Calafiori azua hofu Arsenal
Muktasari:
- Beki huyo wa kushoto amekuwa mchezaji muhimu kwenye kikosi cha Arsenal msimu huu akikisaidia kikosi hicho kinachonolewa na Mhispaniola Mikel Arteta kushika usukani wa msimamo wa Ligi Kuu England.
LONDON, ENGLAND: ARSENAL inahaha kwa sasa kijasho kikiwatoka kuhusu ufiti wa beki wake Riccardo Calafiori baada ya Mtaliano huyo kukosa mechi ya nchi yake ya Italia dhidi ya Moldova kwenye mikikimikiki ya kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia 2026.
Beki huyo wa kushoto amekuwa mchezaji muhimu kwenye kikosi cha Arsenal msimu huu akikisaidia kikosi hicho kinachonolewa na Mhispaniola Mikel Arteta kushika usukani wa msimamo wa Ligi Kuu England.
Calafiori ameanzishwa kwenye mechi zote 11 za Ligi Kuu England ilizocheza Arsenal msimu huu, akifunga mara moja na kuasisti mara mbili akitokea kwenye beki ya kushoto.
Staa huyo wa zamani wa Bologna amekuwa mchezaji muhimu katika kikosi cha Arsenal, lakini sasa kumekuwa na wasiwasi mkubwa juu ya maumivu ya nyonga yanayomsumbua.
Calafiori, 23, alijumuishwa kwenye kikosi cha Italia na kocha Gennaro Gattuso, lakini alilazimika kufanya mazoezi kivyake kwenye kambi ya kikosi hicho cha Azzurri huko Florence.
Calafiori alikuwa kwenye hatari ya kukosa mechi ya jana Alhamisi dhidi ya Moldova, huku kikosi cha Italia kikikabiliwa na mechi nyingine muhimu nyumbani dhidi ya Norway, Jumapili.
Italia itatamani sana kuwa na huduma ya beki huyo uwanjani huku taifa hilo likiwa kwenye hatari ya kushindwa kufuzu fainali za Kombe la Dunia.
Kikosi cha Azzurri kipo nyuma kwa pointi tatu dhidi ya vinara Norway na kitalazimika kuingia kwenye mechi za mchujo endapo kama kitashindwa kupata ushindi kwenye mechi zake mbili za mwisho. Calafiori alianzishwa kwenye mechi mbili za mwisho za Italia, iliposhinda 3-1 dhidi ya Estonia na 3-0 dhidi ya Israel.
Alicheza kwa dakika zote 90 katika sare ya 2-2 iliyopata Arsenal dhidi ya Sunderland kwenye Ligi Kuu England kabla ya kupisha mapumziko haya ya mechi za kimataifa.