Ngassa azua ubishi

Ngassa azua ubishi

Muktasari:

  • WINGA machachari wa Gwambina FC, Mrisho Ngassa amesema bado ana nafasi ya kucheza Taifa Stars licha ya watu wengi kumchukulia kawaida.

WINGA machachari wa Gwambina FC, Mrisho Ngassa amesema bado ana nafasi ya kucheza Taifa Stars licha ya watu wengi kumchukulia kawaida.

Ngassa ndiye kinara wa mabao 25 katika rekodi ya wachezaji wanaoongoza kwa kufunga Taifa Stars katika miaka ya hivikaribuni, Stars sasa inanolewa na kocha Kim Poulsen.

Akizungumza na Mwanaspoti, Ngassa alisema; “Yule mtu ambaye anaongoza kwa mabao anaweza asiwe na msaada sana, lakini anaweza akawaharibu kisaikolojia wapinzani wakawa wananikaba mimi na mwingine akafunga, lakini Watanzania hatujui umuhimu huu.”

“Waandishi wengi wa Tanzania mfano timu ikija, wakisema mfungaji wao wa muda wote yupo, ukweli ni kwamba lazima watakuwa wanajipanga na mimi kwani muda wowote wanajua nitafunga,” alisema Ngassa huku akisisitiza kwamba haoni mchezaji wa kumzidi kwa kiwango cha kutisha katika nafasi yake Stars.

Ngassa alisema kuwa kwasasa yupo Gwambina na hana mpango wa kustaafu kucheza soka kwani anajiona bado ana uwezo mkubwa wa kucheza.

“Nina malengo yangu siku zote, naweza kucheza hapa, halafu baadae nikarudi tena katika timu kubwa, kikubwa ni kujituma na kujiwekea malengo tu”.

Aliongeza kwa kusema kuwa; “Kwasasa nipo majeruhi na hapa nimeanza kupona, naelewana vizuri na mwalimu na naamini kabisa Watanzania wataniona”.