Iraola: Mac Allister, Alisson hawauzwi
Muktasari:
- Kauli hiyo inakuja wakati kukiwa na tetesi zinazomhusisha Mac Allister na kuondoka Anfield baada ya kushindwa kuanza mazungumzo ya kuongeza mkataba mpya.
LONDON, ENGLAND: KOCHA wa Liverpool, Andoni Iraola, amesema hana mpango wa kuwauza kiungo Alexis Mac Allister na kipa Alisson Becker, akisisitiza kuwa anataka kuwabakisha nyota wake muhimu kuelekea msimu wa 2026-27.
Kauli hiyo inakuja wakati kukiwa na tetesi zinazomhusisha Mac Allister na kuondoka Anfield baada ya kushindwa kuanza mazungumzo ya kuongeza mkataba mpya.
Kiungo huyo wa kimataifa wa Argentina bado ana miaka miwili katika mkataba wa miaka mitano aliouweka alipojiunga na Liverpool mwaka 2023.
Akizungumza jijini Chicago mwanzoni mwa ziara ya maandalizi ya msimu mpya nchini Marekani, Iraola amesema ni jambo la kawaida kwa klabu nyingine kuwinda wachezaji bora wa Liverpool.
"Alexis amekuwa mmoja wa wachezaji bora wa Liverpool katika miaka ya hivi karibuni na pia amekuwa na Kombe la Dunia zuri. Ni kawaida kuona klabu nyingine zikivutiwa na wachezaji wetu bora," amesema Iraola.
Hata hivyo, alisisitiza kuwa lengo lake si kuuza mastaa bali kuongeza nguvu kikosini.
"Nataka kubaki na wachezaji wangu wazuri. Ninapendelea kusajili wachezaji wapya kuliko kupoteza tulionao."
Alisson bado ni nguzo muhimu
Kipa Alisson Becker, ambaye amebakiza mwaka mmoja katika mkataba wake, amekuwa akihusishwa na kuhamia Juventus, lakini Iraola amesema hana mpango wa kumruhusu kuondoka.
Kocha huyo amesema uzoefu wa Alisson ni muhimu hasa wakati Liverpool ikiendelea kuwapokea wachezaji wapya.
"Nimeridhishwa na hali ya kikosi chetu cha makipa. Alisson ni mmoja wa viongozi ndani ya chumba cha kubadilishia nguo na atatusaidia kuwaongoza wachezaji wapya pamoja na vijana."
Ameongeza kuwa Liverpool bado inawahitaji wachezaji wenye uzoefu kama Virgil van Dijk, Joe Gomez na Alisson ili kuimarisha mshikamano wa kikosi.
Liverpool yatafuta beki
Pamoja na kutaka kuwabakisha nyota wake, Iraola amekiri kuwa Liverpool inahitaji kuongeza beki mmoja au zaidi kabla ya dirisha la usajili kufungwa.
Kocha huyo amesema hali imekuwa ngumu baada ya beki wa kulia Conor Bradley kuumia goti mwezi Januari na kutarajiwa kukaa nje kwa miezi kadhaa zaidi.
"Kama Conor angekuwa fiti, tusingekuwa tunajiuliza maswali haya. Tuna imani naye kwa muda mrefu na tunataka awe beki wetu wa kulia, lakini bado yuko mbali kurejea uwanjani."
Kutokana na hali hiyo, Iraola amesema Liverpool inatafuta suluhisho la kuongeza nguvu eneo la ulinzi.
"Kwa sasa hatuna wachezaji wa kutosha katika safu ya ulinzi, hasa beki wa kati na beki wa kulia. Ndiyo maana tunaendelea kutafuta mchezaji wa kutusaidia katika maeneo hayo."