Masikini! Musiala aanguka uwanjani
Muktasari:
- Musiala, mwenye umri wa miaka 23, alianza kuonekana akiyumba na kuchanganyikiwa muda mfupi baada ya kufunga bao la tatu la Bayern katika ushindi wao wa mabao 3-1.
MUNICH, UJERUMANI: KIUNGO Jamal Musiala aliwaacha mashabiki wa Bayern Munich wakiwa na hofu baada ya kuanguka uwanjani kutokana na joto kali wakati timu hiyo ilipocheza mechi ya kirafiki ya kujiandaa na msimu mpya dhidi ya RB Leipzig.
Musiala, mwenye umri wa miaka 23, alianza kuonekana akiyumba na kuchanganyikiwa muda mfupi baada ya kufunga bao la tatu la Bayern katika ushindi wao wa mabao 3-1.
Winga huyo alifunga bao hilo dakika ya 81 baada ya kupokea pasi kutoka kwa Ismael Saibari, ambaye dakika mbili baadaye aliona Musiala akianza kupoteza nguvu na kukimbia kumuwahi kabla hajaanguka vibaya.
Musiala alionekana akiwa hana nguvu na mwenye kuyumba wakati akisubiri mchezo uendelee, huku joto la nyuzi 33 likiwa limeonekana kumletea usumbufu mkubwa.
Muda mfupi baadaye alianza kupoteza mlingano na kuanguka taratibu, huku Saibari pamoja na Joshua Kimmich wakimsaidia. Madaktari waliingia haraka uwanjani na kuanza kumpatia matibabu huku mashabiki waliokuwa Allianz Arena wakitazama kwa wasiwasi.
Musiala alilazwa chini kwa muda akipatiwa matibabu huku wachezaji wenzake wa Bayern wakimzunguka.
Hata hivyo, hofu ilipungua baada ya madaktari kuonyesha ishara ya dole gumba kuthibitisha kuwa hali yake ilikuwa imetulia. Musiala alisaidiwa kutoka uwanjani huku mashabiki wa Bayern wakiimba jina lake.
Mashabiki wa Bayern sasa watakuwa na hamu ya kumuona Musiala akiwa fiti kabla ya msimu mpya kuanza, hasa baada ya kiungo huyo kukumbwa na majeraha makubwa ya mguu katika maandalizi ya msimu uliopita yaliyomuweka nje kwa zaidi ya miezi sita.
Kutokana na jeraha hilo, Musiala alicheza mechi 15 pekee za Ligi Kuu msimu uliopita.
Katika mchezo huo dhidi ya Leipzig, Bayern ilianza kwa kuongoza baada ya Luis Diaz kufunga bao la mapema, kabla Brajan Gruda, anayekipiga kwa mkopo kutoka Brighton, kusawazisha dakika ya 53.
Nathaniel Brown na Musiala walifunga mabao yaliyofuata na kuipa Bayern ushindi wa mabao 3-1 pamoja na kutwaa taji la Telekom Cup.