Ruud Gullit afichua sababu ya kutompigia kura Lamine Yamal
Muktasari:
- Lamine Yamal alimshinda kinda wa Ufaransa na klabu ya PSG, Desiré Doué wakati wa hafla ya tuzo ya Ballon d'Or iliyofanyika Septemba 22, 2025.
Gwiji wa zamani wa AC Milan, Ruud Gullit ametaja sababu ya kutomchagua nyota wa Barcelona, Lamine Yamal, katika upigaji kura wa tuzo ya Kopa (mchezaji bora chipukizi duniani), licha ya kinda huyo wa miaka 18 kuwa mpenzi wa wengi na mshindi wa tuzo hiyo 2025.
Lamine Yamal alimshinda kinda wa Ufaransa na klabu ya PSG, Desiré Doué wakati wa hafla ya tuzo ya Ballon d'Or iliyofanyika Septemba 22, 2025.
Gullit, ambaye alimkabidhi Yamal tuzo hiyo, amezungumza na kituo cha Ziggo Sport cha Uholanzi na kufichua kuwa alimchagua Desiré Doué badala ya Lamine Yamal, akieleza kuwa nyota huyo wa Barcelona tayari amefikia kiwango cha juu zaidi na hatakiwi tena kupewa msukumo.
"Kwa nini sikumpigia kura Lamine Yamal kwenye tuzo ya Kopa? Kupiga kura katika tuzo hii kunamaanisha kumpa mchezaji kijana msukumo wa kujiendeleza. Na Yamal hahitaji hilo tena, tayari ameshapita hatua hiyo. Hivyo nilimchagua Desiré Doué," amesema Gullit.
Ushindi huu ulimfanya Lamine Yamal kuwa mchezaji wa kwanza kuwahi kushinda tuzo hiyo zaidi ya mara moja, baada ya pia kuibuka mshindi mwaka 2024.
Desiré Doué alikuwa na msimu mzuri akiwa PSG, akichangia kwa kiwango kikubwa mafanikio ya timu hiyo chini ya kocha Luis Enrique, ambapo walitwaa mataji matatu makubwa (treble) kwa mara ya kwanza.
Doué alifunga mabao 15 na kutoa pasi za mabao 14 katika mechi 54, na kufunga mabao mawili kwenye fainali dhidi ya Inter Milan.
Kwa upande wa Yamal, aliisaidia Barcelona kutwaa La Liga, Copa del Rey, na Supercopa de España.
Pia aling'ara katika timu ya taifa ya Hispania ambayo ilifika fainali ya UEFA Nations League, na alimaliza nafasi ya pili kwenye kura za Ballon d'Or, nyuma ya Ousmane Dembele.