Yamal amnunulia demu gari, mama aibuka
Muktasari:
- Akiwa mapumzikoni, inadaiwa kiungo huyo mwenye umri wa miaka 19 alimfanyia sapraizi mpenzi wake kwa kumnunulia gari aina ya Mercedes-Benz lenye thamani ya zaidi ya Sh300 milioni za Tanzania.
KIUNGO mshambuliaji wa Barcelona na timu ya taifa ya Hispania, Lamine Yamal yupo mapumzikoni Saint-Tropez, Ufaransa, akila bata na mpenzi wake, Inés García, kabla ya kuanza maandalizi ya msimu mpya wa Ligi Kuu Hispania.
Akiwa mapumzikoni, inadaiwa kiungo huyo mwenye umri wa miaka 19 alimfanyia sapraizi mpenzi wake kwa kumnunulia gari aina ya Mercedes-Benz lenye thamani ya zaidi ya Sh300 milioni za Tanzania.
Baada ya picha hizo kusambaa mitandaoni, mama yake Lamine Yamal, Sheila Ebana, alizungumza kuhusu umuhimu wa mwanawe kuwa makini na matumizi ya fedha kutokana na umri wake mdogo na umaarufu alioupata mapema.
Ebana amesema amekuwa makini kumsaidia Lamine Yamal kuwa na nidhamu katika matumizi ya fedha, jambo analoamini ni changamoto kubwa kwa vijana. “Kila mara namwambia abaki kuwa yeye mwenyewe, aendelee kuwa mnye nyekevu na asiruhusu mafanikio au umaarufu kumpanda kichwani kwa sababu huja na kupotea,” amesema Ebana, kisha akaongeza:
“Lamine Yamal bado ni mdogo. Kuna mambo hawezi kujisimamia mwenyewe, hasa kwenye matumizi ya fedha. Ndiyo maana niko makini kumshauri na kumwelekeza katika upande huo.”
Mama huyo alieleza moja ya maeneo muhimu anayopaswa kupewa ushauri ni namna ya kutumia fedha zake. Amesema katika ulimwengu wa soka, wachezaji vijana wanaopata mafanikio makubwa mapema mara nyingi hukutana na changamoto ya watu wengi kuingia kwenye maisha yao kutokana na umaarufu na uwezo wao wa kifedha.
Kauli hiyo imesambaa mitandaoni na kuwa gumzo, huku baadhi ya mashabiki wakiunga mkono hoja ya Ebana na wengine wakisema Lamine Yamal sasa ni mtu mzima na hana haja ya kusimamiwa kwa karibu.
Wakati hayo yakiendelea, mpenzi wa Lamine Yamal, Inés García, hivi karibuni alitangaza hadharani hajampendea pesa kiungo huyo, bali anampenda kwa dhati.
Inés amekuwa akijibu baadhi ya mijadala kuhusu maisha yake binafsi na Lamine, akisisitiza watu wanaweza kuwa na mitazamo tofauti kuhusu uhusiano wao, lakini yeye anajua sababu zinazomfanya kuwa karibu na mchezaji huyo.
Mwanamitindo huyo amesema hayo baada ya kuzuka kwa taarifa zinazodai kuwa aliyekuwa mpenzi wake wa zamani alimshauri Lamine Yamal kuwa makini, akidai anaamini Inés hayuko kwenye uhusiano huo kwa upendo bali kwa masilahi. Madai hayo yameendelea kujadiliwa mitandaoni, lakini hayajathibitishwa rasmi.