Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Messi, Ronaldo wameshindika

MAGWIJI Pict

Muktasari:

  • Bao la Lionel Messi katika ushindi wa Argentina wa mabao 3-2 dhidi ya Misri katika hatua ya 16 bora halikuwasaidia tu mabingwa watetezi kutinga robo fainali, bali pia lilimpunguza pengo dhidi ya Cristiano Ronaldo kwenye orodha ya wafungaji bora wa muda wote.

DALLAS, MAREKANI: USHINDANI wa muda mrefu kati ya Lionel Messi na Cristiano Ronaldo umeendelea kuandika historia mpya katika Kombe la Dunia 2026, huku nyota hao wawili wakiendelea kupigania rekodi ya kuwa mfungaji bora zaidi katika historia ya soka la kulipwa.

Bao la Lionel Messi katika ushindi wa Argentina wa mabao 3-2 dhidi ya Misri katika hatua ya 16 bora halikuwasaidia tu mabingwa watetezi kutinga robo fainali, bali pia lilimpunguza pengo dhidi ya Cristiano Ronaldo kwenye orodha ya wafungaji bora wa muda wote.

Bao hilo lilikuwa la nane kwa Messi katika Kombe la Dunia la mwaka huu, na limeimarisha nafasi yake kama mmoja wa wachezaji bora zaidi wa mashindano hayo.

Kwa mujibu wa takwimu za hivi karibuni, Ronaldo bado anaongoza akiwa amefunga mabao 977 rasmi na kutoa asisti 261 katika mechi 1,330 alizocheza.

Messi anashika nafasi ya pili akiwa na mabao 920 na asisti 415 katika mechi 1,161 pekee.

MAGWI 01

Hivyo, nahodha huyo wa Argentina sasa anabaki nyuma ya Ronaldo kwa tofauti ya mabao 57, licha ya kuwa amecheza mechi 169 chache zaidi kuliko mpinzani wake huyo wa muda mrefu.

Mbio hizo sasa zimeelekezwa kwenye rekodi nyingine kubwa zaidi.

Ronaldo anahitaji mabao 23 pekee kufikisha mabao 1,000 rasmi katika soka la kulipwa, hatua ambayo itamweka katika historia kama mmoja wa wachezaji wa kwanza kufikia mafanikio hayo.

Kwa upande wa Messi, anahitaji mabao 80 zaidi ili kufikia rekodi hiyo.

Ingawa Ronaldo bado anaongoza kwa tofauti nzuri, kiwango bora cha Messi katika Kombe la Dunia kimefanya ushindani huo uendelee kuwa hai.

Akiwa na umri wa miaka 39, nahodha huyo wa Inter Miami anaendelea kuonyesha uwezo wake wa kuamua mechi katika jukwaa kubwa zaidi la soka duniani, huku Ronaldo akishindwa kuisaidia Ureno baada ya kuondolewa katika Kombe la Dunia.

Messi amemtawala Ronaldo katika Kombe la Dunia

Licha ya Ronaldo kuendelea kushikilia rekodi ya mabao mengi zaidi katika historia ya soka la kimataifa na soka la kulipwa, Messi ana takwimu bora zaidi katika historia ya Kombe la Dunia.

Baada ya bao lake dhidi ya Misri, Messi sasa amefikisha mabao 21 katika Kombe la Dunia, wakati Ronaldo akiwa na mabao 11.

Messi pia anaongoza kwa idadi ya asisti katika mashindano hayo akiwa nazo tisa, huku Ronaldo akiwa ametoa mbili pekee.

MAGWI 02

Tofauti kubwa zaidi kati ya wawili hao ni mafanikio ya kutwaa Kombe la Dunia.

Messi alitimiza ndoto yake mwaka 2022 baada ya kuiongoza Argentina kutwaa taji hilo nchini Qatar, mafanikio yaliyomweka rasmi miongoni mwa wachezaji wakubwa zaidi kuwahi kutokea.

Kwa upande wa Ronaldo, mafanikio yake makubwa zaidi katika Kombe la Dunia yalikuwa mwaka 2006 nchini Ujerumani, ambapo Ureno ilifika nusu fainali lakini ikashindwa kutinga fainali.


Rekodi za kimataifa zinaendelea kuandikwa.

Ronaldo bado ndiye kinara wa mabao katika historia ya soka la kimataifa kwa wanaume akiwa na mabao 146 akiwa na jezi ya Ureno.

Messi anashika nafasi ya pili akiwa na mabao 125 kwa Argentina, baada ya kumpita mshambuliaji wa zamani wa Iran, Ali Daei.

Takwimu za ufanisi nazo zinaonyesha ubora wa Messi.

Nyota huyo wa Argentina anahusika moja kwa moja katika bao la timu yake, kwa kufunga au kutoa asisti, wastani wa kila dakika 90.

Kwa upande wa Ronaldo, anahusika katika bao la Ureno wastani wa kila dakika 121.

MAGWI 03

Katika ngazi ya klabu, wote wawili wameandika historia.

Messi alitwaa mataji kadhaa ya Ligi ya Mabingwa Ulaya akiwa Barcelona kabla ya kucheza Paris Saint-Germain na baadaye Inter Miami.

Ronaldo ametwaa mataji ya ligi nchini England, Hispania na Italia pamoja na kushinda Ligi ya Mabingwa Ulaya mara tano.

Kwa pamoja, mastaa hao wameshinda jumla ya tuzo 13 za Ballon d'Or na wametawala soka la dunia kwa karibu miongo miwili, wakivunja rekodi ambazo awali zilionekana haziwezi kufikiwa.

Ingawa wote wawili wanakaribia kufunga pazia la safari zao za soka, mbio za kuandika historia bado hazijaisha.

Kila bao watakalofunga katika sehemu iliyobaki ya Kombe la Dunia 2026 litakuwa na uzito mkubwa.

Ronaldo anawania kuwa mchezaji wa kwanza kufikisha mabao 1,000 rasmi katika historia ya soka la kulipwa, huku Messi akiendelea kupunguza pengo na kuimarisha hoja za wengi wanaomwona kuwa mchezaji bora zaidi kuwahi kutokea duniani.

Iwapo mmoja wao atafikia rekodi hiyo kabla ya kustaafu bado ni suala la kusubiri, lakini jambo moja ni la uhakika, ushindani kati ya Messi na Ronaldo unaendelea kuandika historia kila wanapoingia uwanjani.