Man United, Amorim kuna jambo haliko sawa
Muktasari:
- Amorim alikataa kabisa uwezekano wa kufanya usajili wa wachezaji Januari hii, siku mbili tu baada ya dirisha kufunguliwa, huku akitoa majibu ya mafumbo wakati ambao ripoti za ndani zinadai kuna fukuto.
MANCHESTER, ENGLAND: UHUSIANO kati ya kocha wa Manchester United, Ruben Amorim, na baadhi ya viongozi wa timu hiyo kwa sasa unadaiwa kuharibika.
Amorim alikataa kabisa uwezekano wa kufanya usajili wa wachezaji Januari hii, siku mbili tu baada ya dirisha kufunguliwa, huku akitoa majibu ya mafumbo wakati ambao ripoti za ndani zinadai kuna fukuto.
Mwishoni mwa mwaka jana, Amorim alinukuliwa akisema kwamba ili kucheza mfumo wa 3-4-3 kamilifu, wanahitaji kutumia pesa nyingi na muda, lakini sasa anaona hilo haliwezekani, hivyo inabidi yeye ndio abadilishe mfumo.
Alipoulizwa kama mkurugenzi wa mpira wa Man United, Jason Wilcox, alikataa maombi yake ya usajili, Amorim alijibu kwa hasira: "Sitaki kuzungumzia hilo. Wewe ni mwerevu sana, hivyo..."
Man United kwa sasa wako nafasi ya sita katika Ligi Kuu, wakiwa sawa na Chelsea kwa pointi, lakini maisha katika ya Old Trafford yanaweza kuwa magumu kutokana na ukosefu wa wachezaji kadhaa muhimu.
Matokeo mabaya ya hivi karibuni na majeraha ya wachezaji muhimu kama kapteni Bruno Fernandes, Mason Mount, na Kobbie Mainoo, yamemwacha Amorim akiwa na uhaba mkubwa wa wachezaji.
Amorim pia anakosa wachezaji watatu ambao wameenda kuwakilisha mataifa yao katika Kombe la Mataifa ya Afrika (AFOCN) ambao ni Bryan Mbeumo, Amad Dialo, na Noussair Mazraoui, pia Harry Maguire na Matthijs de Ligt wanakosekana kutokana na majeraha.
Inaelezwa Mazungumzo kati ya Amorim na viongozi wa klabu yamefanyika wiki hii na taarifa za ndani zinadai wamekataa kumpa fungu la usajili wa wachezaji anaohitaji jambo linalodaiwa kumtia hasira.
Kukataa kutoa fungu la usajili Januari hii, kunaweza kusababisha pia kusitishwa kwa mpango wa kuuzwa na kutolewa kwa mkopo mastaa wengine kama Joshua Zirkzee, Manuel Ugarte na Mainoo.
"Ukitazama kikosi chetu, haiwezekani mtu kuondoka. Lakini nadhani wanapaswa kuzungumza na Jason Wilcox," amesema Amorim alipoulizwa kama wanaweza kumruhusu mchezaji yeyote kuondoka.
Kwa sasa Wilcox ndio anayeendesha shughuli za usajili na utendaji wa timu baada ya kupandishwa kutoka nafasi ya mkurugenzi wa kiufundi hadi mkurugenzi wa michezo baada ya kuondoka kwa Dan Ashworth.