Dah! Manchester United yaporomoka kiuchumi
Muktasari:
- Licha ya mapato yao kuongezeka kwa Pauni 40 milioni, uongozi wa Sir Jim Ratcliffe na kundi la Ineos, umeshuhudia klabu hiyo ikishuka hadi nafasi ya chini zaidi kuwahi kufika kwenye jedwali la mapato.
MANCHESTER, ENGLAND: MANCHESTER UNITED imeshuka hadi nafasi ya nane kwenye orodha ya klabu zenye mapato makubwa zaidi duniani.
Licha ya mapato yao kuongezeka kwa Pauni 40 milioni, uongozi wa Sir Jim Ratcliffe na kundi la Ineos, umeshuhudia klabu hiyo ikishuka hadi nafasi ya chini zaidi kuwahi kufika kwenye jedwali la mapato.
Takwimu za hivi karibuni zilizokusanywa na wataalamu wa masuala ya fedha za soka wa Deloitte zinaonyesha Man United wako nyuma ya Liverpool, Manchester City na Arsenal, hivyo kushika nafasi ya nne kwenye orodha ya timu zenye mapato makubwa kwa upande wa Ligi Kuu England.
Mapato ya jumla ya Man United kutokana na viingilio vya mashabiki uwanjani, haki za matangazo na mikataba ya kibiashara yaliongezeka kutoka Pauni 653 milioni msimu wa 2023-24 hadi Pauni 692 milioni msimu uliopita.
Hata hivyo, kumaliza ligi nafasi ya 15 kulichangia kupungua kwa mapato ya matangazo kwa Pauni 45 milioni.
Man United ambayo imewahi kuwa kileleni mwa orodha hiyo miaka ya nyuma, imeshuka nafasi nne ikilinganishwa na mwaka jana.
Hii ni mara ya kwanza kwa klabu hiyo yenye maskani yake Old Trafford kutoka nje ya tano bora katika miaka 29 tangu orodha ya Deloitte Money League ilipoanza kutolewa.
Kwa kuwa Man United imecheza mechi 20 tu za nyumbani msimu huu baada ya kutolewa mapema kwenye mashindano yote mawili ya vikombe vya ndani, inatarajiwa kupoteza takribani Pauni 85 milioni kutokana na kupungua kwa idadi ya mechi.
Tim Bridge wa Deloitte alisema: “Kama ungerudi nyuma miaka 10 au 15 na kuangalia mapato ya Manchester United siku za mechi, walikuwa ndio wanaongoza. Uwezo wao wa kuzalisha mapato makubwa, ulikuwa kipimo ambacho kila klabu ilikiangalia. Sidhani kama hali hiyo bado ipo."
“Fursa bado ipo kwa Manchester United. Bila shaka bado ni moja ya chapa kubwa zaidi za soka duniani na inaweza kutumika kikamilifu kuzalisha mapato makubwa."
Kwa upande mwingine, Liverpool baada ya msimu wao wa ubingwa chini ya Arne Slot, mapato yao yameongezeka kwa Pauni 106 milioni hadi Pauni 729 milioni na sasa imeshika nafasi ya tano kwenye orodha hiyo.
Manchester City pia ilipata pigo kidogo, mapato yao yakishuka kwa Pauni 7 milioni wakipata Pauni 723 milioni kutoka Pauni 730 milioni, hali iliyowafanya kushuka kutoka nafasi ya pili mwaka jana hadi ya sita kwa sasa.
Hiyo imetokea baada ya kumaliza ligi nafasi ya tatu na kutolewa kwenye hatua ya 16 bora ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu uliopita.
Arsenal, imepanda kutoka nafasi ya 10 hadi ya saba, mapato yao yakiongezeka karibu kwa asilimia 15 kutoka Pauni 624 milioni hadi Pauni 717 milioni ikiwa ni baada ya kufika nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na kupata takribani Pauni 99 milioni kutokana na zawadi za Uefa.
Liverpool ndiyo klabu pekee ya Ligi Kuu England iliyo kwenye tano bora ya mapato, huku Real Madrid ikiwa ya kwanza kuvunja rekodi ya kufikisha zaidi ya Pauni 1 bilioni ikifuatiwa na Barcelona, Bayern Munich na PSG.
Takwimu hizo pia zinaonyesha baadhi ya timu zilifaidika na mfumo mpya wa Ligi ya Mabingwa Ulaya na mikataba mipya ya matangazo ya televisheni iliyoanzishwa msimu uliopita.
Tottenham Hotspur, ambayo bado wako nafasi ya tisa, iliona mapato yao yakiongezeka kwa Pauni 52 milioni kutoka Pauni 536 hadi Pauni 587 milioni, Chelsea ambayo imeshika nafasi ya 10, ilikusanya jumla ya mapato ya pauni 510 milioni.
Vilevile, Bridge aliongeza:"Matokeo ya uwanjani bado ndiyo sababu kuu inayofanya klabu kupanda hadi ngazi za juu za orodha hii."
MAPATO YA KLABU 20 MWAKA 2025
1. Real Madrid Pauni 1 bilioni
2. FC Barcelona Pauni 974.8 mil
3. Bayern Munich Pauni 860.6 mil
4. Paris Saint-Germain Pauni 837 mil
5. Liverpool Pauni 836.1 mil
6. Manchester City Pauni 829.3 mil
7. Arsenal Pauni 821.7 mil
8. Manchester United Pauni 793.1 mil
9. Tottenham Hotspur Pauni 672.2 mil
10. Chelsea Pauni 584.1 mil
11. Inter Milan Pauni 537.5 mil
12. Borussia Dortmund Pauni 531.3 mil
13. Atlético de Madrid Pauni 454.5 mil
14. Aston Villa Pauni 450.2 mil
15. AC Milan Pauni 410.4 mil
16. Juventus Pauni 410.7 mil
17. Newcastle United Pauni 398.4 mil
18. VFB Stuttgart Pauni 296.3 mil
19. SL Benfica Pauni 283.4 mil
20. West Ham United Pauni 276 mil