Mapumziko ni ahueni au majanga kwa makocha EPL
Muktasari:
- Wiki tatu ni muda mrefu katika soka, hasa kwa kocha anayehangaika kupata matokeo mazuri. Hadi sasa msimu huu, makocha wawili tayari wamepoteza ajira zao, Paul Heckingbottom wa Preston North End na Michael Duff wa Wycombe Wanderers.
LONDON, ENGLAND: NI ahueni au majanga kwa Michael Carrick, Alvaro Arbeloa na makocha wengine wanaokabiliwa na presha, huku mapumziko ya wiki tatu yakitoa nafasi kwa klabu kufanya mabadiliko.
Wiki tatu ni muda mrefu katika soka, hasa kwa kocha anayehangaika kupata matokeo mazuri. Hadi sasa msimu huu, makocha wawili tayari wamepoteza ajira zao, Paul Heckingbottom wa Preston North End na Michael Duff wa Wycombe Wanderers.
Hata hivyo, makocha wengine wengi wanaweza kujikuta wakitazama nyuma ya mabega yao wakati wa kuelekea mapumziko marefu ya kimataifa ya FIFA.
Miongoni mwao ni makocha wa Fulham na Manchester United, waliokutana jana Jumapili kwenye Uwanja wa Craven Cottage, katika mchezo wa mwisho kabla ya wachezaji kuondoka kwenda kujiunga na timu zao za taifa.
Kwa Arbeloa, kocha wa Fulham aliyeteuliwa msimu huu, baada ya kuiongoza Real Madrid katika mechi 28 pekee katika kipindi cha pili cha msimu uliopita.
Lakini baada ya kushindwa kushinda mchezo wowote na kupoteza mara tatu katika mechi zake nne za kwanza za Ligi Kuu England, presha tayari imeanza kumwandama. Pia, taarifa kuhusu kutoridhika kwa baadhi ya wachezaji wa Fulham, zikichochewa na shughuli zao kwenye mitandao ya kijamii, zimeongeza maswali kuhusu hali ya ndani ya kikosi hicho.
Hali si tofauti sana kwa Carrick wa Manchester United, hasa baada ya timu yake kutolewa katika Kombe la Ligi na Brighton kwa kufungwa mabao 3-2 Jumatano iliyopita.
Ilikuwa mara ya kwanza tangu mwaka 1976 kwa Manchester United kuongoza mchezo wa nyumbani kwa tofauti ya mabao mawili na hatimaye kupoteza, baada ya Tottenham kufanya hivyo miaka 50 iliyopita.
Matokeo hayo yalifuatia kipigo cha mabao 1-0 dhidi ya Manchester City iliyokuwa na wachezaji 10 uwanjani. Kwa kuzingatia kwamba ushindi wao pekee msimu huu umepatikana dhidi ya Ipswich Town na Sabah, Carrick anahitaji matokeo mazuri.
Lakini si makocha hao pekee wanaoweza kuwa na sababu za kuhofia mustakabali wao.
JE, MAPUMZIKO YA FIFA NI WAKATI WA KUFUKUZA MAKOCHA?
Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, imekuwa nadra kwa klabu ya Ligi Kuu England kumbadilisha kocha mapema kiasi hiki cha msimu, hususan wakati wa mapumziko ya kimataifa.
Hata hivyo, msimu huu unaweza kuwa tofauti kutokana na mapumziko ya kwanza kuwa marefu zaidi, wiki tatu badala ya mbili, huku yakija mapema kuliko ilivyozoeleka.
Kwa miaka ya nyuma, mapumziko ya Septemba yalikuwa yakifanyika mwanzoni mwa mwezi, wakati ambapo klabu zilikuwa zimecheza mechi tatu pekee za ligi.
Katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, makocha wawili tu wameondoka kwenye ajira zao wakati wa mapumziko hayo. Javi Gracia aliondoka Watford mwaka 2019, huku Nuno Espirito Santo akiondoka Nottingham Forest mwaka uliopita.
