Chelsea yatua kwa Gianluigi Donnarumma
Muktasari:
- Donnarumma, alionyesha kiwango bora sana kwa msimu uliopita 2024-25, ambapo alicheza mechi 12 bila ya kuruhusu bao na akaisaidia PSG kushinda mataji matatu makubwa.
KUTOKANA na kiwango kibovu alichoonyesha kipa wao Roberto Sanchez, kocha wa Chelsea amewasilisha jina la kipa wa Paris St-Germain na timu ya taifa ya Italia, Gianluigi Donnarumma, akihitaji asajiliwe katika dirisha hili.
Donnarumma, alionyesha kiwango bora sana kwa msimu uliopita 2024-25, ambapo alicheza mechi 12 bila ya kuruhusu bao na akaisaidia PSG kushinda mataji matatu makubwa.
Kiwango hicho amekiendeleza pia hata kwenye mashindano ya Kombe la Dunia la Klabu yanayoendelea huko Marekani, ambapo hadi sasa ameruhusu bao moja tu katika mechi tano.
Hata hivyo, kwa mujibu wa gazeti la L’Equipe, uamuzi wowote juu ya kusalia au kuondoka utasubiri hadi mashindano hayo Kombe la Dunia la Klabu yatakapomalizika.
Kwa upande wa mchezaji mwenyewe, Donnarumma tayari ametangaza hadharani kuwa anataka kubaki PSG licha ya timu nyingi kubwa za Ulaya kuonyesha nia ya kumsajili.
Hata hivyo, ikiwa atabadilisha mawazo Chelsea itatakiwa kutoa pesa nyingi ili kumnunua kutokana na thamani yake kwa sasa sokoni na hadi sasa haijajulikana PSG ni kiasi cha ada watakachohitaji ili kumuuza Donnarumma ambaye mkataba wake unamalizika mwakani.
Hugo Ekitike
NEWCASTLE imerudi tena katika vita ya kumsajili mshambuliaji wa Eintracht Frankfurt na timu ya taifa ya Ufaransa, Hugo Ekitike, mwenye umri wa miaka 23, na ina matumaini makubwa ya kuishinda Liverpool katika vita hiyo. Awali Ekitike alikuwa akihitajika na Arsenal lakini timu hiyo ilirudi nyuma baada ya staa huyo kudai kuwepo kwa kipengele kinachoelezea ni kiasi gani kitahitajika ili kuvunja mkataba wake muda wowote atakapohitaji kuondoka.
Douglas Luiz
WEST Ham ipo kwenye mazungumzo kwa ajili ya kumsajili kiungo wa zamani wa Aston Villa, Douglas Luiz kutoka Juventus, katika dirisha hili. Mbrazil huyo mwenye umri wa miaka 27, hajaonyesha kiwango bora sana akiwa na Juve kwa msimu uliopita na hata yeye anatamani kupata changamoto mpya sehemu nyingine. Mkataba wake na vigogo hao unatarajiwa kumalizika mwaka 2026.
Luis Diaz
VIGOGO wa Barcelona wanaendelea kufanyia kazi dili la winga wa Liverpool na timu ya taifa ya Liverpool, Luis Diaz, mwenye umri wa miaka 28, na lile la mshambuliaji wa Manchester United na timu ya taifa ya England, Marcus Rashford, mwenye umri wa miaka 27, lakini hawatofanya haraka kukamilisha usajili wao. Diaz ambaye mkataba wake wa sasa unatarajiwa kumalizika mwaka 2027, pia anahusishwa na Bayern Munich.
Emiliano Martinez
IMEFICHUKA kuwa Manchester United bado inawasiliana na Aston Villa juu ya kumnunua kipa wa timu hiyo Emiliano Martinez katika dirisha hili lakini hadi sasa bado hawajafikia makubaliano yoyote juu ya ada ya uhamisho. Kipa huyo wa kimataifa wa Argentina aliandika ujumbe uliotafsiriwa kuwa ni kuagana na Villa na tangu wakati huo Man United na timu kadhaa za Saudi Arabia zimekuwa zikitajwa kumhitaji.
Ethan Nwaneri
MABOSI wa Arsenal wamepiga hatua katika mazungumzo ya mkataba mpya na wawakilishi wa kiungo wao raia wa England mwenye umri wa miaka 18, Ethan Nwaneri. Arsenal imeingia katika mazungumzo na wawakilishi wa Nwaneri kwa sababu kumekuwa na timu kibao zinazomnyemelea na mbaya zaidi ni kuwa mkataba wake unatarajiwa kumalizika mwisho wa msimu ujao.
Christopher Nkunku
BAYERN Munich bado inamfuatilia mshambuliaji wa Chelsea na timu ya taifa ya Ufaransa, Christopher Nkunku kwa ajili ya kumsajili katika dirisha hili. Hata hivyo, hadi sasa Bayern bado haijawasilisha ofa yoyote kwa ajili ya kumsajili kwani inataka kuona wachezaji ambao itaachana nao kabla ya kufanya uamuzi wa kumnunua.
Rodrygo
LIVERPOOL bado inahitaji saini ya winga wa Real Madrid, Rodrygo katika dirisha hili baada ya timu yake kuweka wazi kuwa ipo tayari kumwachia katika dirisha hili. Rodrygo mwenye umri wa miaka 24, bado anatamani kuendelea kusalia barani Ulaya licha ya uwepo wa ofa za Saudi Arabia. Mkataba wake wa sasa unatarajiwa kumalizika mwaka 2028.