Patrick Vieira kocha mpya Senagal
Muktasari:
- Vieira, aliyezaliwa jijini Dakar na kushinda Kombe la Dunia mwaka 1998 akiwa na timu ya taifa ya Ufaransa, amesaini mkataba wa miaka minne akichukua nafasi ya Pape Thiaw aliyeondoka mwezi uliopita.
Shirikisho la Soka la Senegal (FSF) limemtangaza kiungo na nahodha wa zamani wa Arsenal, Patrick Vieira, kuwa kocha mkuu mpya wa timu ya taifa ya nchi hiyo (Lions of Teranga).
Vieira, aliyezaliwa jijini Dakar na kushinda Kombe la Dunia mwaka 1998 akiwa na timu ya taifa ya Ufaransa, amesaini mkataba wa miaka minne akichukua nafasi ya Pape Thiaw aliyeondoka mwezi uliopita.
Uteuzi huu unakuja kupitia mpango wa muda mrefu unaojulikana kama ‘Patrick Vieira Vision 2030,’ ukilenga kuleta mageuzi makubwa na kujenga muundo wa kiufundi wa hali ya juu unaoendana na matarajio ya soka la nchi hiyo.
Chini ya makubaliano hayo, malengo makuu ya Vieira ni kuifikisha Senegal katika fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) na kuhakikisha inafuzu Kombe la Dunia 2030.
Kocha huyo ana uzoefu mkubwa wa kufundisha soka la ngazi ya juu barani Ulaya na Marekani baada ya kuzinoa timu kama Crystal Palace, OGC Nice, Strasbourg, na Genoa, na huu unakuwa mtihani wake wa kwanza katika usimamizi wa timu ya taifa.