Mac Allister awaamsha Liverpool
Muktasari:
- Mac Allister, ambaye Jumanne alikiri kuwa alikuwa mtu mwenye huzuni kwa kutopatiwa ofa mpya ya mkataba, aligeuka shujaa wa Anfield usiku uliofuata baada ya kupachika bao maridadi la mguu wa kushoto lililoipa Liverpool ushindi huo.
LIVERPOOL, ENGLAND: ALEXIES Mac Allister alitumia miguu yake kuzungumza baada ya malalamiko yake ya kutokupewa mkataba mpya, akifunga bao la ushindi na kuipa Liverpool ushindi wa 2-1 dhidi ya Atletico Madrid katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Mac Allister, ambaye Jumanne alikiri kuwa alikuwa mtu mwenye huzuni kwa kutopatiwa ofa mpya ya mkataba, aligeuka shujaa wa Anfield usiku uliofuata baada ya kupachika bao maridadi la mguu wa kushoto lililoipa Liverpool ushindi huo.
Ushindi huo pia ulimpa Andoni Iraola mwanzo mzuri katika safari yake ya Ligi ya Mabingwa, baada ya kikosi chake kuonyesha uwezo wa kurejea mchezoni kufuatia kuanza vibaya dhidi ya Atletico ya Diego Simeone.
Atletico ndiyo ilianza kwa kasi na kufunga bao dakika ya 17 kupitia Marcos Llorente, ambaye kwa mara nyingine alionyesha kuwa Anfield ni uwanja wake wa bahati.
Julian Alvarez alipata muda wa kutosha kupanga pasi yake na kumtengenezea Llorente nafasi katikati ya ulinzi wa Liverpool. Kiungo huyo aliingia eneo la hatari na kumpiga Alisson kutoka nje kidogo ya boksi.
Llorente, ambaye alikuwa amefunga mabao mawili katika kila moja ya mechi zake mbili zilizopita za Ligi ya Mabingwa dhidi ya Liverpool, aliendelea kuendeleza rekodi yake nzuri kwenye uwanja huo. Hata jina la mbwa wake, “Anfield”, limetokana na kumbukumbu zake dhidi ya Liverpool.
Atletico ilikaribia kuongeza bao la pili wakati Alvarez alipopiga shuti kali kutoka umbali wa takribani mita 23, lakini Alisson alifanya kazi kubwa kwa kuruka na kuliondoa.
Liverpool hata hivyo ilisawazisha dakika tano kabla ya mapumziko.
Milos Kerkez, ambaye alionekana kufanya makosa kwenye bao la Atletico, alifanikiwa kuupata mpira umbali wa takribani mita 36 kutoka lango. Liverpool ikaendelea na shambulizi hilo, Jan Oblak akamzuia Bradley Barcola, lakini wenyeji wakauendeleza mpira.
Cristian Romero alishindwa kuzuia kwa ufanisi kabla ya Ronald Araujo kufanya mguso wa kisigino uliompa Dominik Szoboszlai nafasi ya kumalizia kutoka karibu na lango.
Szoboszlai hakufanya makosa, akafunga na kuufanya ubao wa matokeo kusomeka 1-1 kabla ya mapumziko.
Liverpool ilianza kipindi cha pili kwa nguvu, huku Barcola akipoteza nafasi nyingine baada ya kupewa pasi nzuri na Florian Wirtz.
Hata hivyo, makosa hayo hayakuigharimu Liverpool.
Muda mfupi baadaye, Mac Allister aliibuka na kupiga shuti kali kutoka umbali wa mita 18, likapenya katikati ya msitu wa wachezaji na kumwacha Oblak akiwa hana la kufanya.
Bao hilo lilifanya mashabiki wa Anfield walipuke kwa shangwe, huku Mac Allister akipata jibu bora zaidi kwa uongozi wa klabu kuhusu hatma ya mkataba wake.
Lakini furaha hiyo ilichanganyika na wasiwasi baada ya Barcola, ambaye alikuwa akionekana hatari licha ya kupoteza nafasi kadhaa, kulazimika kutoka uwanjani kabla ya kufikisha dakika 60.
Mshambuliaji huyo alionekana kupata tatizo la misuli baada ya kuanguka bila kuguswa na mchezaji mwingine, jambo lililomlazimisha Iraola kumtoa.
Iraola sasa atakuwa akiiombea hali ya Barcola isiwe mbaya, huku akifarijika na namna kikosi chake kilivyobadilika baada ya nusu saa ya kwanza iliyokuwa ngumu.