Mechi mbili za kibabe Ligi Kuu Bara
Muktasari:
- Mchezo wa mapema utakuwa pale Uwanja wa Majaliwa, Lindi na Namungo itaikaribisha Fountain Gate, mechi utakaoanza saa 12:00 jioni, wenyeji wakitafuta ushindi wa pili.
LIGI Kuu Bara inaendelea leo na viwanja viwili tofauti nyasi zake zitakuwa kwenye joto kwa timu nne kuwania pointi tatu.
Mchezo wa mapema utakuwa pale Uwanja wa Majaliwa, Lindi na Namungo itaikaribisha Fountain Gate, mechi utakaoanza saa 12:00 jioni, wenyeji wakitafuta ushindi wa pili.
Namungo ilianza ligi kwa kupoteza nyumbani dhidi ya bingwa mtetezi, Yanga kwa mabao 3-1, lakini ikafanikiwa kubadili matokeo kwa kuichapa Geita Gold bao 1-0, ushindi ambao utatumika kama silaha wakati wakikutana na Fountain.
Fountain nayo ilitangulia kupoteza ugenini dhidi ya Singida Black Stars kwa mabao 3-0, lakini nayo ikabadili matokeo yake kwa ushindi wa bao 1-0 nyumbani dhidi ya Mashujaa na timu zote mbili zitakutana kwenye mechi ya tatu zikiwa zimetoka kupata ushindi.
Kocha wa Namungo, Juma Mgunda akizungumzia mechi hiyo, amesema: “Haitakuwa mechi rahisi, Fountain Gate ni timu nzuri ambayo inatoka kushinda kama sisi lakini tumejiandaa kukutana na ugumu ili tuweze kupata ushindi.”
Kocha wa Fountain Gate, Fred Felix Minziro, amesema: “Tunakwenda kucheza mchezo wetu wa tatu, kila mmoja anajua namna Namungo inafundishwa na kocha mzoefu, timu yake inakuwa na nguvu kubwa inapokuwa nyumbani, tupo tayari kutumia mbinu zetu kupata kutafuta ushindi.”
Baada ya mchezo huo, macho yatahamishiwa Uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma ambapo kuanzia saa 2:30 usiku wenyeji Dodoma Jiji wataikaribisha wabishi Polisi Tanzania, ambayo imerudi Ligi Kuu kwa kishindo kikubwa.
Dodoma Jiji haijafanya vizuri kwenye mechi zake mbili za kwanza ikianza msimu kwa sare ugenini ya bao 1-1 dhidi ya Pamba Jiji kisha kwenda kupoteza ugenini kwa mabao 2-0 mbele ya Mbeya City.
Kocha wa Dodoma Jiji, Vincent Mashami, amesema: “Tunarudi nyumbani baada ya kucheza mechi mbili za ugenini, kuna mambo hayakuwa sawa na kuna mengine tulikuwa sawa, tunahitaji matokeo mazuri ili kurudisha morali ya timu lakini tunajua hautakuwa mchezo rahisi.”
Polisi Tanzania imerudi Ligi Kuu msimu huu ikianza msimu ikigoma kupoteza mbele ya matajiri wa Chamazi, Azam FC kwa sare ya bao 1-1, kisha ikainyoa JKT Tanzania kwa mabao 2-0.
Kocha wa Polisi Tanzania, Mbwana Makata, akizungumzia mechi hiyo ambayo itakuwa ya kwanza ugenini, amesema: “Siku zote sio rahisi kucheza ugenini hasa unapokutana na timu ambayo inatafuta ushindi, tulianza vizuri lakini tunataka kuendelea kufanya vizuri.”