Gwiji wa England Kevin Keegan Afariki dunia akiwa na miaka 75
Muktasari:
- Familia ya Keegan imethibitisha kifo chake, ikieleza kuwa alifariki akiwa amezungukwa na wapendwa wake.
Soka la England na dunia limegubikwa na simanzi baada ya gwiji wa zamani wa Liverpool, Hamburg, Southampton na Newcastle United, Kevin Keegan, kufariki dunia akiwa na umri wa miaka 75 baada ya kuugua saratani ya tumbo.
Familia ya Keegan imethibitisha kifo chake, ikieleza kuwa alifariki akiwa amezungukwa na wapendwa wake.
Keegan aligundulika kuwa na saratani ya tumbo iliyokuwa imefikia hatua ya nne mwezi Januari mwaka huu, baada ya kulazwa hospitalini kutokana na maumivu ya tumbo yaliyokuwa yakimsumbua kwa muda mrefu.
Licha ya hali yake, mara ya mwisho alionekana hadharani Mei 31 akiwa katika hali ya uchangamfu.
Rafiki yake wa karibu, Peter Graves, alitoa taarifa ya kifo hicho kwa ujumbe wa kugusa hisia.
"Kwa masikitiko makubwa tunatangaza kuwa Kevin Keegan amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 75," alisema Graves.
Alitamani kuaga Newcastle
Mwezi Mei, Keegan alihudhuria hafla katika Ukumbi wa Tyne Theatre ambako alieleza wazi kuwa alitamani kupata nafasi ya kuwaaga rasmi mashabiki wa Newcastle United kwenye Uwanja wa St James' Park.
Akizungumza na Graves, alisema:
"Nataka kusema kwaheri. Sikupata nafasi hiyo nilipoondoka Newcastle mara ya mwisho."
Kauli hiyo sasa imebaki kuwa moja ya maneno yake ya mwisho hadharani.
Alizungumza kuhusu ugonjwa wake
Keegan, aliyewahi kushinda tuzo ya Ballon d'Or mara mbili mfululizo, pia aliwahi kusimulia mazungumzo aliyofanya na daktari aliyekuwa akimhudumia.
"Waliniambia wana daktari bingwa mwenye mbinu mpya za kupambana na ugonjwa nilionao, ambao ni saratani ya hatua ya nne," alisema.
Kwa utani uliogusa hisia, aliongeza:
"Daktari huyo alikuwa shabiki wa Liverpool, hivyo nilikwenda kukutana naye. Nilijua sitatembea peke yangu, kama mnavyoelewa ninachomaanisha."
Ameacha historia kubwa
Keegan anakumbukwa kama mmoja wa wachezaji bora kabisa kuwahi kutokea England. Alishinda Ballon d'Or mwaka 1978 na 1979, akiwa mmoja wa Waingereza wachache kufikia mafanikio hayo.
Baada ya kustaafu kucheza, aliendelea kuandika historia akiwa kocha wa Newcastle United, timu aliyoiongoza kupigania ubingwa wa Ligi Kuu ya England na kuifanya kuwa moja ya timu zilizokuwa zikicheza soka la kuvutia zaidi katika miaka ya 1990.
Kifo chake kimeacha pengo kubwa katika familia ya soka duniani, huku akibaki kuwa mmoja wa watu waliotoa mchango mkubwa kwa mchezo huo ndani na nje ya uwanja.