Barcelona yafuatilia mkataba wa Harry Kane
Muktasari:
Kane ameweka kipaumbele katika kutatua suala la mustakabali wake na mabingwa hao wa Ujerumani, ambako amezoea maisha na anaendelea kuwa sehemu muhimu ya timu hiyo.
BARCELONA, HISPANIA: BARCELONA inafuatilia kwa karibu mazungumzo yanayoendelea kuhusu mkataba mpya wa mshambuliaji wa Bayern Munich na nahodha wa England, Harry Kane.
Kane ameweka kipaumbele katika kutatua suala la mustakabali wake na mabingwa hao wa Ujerumani, ambako amezoea maisha na anaendelea kuwa sehemu muhimu ya timu hiyo.
Mazungumzo yanaendelea kuhusu muda wa mkataba mpya wa mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 33.
Inaelezwa kuwa Kane anataka mkataba wa miaka mitatu. Kama ilivyoripotiwa na Daily Mail Sport mwanzoni mwa majira haya ya kiangazi, Barcelona tayari imeonyesha wazi nia yake ya kumsajili.
Al Hilal pia inamtaka Kane, licha ya klabu hiyo ya Saudi Arabia kuendelea kumfuatilia mshambuliaji wa Aston Villa, Ollie Watkins.
Kane sasa ameingia kwenye miezi 12 ya mwisho ya mkataba wake wa miaka minne alioutia saini na Bayern Munich baada ya kujiunga na klabu hiyo kutoka Tottenham kwa ada ya pauni 86.4 milioni mwaka 2023.
Msimu uliopita, Kane alifunga mabao 61 katika mechi 51 kwenye mashindano yote akiwa na Bayern, huku kikosi cha Vincent Kompany kikifanikiwa kutwaa ubingwa wa ligi pamoja na kombe.
Kane amesema:
“Kwa kweli tulisema tunataka kuzungumza baada ya Kombe la Dunia na baada ya likizo yangu. Kwa hiyo sijui hasa ni lini, lakini wataanza wiki hii, wiki ijayo... tutaanza mazungumzo hayo.
“Kama nilivyosema hapo awali, tuko watulivu. Nafikiri wao pia wako watulivu kuhusu hali hiyo.
“Kwa kweli sasa ndiyo wakati wa kuanza kuzungumza, kwa sababu zimebaki mwaka mmoja tu. Hilo ni muhimu. Lakini pande zote mbili zimetulia, na nina uhakika kutakuwa na mazungumzo wiki hii au wiki ijayo.”
Barcelona inaendelea kuchunguza chaguo mbalimbali kwenye soko la usajili wakati Atletico Madrid ikiendelea kung’ang’ania kumbakisha mchezaji anayelengwa zaidi na Barcelona, Julian Alvarez.