Majeraha yaliyosumbua Kombe la Dunia 2026
Muktasari:
- Mara nyingi ni kawaida wachezaji wanaocheza ligi za kulipwa ambao waliitwa kuchezea timu zao za taifa kucheza mashindano haya wakiwa na tahadhari kubwa dhidi ya majeraha mbalimbali yatokanayo na soka.
Mashindano ya Kombe Dunia 2026 yaliyofanyika nchini Marekani, Canada na Mexico yalifika tamati siku ya Jumapili kwa Hispania kunyakua ubingwa kwa mara ya pili katika mchezo uliochezwa Jijini New Jersey.
Ilikuwa fainali kali iliyowakutanisha mabingwa watetezi Argentina dhidi ya Hispania ambayo ndio timu pekee ambayo katika mashindano haya haikupoteza mchezo wowote.
Mara nyingi ni kawaida wachezaji wanaocheza ligi za kulipwa ambao waliitwa kuchezea timu zao za taifa kucheza mashindano haya wakiwa na tahadhari kubwa dhidi ya majeraha mbalimbali yatokanayo na soka.
Ingawa zipo mbinu zinazosaidia kuepukana na majeraha lakini kwa mashindano kama haya ni vigumu kukosekana kwa majeraha kwani mchezo wa soka unahusisha kukumbana kimwili.
Mtakumbuka namna kadi nyekundu ya kiungo wa Argentina Enzo Fernandez katika dakika za majeruhi, ilionyesha kuwa mchezo wa soka unabeba vitu vingi ikiwamo kasi na nguvu lakini pia inahatarisha kupata majeraha.
Mpaka hatua ya fainal bado mastaa wengi walikuwa wako timamu wakiwa wamekwepa kupata majeraha makubwa , leo tutayaona mambo hatarishi na aina ya majeraha yanaliyojitokeza FIFA kombe la dunia 2026.
MAMBO YANAHATARISHA KUPATA MAJERAHA
Wachezaji ambao wako katika hatari ya kupata majeraha haya ni pamoja na wale wachezaji wanaotumika sana klabuni na timu ya taifa, umri mkubwa na majeraha mara kwa mara.
Vile vile wale wenye miili isiyo na ustahimilivu, kuwa na mazoezi yasiyo na kipimo, wasipasha moto mwili, wasiopumzimka, lishe duni, vifaa vya mazoezi visivyo sahihi na mbinu zisizo sahihi
Majeraha haya yanajitokeza kwa wanasoka hasa katika eneo la miguuni ikiwamo misuli, maungio, nyuzi za ligament na tendoni. Majeraha mengi mpaka hatua ya fainali yalikuwa ni wastani yanayopona.
AINA ZA MAJERAHA WANAYOPATA
- Majeraha ya misuli
Kuvutika kwa misuli ya mwili ni kazi ya mara mara katika soka, ni kawaida kukimbia kasi mara kwa mara. Misuli kuvutika kupita kiwango chake na kusababisha vijeraha vya ndani kwa ndani.
Hapo baadaye huweza kuwa vikubwa endapo mchezaji atacheza akiwa hajapona vizuri. Majeraha ya misuli huwa ni kuchanika msuli na kuvutika kupita kiasi, majeraha ya kamba za miishilio ya misuli yaani tendoni, uchovu wa misuli na kubanwa na msuli.
- Majeraha ya kifundo
Eneo la kifundo cha mguu huwa na harakati nyingi ikiwamo kupiga mpira, kujijeruhi kwa kujipinda vibaya au kukanywagwa. Ni kawaida kuwaona wakichechema wakati wa mwisho wa mchezo.
Majeraha ya kifundo cha mguu yanahusisha kuvunjika vifupa vya vidole vya miguu, majeraha ya tishu laini ikiwamo kuvutika kupitiliza, kukwanyuka na kuchanika kwa ligaments.
