Mrithi wa Casemiro akaribia kutua Old Trafford
Muktasari:
- Ederson amekuwa mchezaji muhimu kwa Atalanta tangu alipojiunga na klabu hiyo akitokea Salernitana na amecheza mechi 178 katika kipindi cha misimu minne.
MANCHESTER, ENGLAND: KWA mujibu wa mwandishi wa habari za usajili kutoka Italia, Alfredo Pedulla, Manchester United inaongoza mbio za kumsajili kiungo wa Atalanta, Ederson ambaye anatazamwa kama mrithi wa Casemiro.
Pedulla amesema Man United wamekuwa wakimfuatilia Ederson kwa zaidi ya mwaka mmoja na nusu na sasa wanataka kuharakisha dili hilo kwa kutoa zaidi ya Euro 40 milioni ili kuwazidi wapinzani wao.
Ederson amekuwa mchezaji muhimu kwa Atalanta tangu alipojiunga na klabu hiyo akitokea Salernitana na amecheza mechi 178 katika kipindi cha misimu minne.
Casemiro anatarajiwa kuondoka Old Trafford mwishoni mwa msimu huu huku ikitajwa anaweza akatimkia Marekani.
Man United wanajiandaa kuimarisha kikosi chao kwa ajili ya msimu ujao, hasa baada ya kujihakikishia kurejea katika Ligi ya Mabingwa baada ya kukosekana kwa miaka miwili.
Ingawa bado hakuna uamuzi rasmi kuhusu nani ataiongoza timu hiyo msimu ujao, kocha wa muda Michael Carrick ameendelea kupewa nafasi kubwa ya kubaki kutokana na matokeo mazuri aliyopata hadi sasa.
Pamoja na kiwango kizuri kilichoonyeshwa na Casemiro chini ya Carrick, ripoti zinaeleza kiungo huyo wa Brazil bado ana mpango wa kuondoka.
Man United inakabiliwa na ushindani kutoka Atletico Madrid na Arsenal, ambazo pia zimeonyesha nia ya kumsajili kiungo huyo wa kimataifa wa Brazil.
Ripoti zinaeleza Atletico Madrid hawapo tayari kutoa zaidi ya Pauni 39 milioni kwa ajili ya mchezaji huyo, jambo mbalo linaipa nafasi Man United.
Kwa upande wa Arsenal, mkurugenzi wao wa michezo Andrea Berta anaripotiwa kuwa shabiki mkubwa wa Ederson na angependa kumuona akijiunga na kikosi hicho msimu ujao.