Sio kinyonge… Wasanii hawa watanogesha Marekani

Muktasari:
- Mechi ya ufunguzi ambayo itapigwa katika dimba la Hard Rock, Miami, Florida, Al Ahly FC na Inter Miami CF zitaumana na kunatarajiwa kuwa na burudani mbalimbali kabla ya mechi ikiwemo muziki kutoka kwa Ma DJ wakubwa pamoja na shoo za kibabe kutoka kwa wasanii.
FLORIDA, MAREKANI: IKIWA imebakia wiki moja kabla ya kuanza kwa michuano ya Kombe la Dunia kwa klabu, tayari orodha ya wasanii watakaotumbuiza katika sherehe za ufunguzi wameshatangazwa.
Mechi ya ufunguzi ambayo itapigwa katika dimba la Hard Rock, Miami, Florida, Al Ahly FC na Inter Miami CF zitaumana na kunatarajiwa kuwa na burudani mbalimbali kabla ya mechi ikiwemo muziki kutoka kwa Ma DJ wakubwa pamoja na shoo za kibabe kutoka kwa wasanii.
WASANII WATAKAOKUWEPO
Wasanii chipukizi kutoka Afrika Kusini, Vikina na Richaelio ndio watakaoanza katika shoo za ufunguzi wakitarajiwa kuleta ladha ya muziki wa Afrika na watakuwa chini ya mtayarishaji wa muziki wa Marekani, Emilio Estefan Jr.
Akizungumza kuhusu sherehe hizo, Estefan alisema, "Hii itakuwa ni katika kusherehekea sauti za tamaduni mbalimbali kutoka duniani kote, tukionyesha mchanganyiko wa tamaduni na midundo mbalimbali. Tunaikaribisha dunia hapa Miami waje kufurahia muziki."
Kwa upande wa Vikina alisema kupewa nafasi ya kutumbuiza katika sherehe kwake ni ndoto iliyotimia.
Pia kutakuwa na wasanii wakongwe wa rap kama French Montana ambaye aliwahi kutamba na nyimbo yake ya No Stylist aliyomshirikisha Drake mwaka 2018.
Msanii mwingine mkubwa atakayetumbuiza ni Swae Lee, rapa maarufu kutoka kundi la Rae Sremmurd, ambaye hii itakuwa ni mara ya kwanza kutumbuiza katika shindano kubwa la mpira wa miguu.
Swae Lee alishirikiana na French Montana katika wimbo maarufu wa "Unforgettable," ambao ulipata umaarufu mkubwa na ulichezwa kwenye sherehe mbalimbali za mpira wa miguu.
Akizungumzia nafasi hiyo Montana alisema: "Hili ni jambo kubwa sana kwangu, naona nachelewa kufanya shoo hii na kuungana na mashabiki wote na kusherehekea kwa pamoja tukiunganisha soka na muziki kwa pamoja."
Kwa upande wa Lee alisema: "Hili si onyesho tu la muziki, linaunganisha mambo mengi, kuna soka, muziki wenyewe na tamaduni, tutafanya makubwa kuhakikisha dunia inaona moto uliopo Marekani."
BURUDANI NYINGINE
Pia kutakuwa na shoo nyingine za utumbuizaji kwa bendi na onyesho la watoto wadogo 32 ambao kila mmoja ataiwakilisha timu moja zinazoshiriki, watabeba nembo za timu hizo na kwa pamoja watatengeneza umbo la maandishi ambalo litasomeka 'FIFA'.
Sherehe zote hizi zitakuwa chini ya sauti ya mmoja kati ya MC wakubwa duniani ambaye amezoeleka kuonekana katika mapambano makubwa ya ngumi na sherehe mbalimbali, Michael Buffer.
Buffer alianza kuonekana kwenye kampeni ya matangazo ya DAZN ya Club World Cup 2025, akiwatambulisha wachezaji kama Erling Haaland, Harry Kane na Luis Suarez kwa namna ya kipekee.