Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Simba pungufu yailaza Pamba Jiji

Muktasari:

  • Katika mchezo huo uliochezwa leo Agosti 19, 2026 ambapo Simba ilikuwa ugenini, imeonyesha ubora mkubwa na kufunga mabao mawili ya kipindi cha kwanza yaliyotosha kuipa pointi tatu.

SIMBA imeendelea kuonyesha ubora wake dhidi ya Pamba Jiji baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1, katika mechi ya Ligi Kuu Bara iliyochezwa Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, huku ikiwa pungufu ya mchezaji mmoja.

Katika mchezo huo uliochezwa leo Agosti 19, 2026 ambapo Simba ilikuwa ugenini, imeonyesha ubora mkubwa na kufunga mabao mawili ya kipindi cha kwanza yaliyotosha kuipa pointi tatu.

Ushindi huo unaifanya Simba kuendelea kuwa na rekodi nzuri dhidi ya Pamba Jiji, lakini jambo kubwa zaidi kwenye mchezo huo lilikuwa namna ilivyoutumia vizuri mwanzo wa mchezo na kumaliza kazi mapema.

Katika mechi tano ilizokutana timu hizo, Simba imeshinda nne, huku sare ikiwa moja. Pamba Jiji haijapata ushindi.

Simba ilihitaji dakika 18 tu kufunga bao dhidi ya Pamba Jiji baada ya Clatous Chama kutumia mpira uliotemwa na kipa Erick Johora.

Dakika ya 30, Simba ikaongeza bao la pili kupitia Anicet Oura aliyefunga kwa kichwa akiunganisha krosi ya Libasse Gueye na kwenda mapumziko iko kifua mbele kwa mabao 2-0.

Katika mechi hiyo ambayo Simba ilimaliza ikiwa pungufu baada ya kiungo wake, Ibraheem Jabaar kuonyeshwa kadi nyekundu, iliingia ikiwa na kasi, ikatumia mipira ya pembeni na kuwafanya mabeki wa Pamba kurudi nyuma mara kwa mara.

Anicet Oura upande mmoja na Libasse Gueye upande mwingine, waliipa Simba nguvu pembeni, huku Pamba Jiji ikishindwa kuwazuia kwa ufanisi waliokuwa nao.

Mabao mawili ndani ya dakika 30 yanaonyesha kwamba Simba iliingia kwenye mchezo ikiwa na mpango wa kumaliza mapema.

Sehemu ambayo Pamba ilipata wakati mgumu zaidi ilikuwa pembeni eneo wanalocheza mawinga Oura na Gueye ambao waliendelea kupata nafasi za kufungua njia, hali iliyolazimisha safu ya ulinzi ya Pamba kujisogeza pembeni na kuacha mianya katikati.

Gueye alikuwa na mchango mkubwa kwenye mabao yote mawili, akihusika katika kutengeneza nafasi iliyozalisha bao la pili huku kasi yake ikiwa tatizo kwa upande wa Pamba.

Kwa Simba, hii ilikuwa moja ya silaha zilizofanya iweze kutawala mchezo katika kipindi cha kwanza.

Dakika ya 44, Ibrahim Jabeer alionyeshwa kadi nyekundu baada ya kumrudishia kofi Abdul Kariim Yunus wa Pamba Jiji. Tukio hilo lilitokea baada ya Yunus kumchezea faulo Jabeer aliyekuwa anawania mpira wa kichwa.

Hii ni kadi ya pili nyekundu kuonyeshwa mchezaji wa Simba katika Ligi Kuu Bara msimu huu baada ya beki, David Kameta 'Duchu' dhidi ya Kagera Sugar.

Kipindi cha pili, Pamba Jiji ilirudi kivingine, ikapata bao dakika ya 73 kwa penalti iliyofungwa na Idris Diomande. Hadi mwisho, Simba ikaibuka na ushindi wa mabao 2-1.

Kwa Simba, sasa imekusanya pointi sita kufuatia kuzifunga Kagera Sugar (2-0) na Pamba Jiji (2-1) katika mechi mbili za kwanza ilizocheza, wakati Pamba Jiji ikiwa na moja ilipotoka sare ya 1-1 dhidi ya Dodoma Jiji na leo kupoteza, mechi zote ikiwa nyumbani.