Prime
Wawili Yanga wazua gumzo Botswana! Kocha Gaborone afunguka
YANGA leo usiku itafanya mazoezi yake ya mwisho kabla ya kesho Jumamosi usiku kuanza hesabu zake za kwanza kwenye anga la kimataifa ikikabiliana na Gaborone United nchini Botswana, lakini kocha wa wenyeji wao, amewataja viungo wawili na mshambuliaji Peter Shalulile kwenye hesabu zake.
Yanga itacheza mechi yake ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya awali, itakayopigwa kesho Jumamosi kuanzia saa 2:00 usiku kwa saa za Tanzania kwenye Uwanja wa Kimataifa wa Botswana, kabla ya kurudiana Septemba 12, 2026 jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na Mwanaspoti kwa njia ya simu, kocha wa Gaborone United, Sean Connor, amesema kikosi chake kitakuwa na mchezo mgumu kwa sababu itakutana na timu bora ya Yanga yenye wachezaji wenye wasifu mkubwa.
Connor raia wa Ireland Kaskazini, amesema kuwa amepata taraifa za kutosha za ubora wa Yanga, akiwafannyia umafia kutoka kwa rafiki zake ambao wako Tanzania na kwamba amebaini wageni wao hao wana safu bora ya ushambuliaji inayongozwa na Shalulile.
“Tunakwenda kukutana na timu nzuri yenye jina kubwa Afrika, baada ya kupangwa kwa ratiba hii, nilianza kazi ya kuwafuatilia, kuna rafiki zangu wamenipa taarifa za kutosha kuhusu wao (Yanga), tunatakiwa kujipanga sawasawa,” amesema Connor.
“Ukiiangalia kwenye makaratasi utaona wana safu nzuri ya ushambuliaji, wamekuwa kwenye kiwango kizuri kwenye ligi ya nyumbani, huwezi kuona ni timu rahisi unayokutana nayo ikiwa na mshambuliaji kama Peter Shalulile, ambaye amecheza soka la Afrika Kusini kwa mafanikio na Afrika kwa ujumla.”
Aidha Connor ameongezakuwa, uwepo wa Shalulile, makali yake yanachagizwa na ubora wa viungo wa timu hiyo akiwataja Maxi Nzengeli na Stephanie Aziz KI ambao lazima wawazuie kucheza kwa ubora kudhibiti makali yao.
“Ukiangalia eneo la kiungo nako wana wachezaji wazuri, nimeona kuna kiungo kutoka Kongo (Maxi) ni mchezaji mwenye nishati ya kutosha akiwa uwanjani lakini wana Aziz KI ni mmoja kati ya viungo bora Afrika, unapotakiwa kushindana na timu ya namna hiyo lazima uwe na mpango wa kuwafanya wasicheze kwa uhuru wao.”
Wana mabeki wa pembeni nao wanafanya kazi nzuri ya kupandisha mashambulizi kwenda juu, usisahau wana kocha mwenye wasifu mzuri kutoka Afrika Kusini, Manqoba (Mngqithi), niliwahi kufanya kazi Afrika Kusini, namjua vizuri ni kocha mkubwa.”
Hata hivyo, Connor aliwapiga mkwara Yanga akisema kikosi chake kimejiandaa kupambana na wala hakitaingia kinyonge kwenye mchezo huo wa nyumbani na kwamba watatumia hesabu zao kuwapa sapraizi mabingwa hao wa Tanzania.
“Tumejiandaa kama ambavyo nilikwambia awali, tutakuwa nyumbani mbele ya mashabiki wetu, tutakwenda kupambana nao kwa kutumia ubora wetu, hatutaki kuwakatisha tamaa mashabiki wetu, tutaingia na akili ya kushindana na Yanga.”
HERSI ATUA
Yanga wakati inaondoka nchini, waliongozana na Makamu wa Rais wa klabu hiyo, Arafat Haji, lakini jana vigogo zaidi wakaongezeka wakiongozwa na Rais wa klabu hiyo, injinia Hersi Said akiambatana na wajumbe wengine wa kamati ya utendaji.
Uwepo wa Hersi jijini Gaborone, kunasubiriwa kwa hamu na kikosi hicho ambapo Mwanaspoti linafahamu kwamba kigogo huyo ndiye atatamka bonasi kamili ya mechi hizo za awali kwa wachezaji wa timu hiyo atakapozungumza nao kesho kabla ya mechi.