Barcelona yaendelea kutamani huduma ya Kane kikosini
Muktasari:
- Barcelona inatafuta mrithi wa muda mrefu wa Robert Lewandowski, 37, ambaye anatarajiwa kuondoka mwisho wa msimu huu.
BARCELONA imewaweka katika rada zake mshambuliaji wa Bayern Munich na timu ya taifa ya England, Harry Kane, 32, pamoja na Julian Alvarez, 25, wa Atletico Madrid ambao mmoja inaweza kumsajili katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi.
Barcelona inatafuta mrithi wa muda mrefu wa Robert Lewandowski, 37, ambaye anatarajiwa kuondoka mwisho wa msimu huu.
Kane ana mkataba unaotarajiwa kumalizika 2027, lakini kuna kipengele kinachomwezesha kuondoka mwisho wa msimu huu kwa kiwango maalumu cha fedha, lakini kwa sharti la kutoa taarifa ifikapo Januari kwamba ataondoka baada ya msimu kumalizika huko Ulaya.
Tangu kuanza kwa msimu huu, Kane amecheza mechi 22 za michuano yote akifunga mabao 26 na kutoa asisti nne katika kikosi cha mabingwa watetezi Bundesliga. Barca bado ipo kwenye matatizo ya kifedha, hivyo ili kumsajili mmoja kati ya hao talazimika kuuza wachezaji kama Raphinha, Ferran Torres au Jules Kounde ili kupata pesa za kufanyia usajili.
Bruno Fernandes
MANCHESTER United ipo tayari kumuuza kiungo na nahodha wake Bruno Fernandes, 31, katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi Ulaya ili kupata fedha za kufanikisha usajili wa viungo wengine akiwamo Adam Wharton, 21, kutoka Crystal Palace; Elliot Anderson, 23 wa Nottingham Forest na yule wa Brighton na timu ya taifa ya Cameroon, Carlos Baleba mwenye umri wa miaka 21. Man United inataka kujenga kikosi kipya chenye wachezaji vijana zaidi
Casemiro
MANCHESTER United ipo tayari kumwachia kiungo wa kimataifa wa Brazil, Casemiro na winga wa England, Jadon Sancho katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi yajayo, ili kupunguza gharama za uendeshaji. Casemiro analipwa Pauni 350,000 kwa wiki, huku Sancho akilipwa Pauni 250,000. Sancho anaweza kurudi Borussia Dortmund au kuhamia Juventus, ambazo zote zimeonyesha nia ya kumsajili mara tu dirisha kubwa la usajili lijalo litakapofunguliwa.
Angelo Stiller
REAL Madrid imeanza mazungumzo na Stuttgart ya Ujerumani ili kumsajili kiungo wa timu hiyo, Angelo Stiller, 24, katika dirisha lijalo la usajili huko Ulaya. Real Madrid bado inapambana kutafuta viungo wenye umri mdogo ambao watakuwa na uwezo kama Toni Kroos na Luka Modric, na kuiwezesha kuitumikia timu hiyo kwa muda mrefu. Ada ya uhamisho ya mkali huyo inatajwa kufikia Euro 30 milioni.
Givairo Read
MANCHESTER City inamfuatilia kwa karibu beki wa kulia wa Feyenoord, Givairo Read, 19, ambaye imepanga kumsajili mwisho wa msimu huu. Hata hivyo, huenda ikapigwa bao na Bayern Munich ambayo tayari imefanya mazungumzo na upande wa mchezaji huyo kwa ajili ya vitu anavyotaka. Mkataba wake na Feyenoord unamalizika 2027, na kuna uwezekano timu yake kumuuza kwa Euro 35 milioni.
Pablo Barrios
ATLETICO Madrid haiatamuuza kiungo wa kimataifa wa Hispania, Pablo Barrios, 22, anayehitajika na Chelsea na Bayern Munich kwa ofa ya chini ya Pauni 88 milioni. Kwa mujibu wa tovuti ya Fichajes, kiasi cha Pauni 88 milioni ndicho kilichowekwa katika mkataba wake ikiwa kuna timu inataka kuuvunja. Chelsea inamwona kama mbadala wa muda mrefu wa Enzo Fernandez ambaye anaweza akatimkia Real Madrid mwisho wa msimu huu.
Kenan Yildiz
WAWAKILISHI wa Arsenal wamekutana na wakala Jorge Mendes jijini Turin kujadili uwezekano wa kumsajili mshambuliaji wa Juventus na timu ya taifa ya Uturuki, Kenan Yildiz, 20. Yildiz anachukuliwa kama moja ya washambuliaji bora Ulaya kwa sasa na kocha Mikel Arteta anaona kuwa atasaidia sana eneo la ushambuliaji.
Georges Mikautadze
TOTTENHAM Hotspur inajiandaa kuwasilisha ofa ya Pauni 44 milioni Villarreal ili kuipata saini ya mshambuliaji wa timu hiyo, Georges Mikautadze, 25. Mikautadze aling’ara katika Euro 2024 akiwa mfungaji bora wa Georgia, jambo lililosababisha timu nyingi zianze kumfuatilia. Msimu huu katika La Liga amefunga mabao matano katika mechi 14.