, Arsenal inaongoza msimamo wa Ligi ya EPL kwa pointi 26, ikifuatiwa na Manchester City (22), kuelekea mapumziko ya mechi za kimataifa, na wanatarajiwa kurejea kwa nguvu kutafuta ushindi katika mchezo wao ujao wa ligi.
MECHI TANO ZIJAZO ZA ARSENAL
Tottenham Hotspur – Novemba 23 2025, nyumbani
Chelsea – Novemba 30 2025, ugenini
Brentford – Novemba 03 2025, nyumbani
Aston Villa – Desemba 06 2025, ugenini
Everton – Desemba 21 2025, ugenini
MECHI TANO ZIJAZO ZA MANCHESTER CITY
Manchester City – Novemba 22, 2025, ugenini
Leeds United – Novemba, 29 2025, nyumbani
Manchester City – Desemba 3, 2025, ugenini
Sunderland – Desemba 6, 2025, nyumbani