Federico Chiesa atemwa kikosi cha Ligi ya Mabingwa Ulaya
Muktasari:
- Liverpool imewasilisha rasmi orodha yake ya wachezaji 25 kwa ajili ya michuano hiyo mikubwa ya klabu barani Ulaya, huku ikianza safari ya kusaka taji lake la saba la Ulaya kwa kumenyana na Atletico Madrid kwenye Uwanja wa Anfield Jumatano usiku.
LIVERPOOL, ENGLAND: NYOTA wa Italia, Federico Chiesa, amepata pigo jingine katika maisha yake ya soka ndani ya Liverpool baada ya kuachwa kwenye kikosi cha wachezaji 25 kitakachoshiriki Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu huu.
Liverpool imewasilisha rasmi orodha yake ya wachezaji 25 kwa ajili ya michuano hiyo mikubwa ya klabu barani Ulaya, huku ikianza safari ya kusaka taji lake la saba la Ulaya kwa kumenyana na Atletico Madrid kwenye Uwanja wa Anfield Jumatano usiku.
Hata hivyo, Chiesa hatakuwa sehemu ya safari hiyo baada ya kocha mpya wa Liverpool, Andoni Iraola, kutomjumuisha kwenye kikosi cha michuano hiyo.
Kiungo mwingine aliyeachwa ni Wataru Endo, ambaye kama Chiesa, hajacheza katika mechi mbili za kwanza za Liverpool za Ligi Kuu England msimu huu.
Chiesa, 28, amekosa mechi hizo mbili kutokana na majeraha ya misuli. Lakini hata akirejea akiwa fiti, anatarajiwa kukutana na ushindani mkubwa zaidi wa nafasi kufuatia Liverpool kuimarisha safu yake ya ushambuliaji katika dirisha la usajili la majira ya kiangazi kwa kumsajili Bradley Barcola na Victor Munoz.
Kwa Chiesa, hii ni kama muendelezo kwani alikumbana na hali kama hiyo msimu uliopita chini ya aliyekuwa kocha wa Liverpool, Arne Slot.
Hata hivyo, wakati huo Chiesa alifanikiwa kuingizwa kwenye kikosi cha wachezaji 25 baada ya beki wa kati Giovanni Leoni kupata jeraha kubwa la goti, akipasuka mishipa ya mbele ya goti (ACL).
Leoni ni mmoja wa wachezaji watatu wa Liverpool ambao kwa sasa wana majeraha lakini wamejumuishwa kwenye kikosi cha Iraola kwa ajili ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Wengine ni Conor Bradley na Hugo Ekitike.
Leoni anatarajiwa kurejea mazoezini baadaye mwezi huu baada ya kukaa nje kwa karibu mwaka mmoja. Bradley naye amekuwa nje tangu Januari baada ya kupata jeraha la goti, wakati Ekitike amekuwa akisumbuliwa na jeraha la mishipa ya nyuma ya kifundo cha mguu (Achilles) tangu Aprili.
Kuwajumuisha wachezaji hao watatu waliopo kwenye orodha ya majeruhi kunatoa matumaini kwa mashabiki wa Liverpool kwamba wanaweza kurejea na kushiriki sehemu ya michuano hiyo kabla ya kumalizika kwa hatua ya ligi Januari 27, 2027.
Kwa upande wa Endo, ambaye pia hajashiriki mechi mbili za mwanzo za msimu, nafasi yake imechukuliwa na kinda wa miaka 21, James McConnell, ambaye amependelewa katika orodha ya viungo.
Liverpool pia imewajumuisha vijana wengine waliokulia katika akademi yake, Luke Chambers na Isaac Mabaya, ambao ni sehemu ya mabeki 11 waliotajwa kwenye orodha hiyo.
Kwa mujibu wa kanuni za UEFA, kila klabu inatakiwa kuwa na wachezaji wasiopungua nane katika List A ambao wamepata mafunzo ya soka ndani ya nchi husika au katika klabu hiyo.
Hata hivyo, vijana kama Rio Ngumoha na Trey Nyoni hawajalazimika kuingia kwenye orodha hiyo ya wachezaji 25 kutokana na umri wao. Wanaweza kusajiliwa kupitia List B, na hali hiyo itaendelea hadi watakapofikisha umri wa miaka 21.
Kwa Chiesa, kuachwa tena kwenye kikosi hicho ni pigo jingine katika harakati zake za kupata nafasi ya kudumu ndani ya Liverpool, tangu alipohamia Anfield.
Kwa kipindi alichokaa hapo tangu 2024, amefanikiwa kuwa na maisha ya kupanda na kushuka akiwa amefanikiwa kucheza michezo 50 na kufunga mabao matano.