Clara: Nina mtihani Marekani
Muktasari:
- Dili la nyota huyo linatajwa kufikia Sh6 bilioni, thamani ambayo sasa inamuweka kwenye presha ya kuthibitisha kuwa fedha hizo zinaendana na uwezo wake uwanjani.
BAADA ya kutambulishwa kwenye kikosi cha Washington Spirit ya Marekani, Mshambuliaji wa Tanzania, Clara Luvanga amesema ana mtihani mgumu wa kuthibitisha thamani yake kwenye ligi hiyo.
Dili la nyota huyo linatajwa kufikia Sh6 bilioni, thamani ambayo sasa inamuweka kwenye presha ya kuthibitisha kuwa fedha hizo zinaendana na uwezo wake uwanjani.
Akizungumza na AzamTv, Clara amesema hilo linamfanya aendelea kuonyesha kiwango kilichomfanya Washington Spirit kuamua kumsajili kwa fedha kubwa kutoka Al-Nassr ya Saudi Arabia.
"Hizo namba zinakuja kutokana na kile ulichokionyesha hivyo natakiwa uendeleze huo ubora. Ni mtihani uliokuja, natakiwa kufanya vizuri ili niendane na thamani iliyopo kwa sababu kuna wachezaji wazuri, lakini hawana thamani hiyo," amesema Clara.
Clara ameingia Washington Spirit baada ya kuonyesha kiwango bora Saudi Arabia ambako msimu uliopita alimaliza akiwa mfungaji bora wa ligi baada ya kufunga mabao 24, jambo lililoongeza thamani yake sokoni na kumfanya aendelee kuvutia klabu mbalimbali.
Sasa changamoto si kuishia kwenye rekodi ya kuwa Mtanzania wa kwanza kucheza Ligi Kuu ya Wanawake Marekani, bali namna atakavyoanza maisha mapya katika mazingira tofauti, ligi tofauti na kikosi kipya kinachohitaji kuelewa uwezo wake ndani ya muda mfupi.
Clara ameongeza kuwa hatua ya kwanza kwake baada ya kufika Washington Spirit ni kuifahamu timu, mazingira yake na zaidi mahitaji ya kocha, kabla ya kuanza kuonyesha kile alichonacho ndani ya uwanja.
"Kwanza ni kufika sehemu ya kazi na kujua sehemu iko vipi na kujua kocha, natakiwa kujua kocha anataka nini na kingine nionyeshe ubora," amesema Clara.