Sababu Barbara kujiuzulu Simba ni hii hapa...

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez.
Muktasari:
- Ofisa Mtendaji Mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez ametangaza kujiuzulu nafasi yake ndani ya klabu hiyo kuanzia mwezi Januari mwakani.
MTENDAJI mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez ameandika barua ya kuachia ngazi ya uongozi huo itakapofika Januari 2023 akitaja sababu ya kupisha uongozi mpya.
Taarifa ya Mtendaji huyo aliyoiweka kwenye mitandao yake ya kijamii inasomeka, "Leo nimeandika barua ya kujiuzulu wadhifa wangu kama Afisa Mtendaji Mkuu wa Simba SC, kuanzia Juanuari mwakani, nimetoa notisi ya mwezi mmoja ili nishiriki kuhakikisha kipindi kizuri cha mpito (transition) na makubaliano (handover) na manejimenti mpya.
"Ni jambo la kifahari kwangu kwamba chini ya uongozi wangu, kwa kushirikiana na Rais wa Heshima wa Klabu, mwenyeti wa klabu, Bodi ya Wakurugenzi, wafanya kazi wenzangu, wachezaji, benchi la ufundi, wanachama, washabiki, wafadhili na wadau wetu wengine, klabu ilipata mafanikio makubwa ndani na nje ya uwanja, ikiwemo kutwaa mataji, kuvutia wafadhili na kuanza kuheshimika kama mojawapo ya vilabu vikubwa vya soka barani Afrika.
"Nimechukua uamuzi huu kwa sababu kubwa mbili, mosi ili kutoa nafasi kwa bodi mpya ya wakurugenzi itakavyochaguliwa kwenye uchaguzi ujao kupata fursa ya kuchagua Mtendaji Mkuu na menejimenti mpya itakayoendana na dira yao, pili kujipa nafasi ya kutimiza ndoto na fursa nyingine kwingineko.
"Nitumie nafasi hii, kipekee kabisa kuwashukuru wote tuliosafiri pamoja katika ndoto ya kufanya Simba SC iwe kubwa kuliko ilivyokuwa huko nyuma, ni uamuzi mgumu sana kuacha kazi unayoipenda na ulioifanya kwa moyo wote, lakini ni ukweli pia kwamba mambo yote mazuri huwa na mwisho.
"Simba itabakia ndani ya moyo wangu na kama sehemu ya familia yangu, naahidi kuwa nitaendelea kuwa mwana Simba kindakindaki na balozi mwaminifu wa klabu popote pale nitakapokuwepo, ahsanteni sana."
Mtendaji huyo alianza kuiongoza Simba Septemba 2020, alichukua nafasi ya Senzo Mazingiza ambaye pia alijiuzulu nafasi hiyo na baadae kutimkia kwa watani wa Yanga.