Enzo Maresca achimba mikwara huko Chelsea
Muktasari:
- Madueke, sambamba na mchezaji mwingine Renato Veiga, wote walipigwa chini kwenye kikosi cha Chelsea kilichomenyana na Fulham kwenye Boxing Day.
LONDON, ENGLAND: KOCHA mkuu wa Chelsea, Enzo Maresca amewapiga mkwara mastaa wote wa timu hiyo kwamba wanapaswa kucheza kwa viwango bora baada ya kumuweka kando kwenye kikosi mchezaji Noni Madueke.
Madueke, sambamba na mchezaji mwingine Renato Veiga, wote walipigwa chini kwenye kikosi cha Chelsea kilichomenyana na Fulham kwenye Boxing Day.
Maresca alifichua kwamba wachezaji hao hawakuwa majeruhi bali aliwaweka kando kutokana na sababu za kiufundi. Bosi huyo wa The Blues alimkosoa Madueke kutokana na kile ambacho anakifanya mazoezini na tayari ameshatoa lawama hizo mara mbili tofauti msimu huu.
Wakati kocha huyo wa zamani wa Leicester City, Maresca akifikiria kuwarudisha kwenye kikosi Madueke na Veiga kwenye mchezo wao ujao dhidi ya Ipswich Town utakaofanyika kesho Jumatatu, ametoa onyo kwa mastaa wengine kwamba wanapaswa kuweka juhudi mazoezini. Maresca alisema: “Wakati mwingine ni lazima tuchukua uamuzi na hakuna kingine zaidi ya hicho. Je, atakuwapo kwenye hesabu dhidi ya Ipswich? Ndiyo. Hakuna sababu nyingine ni mambo ya kiufundi tu.”
Kocha wa zamani wa Chelsea, Mauricio Pochettino aliwahi kumlalamikia Madueke msimu uliopita baada ya mchezaji huyo kwenda kufanya starehe wakati alipokuwa majeruhi na baada ya kulumbana na wenzake juu ya nani apige penalti kwenye mechi yao dhidi ya Everton. Maresca naye alimtaka mchezaji huyo kubadilika na kuonyesha uwezo mkubwa kuanzia kwenye uwanja wa mazoezini. Madueke amehusika na mechi 16 kati ya 17 za Ligi Kuu England, akifunga mabao matano na asisti tatu na hajafunga tangu ushindi dhidi ya Southampton.