Wakati wakutembea, kukimbia kuruka na kutua, kifundo huweza kutua vibaya na kujipinda hivyo kujeruhi tishu laini ikiwamo nyuzi ngumu ambazo hujivuta kupita kiasi na kusababisha kupata majeraha.
- Majeraha ya goti
Ungio la goti linalobeba shinikizo kubwa na huwa na harakati nyingi wakati wa kucheza. Hii inalifanya kuwa katika hatari ya kujeruhiwa
Majeraha ya kati ya goti ikiwamo tishu laini, Ligamenti kuu za goti na mifupa plastiki, hupata maumivu sehemu ya goti eneo la mbele na shambulizi la nyuzi ngumu za miishilio ya misuli ya gotini yaani tendoni
Majeraha makubwa ya goti yanahusisha madhara au michubuko katika mfupa plastiki wa goti na nyuzi ngumu za ligament zinazounga mfupa na mfupa.
- Majeraha ya ugoko
Majeraha ya ugoko pamoja na maumivu yake ni moja ya majeraha yanatokea kwa wanasoka hii kwa sababu wao kuvaa kikinga ugoko maarufu kama shin Gurd.
Sehemu hii ambayo iko chini ya goti, maumivu yake yanatokea sehemu ya mbele ambao kuna mfupa mkubwa wa mguu chini ya goti unaoitwa kitabibu Tibia.
Vile vile maumivu ya eneo hili yanaweza pia kutokea katika makutano ya mifupa ya miguuni na sehemu ya mbele ya kifundo cha miguuni.
Majeraha haya kitabibu hujulikana kama shin splints, mara kwa mara yamekuwa yakiwapata wanasoka wanaoshriki mashindano kama haya.
Umbile hili husababisha majeraha ya mara kwa mara katika eneo la ugoko sehemu ya chini karibu na kifundo cha mguuni.
- Majeraha ya mifupa
Mpaka fainali hizo zinaisha hakuna mchezaji aliyepata mvunjiko wala kuteguka mifupa mikubwa ya maungio makubwa mwilini. Ingawa kupata majeraha kwa vijifupa vya funiko la mguu ni kawaida.
Kuvunjika kwa mfupa kunahusisha nyufa au kuvunjika kabisa vijipande viwili au zaidi, wakati kuteguka ni kulazimishwa kuhama kwa mfupa kutoka katika pango la maungio. Kuteguka mabega ndio huwapata wanasoka.
Wachezaji wa mpira wa miguu wamekuwa wakipata mivunjiko kidogo katika eneo la kifundo na magotini kwa kuanguka au kugongwa na mchezaji wa timu pinzani. Matukio ya mvunjiko na kuteguka yameripotiwa ni mawili.
- Majeraha ya kiakili
Tazama kilichowapata mashabiki na wachezaji wa Uingereza wakati wakipoteza mchezo wao dhidi ya Argentina katika mchezo wa nusu fainal. Tukio hilo limewaumiza kihisia na kuacha majeraha ya kiakili.
- Maeneo mengine ya mwili
Ni kawaida pia maeneo mengine ya mwili kugongwa na kupata majeraha ikiwamo maeneo ya kichwa na kifua hasa katika kuwani mipira ya juu. Vile vile mikono na vidole, hasa kwa makipa wakati wa kudaka.
CHUKUA HII
Ili kujikinga na majeraha mchezaji anatakiwa kupasha mwili moto kwa usahihi, kuzingatia mazoezi ya utimamu, lishe sahihi na unywaji maji, kutumia vifaa na mbinu sahihi, kupumzika na kulala, na kuhudumiwa kwa kuzingatia kanuni za Afya anapojeruhiwa hapo kwa papo.
Mchezaji kama Lionel Messi akiwa na umri wa miaka 39, akifunga magoli 8 na kusaidia magoli 4, imedhihirisha kuwa ni mmoja wa Bora zaidi duniani mwenye kuzingatia miiko ya utunzaji utimamu wa mwili.