Dominik Szoboszlai apata dili nono Liverpool
Muktasari:
- Ingawa mkataba huo bado haujawekwa rasmi kwa saini, taarifa zinaeleza kila kitu kiko kwenye hatua za mwisho na Szoboszlai anatarajiwa kuungana na kikosi kitakachosafiri kwenda Marekani kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya.
LONDON, ENGLAND: KIUNGO wa Liverpool, Dominik Szoboszlai, anakaribia kusaini mkataba mpya wa muda mrefu utakaoongeza kwa kiasi kikubwa maslahi yake ndani ya klabu hiyo.
Nahodha huyo wa Hungary amekuwa mmoja wa wachezaji waliokuwa nguzo muhimu kwa Liverpool msimu uliopita na uongozi wa klabu umekuwa kwenye mazungumzo naye kwa muda mrefu kuhusu kumpatia mkataba mpya kama zawadi ya kiwango chake bora.
Ingawa mkataba huo bado haujawekwa rasmi kwa saini, taarifa zinaeleza kila kitu kiko kwenye hatua za mwisho na Szoboszlai anatarajiwa kuungana na kikosi kitakachosafiri kwenda Marekani kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya.
Kiungo huyo alijiunga na Liverpool akitokea RB Leipzig mwaka 2023 na amekuwa mhimili mkubwa wa mafanikio ya timu hiyo. Licha ya ujio wa Florian Wirtz kwa ada kubwa ya pauni 116 milioni, Szoboszlai alipambana na kuthibitisha ubora wake.
Msimu uliopita alicheza nafasi mbalimbali zikiwemo kiungo mshambuliaji, winga, kiungo wa chini na hata beki wa kulia, akifunga mabao 13 na kutoa asisti 12.
Ha bari njema zaidi kwa Liverpool ni kwamba Szoboszlai atakuwa sehemu ya maandalizi yote ya msimu chini ya kocha mpya Andoni Iraola, tofauti na baadhi ya nyota kama Alexis Mac Allister ambaye atajiunga baadaye baada ya majukumu yake ya Kombe la Dunia akiwa na Argentina.