Saini zinazosubiriwa kwa hamu kubwa dirisha hili
Muktasari:
- Kutokana na hilo ndio maana imekuwa bize kufungulia pochi ikichuana na timu nyingine kama Liverpool, Chelsea na Arsenal kunasa mastaa wapya ambao watafanya timu yao kuwa na makali makubwa msimu huu.
LONDON, ENGLAND: MANCHESTER United inafahamu wazi kitu gani inachopaswa kufanya ili kurudi kwenye ubora wake na kuwa timu siriazi kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu England.
Kutokana na hilo ndio maana imekuwa bize kufungulia pochi ikichuana na timu nyingine kama Liverpool, Chelsea na Arsenal kunasa mastaa wapya ambao watafanya timu yao kuwa na makali makubwa msimu huu.
Kutokana na hilo bado kuna dili kibao zinaweza kufanywa na klabu za Ligi Kuu England, ambazo zitashuhudia mastaa kadhaa wakihama timu moja kwenda nyingine kabla ya dirisha halijafungwa Septemba Mosi.
Hizi hapa dili ambazo zinaweza kutokea muda wowote kwenye dirisha hili kabla halijafungwa ili kufanya timu kuwa na sura mpya kibabe msimu ukianza.
12) Rodrygo - Real Madrid kwenda Arsenal
Winga huyo wa Kibrazili amekuwa akihusishwa na Liverpool, lakini Arsenal ndiyo imekuwa ikitajwa mara nyingi kuhitaji winga wa aina yake. Real Madrid ipo tayari kumuuza, lakini kwa ofa nzuri. Arsenal inataka winga, lakini baada ya Liverpool kumuuza Darwin Nunez, hivyo itahitaji mshambuliaji mwingine.
11) Nicolas Jackson - Chelsea kwenda Newcastle
Baada ya kumkosa Benjamin Sesko, Newcastle inamfukuzia Nicolas Jackson kutoka Chelsea. Lakini, The Blues itahitaji pesa nyingi kwenye mauzo ya fowadi huyo, ada isiyopungua Pauni 60 milioni. Newcastle inasawaka pia Rodrigo Muniz, Ollie Watkins, Dominic Calvert-Lewin, Lois Openda na Goncalo Ramos.
10) Bradley Barcola - PSG kwenda Liverpool
Ripoti kutoka Ufaransa zinafichua kwamba Barcola anatazamwa na Liverpool kama mbadala wa Alexander Isak, hasa sasa baada ya Darwin Nunez kuondoka. Hata hivyo, Liverpool bado haijakoleza moto sana kwenye mchakato wa kunasa saini ya mkali wa Paris Saint-Germain licha ya kuwapo kwa pengo la Nunez.
9) Marc Guehi - Crystal Palace kwenda Liverpool
Kwenye dirisha la majira ya kiangazi mwaka jana, Newcastle ilikuwa bize kuwania saini ya beki wa kati wa Crystal Palace, Marc Guehi na bila shaka bado inamsaka hadi kwenye dirisha hili. Lakini, Mwingereza huyo kuna kila dalili akachagua kwenda kujiunga na Liverpool kwa ada ya Pauni 40 milioni.
8) Carlos Baleba - Brighton kwenda Man United
Staa Carlos Baleba anaweza kwenda kuifanya Manchester United kuwa timu ya kupiga pasi nyingi uwanja baada ya kuibuka taarifa za karibuni kwamba miamba hiyo ya Old Trafford inahitaji huduma ya mkali huyo. Man United ipo tayari kulipa Pauni 70 milioni kunasa saini ya Baleba kwenye dirisha hili.
7) Jack Grealish - Man City kwenda Everton
Everton inataka kumpa Jack Grealish kichaka cha kukimbilia ili aondoke kwenye balaa la kukaa benchi huko Manchester City. Hata hivyo, miamba hiyo inahitaji saini ya winga huyo Mwingereza kwa mkopo wa msimu mmoja wenye kipengele cha kumchukua jumla endapo kama itafurahishwa naye.
6) Eberechi Eze - Crystal Palace kwenda Arsenal
Eze yupo kwenye rada za Arsenal baada ya kufanikisha usajili wa straika Viktor Gyokeres. Na kiungo huyo mshambuliaji amekuwa akiwaambia wanzake namba anavyovutiwa na uhamisho wa kutua Emirates, lakini Arsenal bado haijawaweka wazi Crystal Palace kwenye mkwanja wao wanaotaka wa Pauni 68 milioni.
5) Yoane Wissa - Brentford kwenda Newcastle
Wachezaji wengi wanaonekana kuikataa Newcastle United kwenye dirisha hili, lakini staa wa Brentford, Yoane Wissa yupo tayari kujiunga na miamba hiyo ya St James’ Park. Kitu kizuri ni kwamba Brentford haihitaji pesa nyingi sana kwenye mauzo hayo, inataka Pauni 40 milioni tu ili ifanye biashara.
4) Alexander Isak - Newcastle kwenda Liverpool
Liverpool ilipeleka ofa yake ya kwanza ya Pauni 110 milioni ya kumtaka straika Alexandre Isak, lakini Newcastle United ilikataa. Kinachoelezwa ni kwamba Liverpool imepanga ofa nyingine ya Pauni 120 milioni, lakini miamba hiyo ya St James’ Park inamthaminisha straika wao kuwa na thamani ya Pauni 150 milioni.
3) Xavi Simons - RB Leipzig kwenda Chelsea
Uhamisho wa kwenda Chelsea unaonekana kumvutia Xavi Simons na sasa The Blues inapambana kuhakikisha inakamilisha dili hilo. Hata hivyo, itahitaji punguzo kubwa kutoka RB Leipzig kwenye ada ya Pauni 56 milioni ili kufanikisha dili hilo la kumnasa mchezaji huyo aliyewahi kutakiwa na Arsenal.
2) Alejandro Garnacho - Man United kwenda Chelsea
Chelsea imeshamsainisha Jamie Gittens kwenye dirisha hili la uhamisho wa majira ya kiangazi na ipo kwenye michakato ya kumsajili Xavi Simons. Inaonekana kama haimhitaji Garnacho, lakini ukweli ipo kwenye harakati za kumsajili winga huyo wa Kiargentina kutoka Manchester United.
1) Benjamin Sesko - RB Leipzig kwenda Man United
Dili la straika Benjamin Sesko kwenda Manchester United ni suala la muda tu, kwamba linaweza kutangazwa muda wowote. Lakini, hilo halifanyi kuwa dili lisilosubiriwa kwa hamu kutokea kwenye dirisha hili la majira ya kiangazi. Staa huyo ameshatua Manchester kwa ajili ya kupimwa afya huko Carrington.