China: Kagoma, Mudathir wana vitu, Boban namba nyingine
Muktasari:
- Staa huyo wa zamani ambaye alikuwa anamudu kucheza namba 6, 8 na 10, amesema Mudathir ambaye ni kiungo wa Yanga, ana uwezo wa kukaba wakati mwingine kufunga, huku akimtaka Kagoma anayecheza Simba apandishe kiwango kwani ni bora kukaba pekee.
KIUNGO wa zamani wa Yanga, Simba na Taifa Stars, Athuman Abdallah 'China', amesema Mudathir Yahya na Yusuf Kagoma anaona angalau wanafanya vitu alivyokuwa anavifanya uwanjani, lakini kwa Haruna Moshi 'Boban' ilikuwa mashine nyingine.
Staa huyo wa zamani ambaye alikuwa anamudu kucheza namba 6, 8 na 10, amesema Mudathir ambaye ni kiungo wa Yanga, ana uwezo wa kukaba wakati mwingine kufunga, huku akimtaka Kagoma anayecheza Simba apandishe kiwango kwani ni bora kukaba pekee.
"Laiti kama zamani kungekuwa na data kama ilivyo kwa wachezaji wa sasa, nadhani data zingezungumza zaidi kuliko maneno, sijaona mchezaji wa sasa ambaye kafika kiwango nilichokuwa nacho," amesema China na kuongeza;
"Kipindi nacheza Ligi Kuu kila nikiwepo uwanjani, timu inayocheza ilikuwa kama ina wachezaji 13, nadhani walioniona hawatakuwa na shaka na maneno yangu."
Amesema kila akitazama mechi za Ligi Kuu, anaona bado ana uwezo wa kucheza kama ilivyo kwa mshambuliaji wa Al-Nassr, Cristiano Ronaldo ambaye kwa sasa ana umri wa miaka 41.
China ambaye ana umri wa miaka 59, amesema: "Nilichelewa kucheza Simba Day na Wiki ya Mwananchi, nadhani mechi ya maveterani mashabiki wangejionea wenyewe nilichokisema, maana Uingereza nacheza ligi za chini."
Wakati huohuo, China amesema, mchezaji pekee ambaye angefiti kile ambacho alikuwa anakifanya uwanjani, ni Haruna Moshi 'Boban'.
"Boban na mimi waliotuona watakiri kwamba tulikuwa na vipaji vikubwa na vya kushangaza, nadhani Boban angekuwa katika misingi sahihi, basi angecheza ligi kubwa duniani," amesema.