Napoli yaendelea kukomaa na saini ya Jadon Sancho

Muktasari:
- Ripoti zinaeleza mabosi wa Man United wanataka kumtumia staa wao raia wa Uholanzi, Joshua Zirkzee, 24, kama sehemu ya dili hilo ili kutoa pesa kiduchu.
MANCHESTER United inafanya majadiliano ya ndani kuhusu ofa ambayo inaweza kuiandaa kwa ajili ya kumsajili mshambuliaji wa Napoli na timu ya taifa ya Nigeria, Victor Osimhen, mwenye umri wa miaka 26.
Ripoti zinaeleza mabosi wa Man United wanataka kumtumia staa wao raia wa Uholanzi, Joshua Zirkzee, 24, kama sehemu ya dili hilo ili kutoa pesa kiduchu.
Imeelezwa Osimhen alikataa ofa ya kujiunga na Al-Hilal katika dirisha dogo lililopita lililofunguliwa maalum kuzipa nafasi timu zinazoshiriki Kombe la Dunia la Klabu.
Fundi huyu bado anahitaji kuendelea kucheza soka la kiushindani. Timu nyingi zinataka kumsajili lakini zinarudi nyuma kutokana na ada ya uhamisho ambayo ni zaidi ya Pauni 100 milioni. Mkataba wake unaisha 2026. Galatasaray ambayo aliichezea kwa mkopo msimu uliopita inamhitaji jumla pia.
Son Heung-min
TIMU za Saudi Arabia Al-Ahli, Al-Nassr na Al-Qadsiah zimeonyesha nia ya kumsajili mshambuliaji wa Tottenham Hotspur na Korea Kusini, Son Heung-min, mwenye umri wa miaka 32, ambapo kila timu ipo tayari kutoa pauni 34 milioni kama ada ya uhamisho.
Son ambaye amekataa mara kadhaa ofa ya kujiunga na timu hizo za Saudia, mkataba wake wa sasa unatarajiwa kumalizika mwakani.
Cody Gakpo
BAYERN Munich imepanga kumsajili winga wa Brighton na Japan, Kaoru Mitoma, mwenye umri wa miaka 28, na mshambuliaji wa Liverpool na Uholanzi, Cody Gakpo, 26, iwapo itashindwa kuipata nafasi ya kumsajili winga wa kimataifa wa Hispania anayeichezea klabu ya Athletic Bilbao, Nico Williams, 22.
Ripoti zinadai Nico ana asilimia kubwa za kujiunga na Barcelona ambako yuko mshkaji wake mkubwa, Lamine Yamal.
Granit Xhaka
AC Milan imekutana na wawakilishi wa Bayer Leverkusen na kiungo wa kimataifa wa Uswisi, Granit Xhaka, mwenye umri wa miaka 32 kwa ajili ya kujadili uwezekano wa kuipata huduma yake katika dirisha hili.
Xhaka anadaiwa kuonyesha nia ya kujiunga na Milan baada ya kupendezwa na mipango yao kuelekea msimu ujao.
Junior Fripo
REAL Betis imewasilisha ofa ya mkataba wa miaka mitatu kwa beki wa zamani wa Leeds United na Barcelona, Junior Firpo, mwenye umri wa miaka 28, ambaye ameachana na timu yake mwisho wa msimu uliopita.
Licha ya kupokea ofa hiyo, staa huyu wa kimataifa wa Jamhuri ya Dominika hadi sasa bado hajafanya uamuzi ikiwa atajiunga nao au laa.
Tom Heaton
MANCHESTER United imefikia makubaliano ya kumuongeza mkataba wa mwaka mmoja kipa wake raia wa England, Tom Heaton, mwenye umri wa miaka 39, ili aendelee kusalia kwenye kikosi hicho kwa msimu ujao.
Heaton ameongezwa mkataba huo kuendelea kama kipa wa akiba licha ya hapo awali ripoti kudai kuwa alikuwa na mpango wa kutaka kustaafu.
Maxi Aarons
BEKI wa kulia wa Bournemouth na England, Max Aarons, 25, yupo kwenye rada za Rangers, ambayo inahitaji kumsajili katika dirisha hili kwa mkopo. Inaelezwa mabosi wa Bournemouth wapo tayari kumuondoa mchezaji huyu lakini kwa kumuuza moja kwa moja badala ya kumtoa kwa mkopo kama Rangers inavyohitaji.
Axel Tuanzebe
TRABZONSPOR ya Uturuki inahitaji huduma ya beki wa Ipswich Town na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Axel Tuanzebe, mwenye umri wa miaka 27.
Tuanzebe anaripotiwa kutaka kuondoka na tayari ameshawasilisha maombi kwa mabosi wa Ipswich akieleza kuwa anahitaji kutafuta changamoto mpya sehemu nyingine.
Ipswich ipo tayari kumuuza fundi huyu lakini kwa ada isiyopungua pauni 30 milioni.