Wanasoka na Tattoo kuna jambo
Muktasari:
- Alejandro Garnacho ni nyota wa hivi karibuni kujiunga na orodha ndefu ya wanasoka wenye michoro ya kuvutia iliyochorwa kwenye miili yao. Nyota huyo wa Chelsea aliwaonyesha mashabiki wake kupitia Instagram tattoo yake mpya.
LONDON, ENGLAND: WANASOKA na tattoo ni kama uji na mgonjwa. Wachezaji wengi wanaolipwa maelfu ya pauni kila wiki hupenda kutumia muda wao wa mapumziko kuchora tattoo mbalimbali miilini mwao.
Alejandro Garnacho ni nyota wa hivi karibuni kujiunga na orodha ndefu ya wanasoka wenye michoro ya kuvutia iliyochorwa kwenye miili yao. Nyota huyo wa Chelsea aliwaonyesha mashabiki wake kupitia Instagram tattoo yake mpya.
Mchezaji huyo wa Argentina ameongeza mchoro mkubwa wa mhusika wa Joker uliochezwa na Heath Ledger kwenye filamu The Dark Knight, ukiwa umechorwa mgongoni kote na msanii maarufu Ganga.
Tayari Garnacho alikuwa na tattoo zinazohusiana na mhusika wa Millie Bobby Brown katika Stranger Things, pamoja na kumbukumbu za Prison Break na anime ya Captain Tsubasa.
Swali ni: kwa nini wanasoka wengi hupenda tattoo? Mchanganyiko wa ujana, kipato kikubwa na muda mwingi wa mapumziko huwafanya wawe wateja bora wa sanaa hii ya mwilini.
1. Leroy Sane
Leroy Sane aliwahi kuchora mgongoni mwake picha kubwa yake mwenyewe akishangilia bao alilofunga dhidi ya AS Monaco akiwa na Manchester City kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu wa 2016/17.
Tatizo pekee ni kwamba City iliondolewa kwenye mashindano hayo kwa sheria ya mabao ya ugenini baada ya sare ya jumla ya mabao 6-6 dhidi ya Monaco ya Kylian Mbappe.
Sane amesema alitumia siku nne za maumivu makali kukamilisha mchoro huo.
2. Lionel Messi
Lionel Messi alianza kuchora tattoo kwenye mguu wake wa kushoto mwaka 2012 kusherehekea kuzaliwa kwa mwanawe wa kwanza, Thiago.
Kwa miaka kadhaa, mguu huo ulikuwa na michoro mbalimbali ikiwemo visu na mabawa. Baadaye Messi alifunika baadhi ya michoro hiyo kwa rangi nyeusi baada ya kukosolewa mitandaoni.
Kwa sasa, mguu wake una alama ya mkono wa mwanawe, tarehe za kuzaliwa, mpira wa miguu na namba yake maarufu 10.
Mbali na hayo, Messi ana tattoo ya mama yake, picha ya Yesu, rozari na dirisha la kanisa maarufu la Sagrada Familia.
Inakadiriwa kuwa tattoo zake zote zimegharimu zaidi ya pauni 50,000.
3. Marcus Rashford
Marcus Rashford ana tattoo nyingi zinazohusiana na dini, familia na mji wake wa kuzaliwa wa Manchester.
Miongoni mwa michoro yake ni mistari mitatu ya Biblia, kumbukumbu ya bibi yake aliyefariki na mikono iliyounganishwa katika sala.
Pia ana alama ya nyuki wa Manchester mkononi na picha ya nyumba aliyokulia kwenye mwili wake.
Tattoo zake zinakadiriwa kugharimu kati ya pauni 15,000 hadi 20,000.
4. Sergio Ramos
Sergio Ramos anatajwa kuwa mmoja wa wanasoka wenye mkusanyiko wa tattoo nyingi zaidi duniani.
Ana mamia ya michoro mwilini, kuanzia picha za kidini hadi michoro ya mafanikio yake ya soka. Pia ana michoro inayohusiana na mbwa mwitu, mnyama anayempenda sana.
Inakadiriwa kuwa Ramos ametumia hadi pauni 80,000 kwa tattoo zake.
5. Richarlison
Richarlison wa Tottenham Hotspur ana tattoo maarufu ya njiwa shingoni, ikihusiana na aina yake ya kushangilia mabao.
Lakini tattoo yake inayovutia zaidi ipo mgongoni, ikimuonyesha yeye pamoja na mastaa wa Brazil Neymar na Ronaldo Nazario.
Tattoo hiyo kubwa ya mgongoni inakadiriwa kugharimu takribani pauni 15,000.
Kwa ujumla, tattoo zimekuwa sehemu ya utambulisho wa wanasoka wengi wa kisasa. Kwa baadhi ni njia ya kuonyesha mafanikio yao, kwa wengine ni kumbukumbu za familia, dini au safari yao ya maisha, huku wengine wakizitumia kuonyesha mapenzi yao kwa filamu, vipindi vya televisheni na utamaduni wa pop.