Hali kama hiyo pia imeonekana katika mapumziko ya Oktoba, ambapo makocha wawili pekee walipoteza ajira zao katika kipindi hicho: Francesco Guidolin wa Swansea mwaka 2016 na Xisco Munoz wa Watford mwaka 2021.
Takwimu hizo zinaonyesha kuwa klabu kwa kawaida hazitumii mapumziko ya kimataifa kufanya mabadiliko ya makocha. Hata hivyo, hilo halimaanishi kuwa makocha wako salama, kwa sababu mabadiliko yanaweza kufanyika kabla au baada ya mapumziko hayo.
Katika misimu 10 iliyopita, makocha tisa walikuwa wameondoka kwenye ajira zao kabla ya mapumziko ya pili ya kimataifa kufika, kipindi ambacho idadi ya mechi za ligi huwa karibu na ilipo sasa.
Kwa hiyo, swali linalobaki ni kama kocha mwingine ataondolewa katika kipindi cha wiki tatu zijazo.
MAPUMZIKO NAFASI YA KOCHA KUJIPANGA UPYA
Kocha wa zamani wa Stoke City, West Bromwich Albion na Middlesbrough, Tony Pulis, anaeleza namna presha inavyoweza kuongezeka kwa makocha wanaoshindwa kupata matokeo.
“Katika kipindi changu, mapumziko ya kimataifa ya Oktoba na Novemba, mapumziko baada ya Krismasi pamoja na mapumziko ya mwanzoni mwa Machi, yalikuwa vipindi muhimu ambavyo kocha anayehangaika kupata matokeo angeweza kupoteza ajira.”
Pulis anaamini mapumziko hayo huipa klabu nafasi ya kumteua kocha mpya na kumpa muda wa kuzoea mazingira ya kazi kabla ya kuanza kuiongoza timu kwenye mechi rasmi.
“Sababu ya klabu kutumia vipindi hivi kufanya mabadiliko ni rahisi kueleweka. Mapumziko yanaipa klabu nafasi ya kumteua kocha mpya, ambaye anaweza kuzoea majukumu yake, kutathmini mazingira ya klabu na benchi la ufundi, pamoja na kupata muda wa kujiandaa kwa mchezo wake wa kwanza.”
Kwa mujibu wa Pulis, mchezo wa kwanza baada ya mapumziko ya Krismasi mara nyingi huwa wa Kombe la FA, jambo linalompa kocha mpya nafasi ya kuiona timu yake kwa karibu na kutambua uwezo wa wachezaji alionao.
Hata hivyo, anasema mapumziko ya Septemba hayapaswi kuchukuliwa kama ishara kubwa ya hatari kwa makocha, kwa kuwa msimu huwa bado katika hatua za mwanzo.
Pulis pia anakosoa muda wa mapumziko marefu katika hatua za mwanzo za msimu, akisema unawaweka makocha na wachezaji katika mazingira magumu.
“Kama timu yako inashinda, unataka kuendelea kucheza. Lakini kama umeanza vibaya, unahitaji muda zaidi wa kurekebisha mambo. Wachezaji kusafiri na uwezekano wa kupata majeraha katika hatua hii ya mapema ya msimu ni jambo lisiloeleweka kwangu.”
MAKOCHA WANAOWEZA KUWA HATARINI
MANCHESTER UNITED – MICHAEL CARRICK
Kwa mujibu wa mchambuzi Simon Stone, mchezo wa Manchester United dhidi ya Fulham hauonekani kuwa wa kuamua hatima ya Carrick katika suala la ajira yake.
Carrick amewahi kusema itakuwa “ujinga” kufikiria kwamba mchezo huo unaweza kuamua mustakabali wake, na Stone anaunga mkono mtazamo huo.
Kocha huyo alipata heshima kubwa msimu uliopita baada ya kuiwezesha Manchester United kufuzu Ligi ya Mabingwa Ulaya, jambo linaloweza kumpa nafasi ya kuvumilia mwanzo mbaya wa msimu huu.
