Tuchel aja na ishu ya DNA
Muktasari:
- England iliongoza kwa bao 1-0 dhidi ya Argentina katika nusu fainali iliyochezwa Atlanta kabla ya Argentina kufunga mabao mawili na kushinda 2-1.
MIAMI, MAREKANI: KOCHA wa timu ya taifa ya England, Thomas Tuchel, ametetea maamuzi yake yaliyosababisha timu hiyo kuondolewa kwenye Kombe la Dunia, akisema tatizo halikuwa mbinu zake bali ni mtazamo wa wachezaji na kile alichokiita "DNA ya England".
England iliongoza kwa bao 1-0 dhidi ya Argentina katika nusu fainali iliyochezwa Atlanta kabla ya Argentina kufunga mabao mawili na kushinda 2-1.
Baada ya England kupata bao, Tuchel alimtoa mfungaji Anthony Gordon na kubadili mfumo wa ulinzi kwa kuongeza walinzi watano, hatua iliyokosolewa vikali na wachambuzi pamoja na mashabiki.
Hata hivyo, Tuchel amesema timu yake ilishindwa kumiliki mpira na kucheza kwa ujasiri.
"Umiliki wa mpira si sehemu ya DNA yetu kama ilivyo kwa Hispania, Argentina au Brazil. Tulikuwa wapole sana na hatukuonyesha nguvu za kutosha. Kwa maoni yangu, hakuna mfumo wowote duniani ambao ungeweza kutuokoa katika hali hiyo," amesema Tuchel.
Kocha huyo raia wa Ujerumani amesisitiza kuwa bado ana nia ya kuendelea kuifundisha England hadi michuano ya Euro ijayo.
"Ndiyo, kwa asilimia 100 nataka kuendelea. Bado kuna mambo mengi ya kuboresha na ninafurahia kazi hii. Ninaamini timu hii bado ina kiwango kingine cha juu cha kufikia," ameongeza.
England sasa inasubiri kucheza mechi ya mshindi wa tatu dhidi ya Ufaransa, mchezo utakaopigwa Jumapili ijayo muda mchache baada ya kumalizika mechi ya fainali.