Mashujaa na dakika 270 za mateso Ligi Kuu
Muktasari:
- Mashujaa ilianzia ugenini mechi tatu mfululizo ikianza na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Coastal Union, kisha kupoteza mbili mfululizo mbele ya Fountain Gate (1-0) na Mbeya City (2-1). Sasa inarejea mkoani Kigoma kuwakaribisha Kagera Sugar.
BAADA ya kucheza dakika 270 ugenini na kuvuna pointi tatu pekee, Mashujaa inarudi nyumbani, huku Kocha Mkuu Aman Josiah akifungia kazi nyota wake kufanya kweli.
Mashujaa ilianzia ugenini mechi tatu mfululizo ikianza na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Coastal Union, kisha kupoteza mbili mfululizo mbele ya Fountain Gate (1-0) na Mbeya City (2-1). Sasa inarejea mkoani Kigoma kuwakaribisha Kagera Sugar.
Akizungumza na Mwanaspoti, Josiah mbali na kukiri ugumu wa ligi na uzito wa safari, amesema hawana sababu nyingine zaidi ya kujipanga upya na mechi ijayo kuhakikisha wanashinda na kurejesha morali.
Amesema katika mechi dhidi ya Mbeya City, saikolojia ya wachezaji ilionekana kuwa chini, akieleza kuwa benchi la ufundi linaenda kusuka upya mbinu ili kurejesha kasi yao na ishu ya nyumbani na ugenini siyo tatizo kukosa ushindi.
“Kwa sasa hatuna namna nyingine zaidi ya kwenda kujipanga na mechi ijayo nyumbani dhidi ya Kagera Sugar, lazima tukubali ugumu wa ligi na namna ya kukabiliana na uzito huo, vijana wanao uwezo wa kubadili matokeo.
“Pointi tatu katika mechi tatu ugenini si mbaya sana japokuwa si matokeo mazuri pia kwa timu yenye malengo, lazima twende kusahihisha makosa na kuboresha tulipofanikiwa,” amesema kocha huyo.
Kwa upande wake nyota wa timu hiyo, Hija Shamte, amesema kila mchezo kwao ni vita ya pointi tatu na makosa yanayoonekana kiufundi, benchi la ufundi linaendelea kufanyia kazi.
“Matarajio yetu ni Mashujaa kufanya vizuri kwakuwa kila mchezaji anayo kiu ya mafanikio, matokeo ya mwanzo si mazuri sana, hivyo lazima tupambane tuwezavyo ili kufikia malengo,” amesema nyota huyo.