FULHAM – ALVARO ARBELOA
Haijafahamika wazi kiwango cha hatari kinachomkabili Arbeloa, lakini kuna dalili za kutoridhika miongoni mwa baadhi ya wachezaji wa Fulham tangu mwanzo wa msimu.
Mabadiliko makubwa ya kiufundi aliyoyafanya baada ya kuchukua nafasi ya Marco Silva yameifanya timu hiyo kuwa dhaifu katika ulinzi. Hata hivyo, Fulham ilionyesha uimara zaidi katika sare ya bila mabao dhidi ya Liverpool mwishoni mwa wiki iliyopita.
Silva alikuwa ameiongoza Fulham kwa miaka mitano, huku mwenyekiti wa klabu hiyo, Shahid Khan, akiwa amewahi kufanya mabadiliko makubwa ya makocha hapo awali.
Kocha Claudio Ranieri alidumu kwa siku 106 pekee akiwa kocha wa Fulham, wakati Felix Magath alifukuzwa Septemba 2014, ingawa alikuwa ameajiriwa msimu uliotangulia.
TOTTENHAM – ROBERTO DE ZERBI
Matokeo ya Tottenham yameendelea kuwa mabaya, licha ya klabu hiyo kutumia takribani pauni300 milioni kusajili wachezaji wapya.
Hata hivyo, hakuna dalili zinazoonyesha kuwa kocha Roberto de Zerbi yuko kwenye presha, licha ya timu hiyo kushindwa kushinda katika mechi zake sita za mwanzo.
CRYSTAL PALACE – PIERRE SAGE
Pierre Sage amekuwa na mwanzo usioridhisha tangu alipowasili Crystal Palace. Ushindi mmoja pekee katika ligi haujapokelewa vizuri ndani ya klabu, huku ulinzi wa timu hiyo ukiendelea kuonyesha udhaifu tangu kocha huyo wa Ufaransa alipowasili kutoka Lens.
Hata hivyo, klabu imekuwa ikizingatia kutokuwepo kwa washambuliaji muhimu Ismaila Sarr na Jean-Philippe Mateta, ambao wamekosekana kwa sababu mbalimbali.
Ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Lech Poznan katika Europa Ligi Alhamisi ulipunguza presha kwa Sage. Lakini kipigo dhidi ya Leeds kingekuja katika wakati mgumu zaidi kwa kocha huyo.
BURNLEY – NICKY HAYEN
Nicky Hayen aliondoka Genk na kujiunga na Burnley akiwa na jukumu la kuiongoza timu hiyo kurejea Ligi Kuu England mara moja.
Burnley ilianza msimu ikiwa miongoni mwa timu zilizotajwa kuwa na nafasi kubwa ya kupanda daraja, ikiwa nyuma ya West Ham na Wolves kwa mujibu wa matarajio ya awali. Lakini baada ya mechi nane, timu hiyo bado haijapata ushindi.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari Ijumaa, Hayen aliulizwa kuhusu mustakabali wake na akakiri kuwa alikuwa kwenye presha.
WATFORD – ALESSIO DIONISI
Kocha wa Watford mara nyingi huwa hawezi kuwa na uhakika wa usalama wa ajira yake. Alessio Dionisi, aliyeteuliwa msimu huu, amekuwa kocha wa 27 wa klabu hiyo katika kipindi cha takribani miaka 18.
Kipigo dhidi ya Bristol City Ijumaa kiliiacha Watford ikiwa na ushindi mara mbili pekee katika mechi nane za ligi chini ya kocha huyo wa Italia, ambaye aliwahi kuinoa Empoli kabla ya kuhamia England.
Watford ikiwa katika nafasi ya 19 kwenye msimamo wa ligi, ikiwa na tofauti ya pointi tatu dhidi ya eneo la kushuka daraja, haitakuwa jambo la kushangaza iwapo mmiliki Gino Pozzo ataamua kufanya mabadiliko mapema.