Prime
Sayansi kwa Yao Kouassi na Yanga ni nyepesi na imefanya kazi
ILE mechi ya watani pale Unguja imeangaliwa kwa jicho la kawaida tu. Lakini kuna mambo mengi ambayo tumeyasahau na kujifanya tumeyazoea wakati ni mambo mapya katika mpira wetu.
Yao Kouassi Attohoula anaweza kuwa alikuwa mchezaji wa pili bora uwanjani nyuma ya Maxi Nzengeli. Miaka kadhaa nyuma Yao angekuwa nyumbani akitazama mechi hiyo kama mchezaji huru. Si ajabu angekuwa ameanzisha biashara ya duka Kibaha.
Kuna sayansi ya kawaida wale ‘wahuni’ wa Yanga wakiongozwa na Hersi Said inabidi wasifiwe. Namna ambavyo walifanya mambo mawili kumrudisha Yao uwanjani. Aliumia na kukaa nje karibu msimu mzima uliopita.
Alirudi mwishoni. Jina lake liliondolewa katika orodha ya wachezaji ambao wangeiwakilisha Yanga katika mechi za ndani na nje ya nchi. Tumetoka mbali. Zamani ukiona mchezaji anakaa nje msimu mzima ujue ana majeraha ambayo yanahitimisha maisha yake ya soka.
Ni majeraha ambayo yalikuwa hayawezi kutibika katika hospitali zetu kumrudisha uwanjani. Pia ni majeraha ambayo klabu zetu zisingeweza kumpeleka mchezaji nje ya nchi. Wangewezaje kumpeleka mchezaji nje ya nchi wakati klabu zenyewe zilikuwa zinaacha madeni hadi ‘Guest house’?
Klabu zenyewe zilikuwa zinaendeshwa na viingilio vya getini. Unawezaje kwenda kumtibu mchezaji nje ya nchi? Wachezaji wengi wa zamani maisha yao ya soka yalihitimishwa na majeraha ambayo yangeweza kuwarudisha uwanjani.
Miaka imekwenda na leo tupo katika sayansi nyingine ya kawaida tu ambayo kina Hersi wameenda nayo kumrudisha Yao uwanjani. Kwanza kabisa walijua ni ngumu kumpata Yao mwingine kwa urahisi katika soka la Afrika.
Kina Yao wanapatikana zaidi katika nchi za Kiarabu. Vinginevyo kabla yake pale Yanga alikuwepo Djuma Shaban ambaye alisajiliwa kwa mbwembwe kutoka Congo lakini hakuwa na maajabu sana.
Ndiyo maana Yanga walitumia akili ya kawaida tu ya kuendelea kumlipa Yao kwa sababu walijua ni ngumu kumpata Yao mwingine. Ili mradi wanajua ubora wake pindi anapokuwa uwanjani basi ni bora kujishikiza na Israel Mwenda pamoja na Shomari Kibwana.
Zamani hatukuweza kutumia sayansi hii ya kawaida tu. Na si ajabu Yanga wangeweza kwenda sokoni na kumnunua mlinzi mwingine wa kulia wa kigeni ambaye angewagharimu pesa nyingi na ambaye si ajabu asingekuwa na uwezo wa Yao.
Tunachokiona kwa sasa ni ukweli Yanga wanavuna uvumilivu wao kwa Yao. Kilichobaki pia ni kuangalia kama Yao mwenyewe atakuwa na ubinadamu wa kuishukuru Yanga kwa walichomfanyia. Kumtibu, kumlipa mshahara wake wakati hachezi na kumsubiri bila ya nafasi yake kumchukua mchezaji mwingine wa kigeni.
Sayansi hiyo pia inaendelea kutumika kwa Clement Mzize. Zamani mchezaji kama Mzize jina lake lingeondolewa katika orodha ya usajili. Angerudi zake Iringa kuendelea na biashara yake ya kuendesha bodaboda. Shughuli ingeishia hapo. Kusingekuwa na habari za kupelekana Afrika Kusini kwa ajili ya matibabu.
Mchezaji mwingine ambaye nataka kujua kama sayansi ya kisasa inaweza kufanya ni Pacome Zouzoua. Alivunjika vibaya katika pambano la mwisho la msimu dhidi ya JKT Tanzania. Naungana na mashabiki wengi wa kizazi kipya ambao hawajawahi kumuona mchezaji akivunjika vile nchini. Yanga wameondoa jina lake katika usajili wa msimu huu.
Pacome anaweza kurudi na kuwa yule yule? Ni swali ambalo wengi tunajiuliza. Kule nje tumewahi kuwaona wachezaji wakiwa wamevunjika hivyo. Wachezaji wawili wa Arsenal kwa nyakati tofauti waliwahi kuvunjika kiasi kile. Eduardo da Silva na Aaron Ramsey.
Kwa matibabu ya kisasa ya kule walipona na kurudi uwanjani. Huku kwetu tunasubiri kuona kama sayansi hii inaweza kufanya kazi. Tunasubiri kuona kama Pacome anaweza kupona na kuwa yule yule.
Wakati mwingine katika majeraha ya Pacome tatizo sio kupona. Tatizo ni kurudi tena uwanjani ukiwa unajiamini na kucheza bila ya hofu katika kiwango kile kile cha zamani. Nadhani Yanga watakuwa wanasubiri kuona hilo.
Tukirudi kwa Yao kuna jambo ambalo vijana wengi wa Kitanzania wanaocheza nafasi yake wanapaswa kujifunza kutoka kwake. Kipaji kipo wazi katika miguu yake. kitu kinacholeta tofauti zaidi ni uwezo wake mkubwa wa kujiamini na kucheza kwa kujituma zaidi akiwa anatumia nguvu na stamina.
Katika pambano hili lililopita dhidi ya mtani Yao alikuwa kila kitu katika upande wa kulia. Alikaba, alimiliki mpira, alishambulia. Kuanzia nyuma kipa Djigui Diara alikuwa anamtazama zaidi yeye katika kuanzia mashambulizi. Jamaa ni bonge la beki.
Hapo hapo unawauliza vijana wa Kitanzania wanaocheza nafasi yake huku wakiwa wanatamani kwenda kucheza soka la kulipwa Ulaya. Wajiulize, kama Yao anacheza hapa nchini na hayupo hapa itawezekana vipi wao wawe hapa? Ina maana wajitume mara mbili zaidi yake. Pia labda waisubiri bahati maana kuna wakati huwa inafanya kazi.
Wakati tukitafakari hilo pia tunaweza kutumia nafasi hii kutafakari mustakabali wa timu yetu ya taifa. Fikiria mchezaji kama Yao hayupo katika timu yake ya taifa na sidhani kama anafikiriwa.
Yao angekuwa wetu angekuwa na nafasi ya kudumu katika kikosi cha Taifa Stars. Bahati mbaya sio wa kwetu lakini hapo hapo timu yake ya taifa haimtumii. Unadhani tu kukisia namna gani safari ya timu yetu ya taifa ilivyo ndefu. Tusifichane. Tunao wachezaji wengi kama yeye hapa nchini. Hata Rushine de Reauck angekuwa tegemeo hapa kwetu lakini Bafana Bafana haitwi.