Sikia hii mpya ya shabiki wa Man United
Muktasari:
- Shabiki Marin Levidzhov, 62, amekuwa na mapenzi makubwa kwa klabu ya Man United kiasi cha kumfanya achore tattoo ya nembo ya timu hiyo katika paji lake la uso.
SOFIA, BULGARIA: SHABIKI wa damu wa mchezo wa soka ambaye aliamua kubadili jina lake na kuitwa Manchester United amefariki dunia kwa kihoro baada ya timu yake kupata matokeo mabovu, amebainisha shemeji yake.
Shabiki Marin Levidzhov, 62, amekuwa na mapenzi makubwa kwa klabu ya Man United kiasi cha kumfanya achore tattoo ya nembo ya timu hiyo katika paji lake la uso.
Shemeji wa shabiki huyo, mrembo Elka Cankova, 63, alitoa lawama kwamba kifo cha Levidzhov kilichotokea wiki iliyopita kwa shambulio la moyo kimechangiwa na timu yake anayoshabikia, Man United kushindwa kufanya vizuri kwa miaka ya karibuni.
Amesema: “Kwake, Manchester United yalikuwa maisha yake. Alikuwa na hisia sana na mara zote baada ya vipigo alikuwa akinyong'onyea sana.
“Kuanzia kipindi ambacho Man United ilianza kuporomoka, alionekana kunyong'onyea. Inawezekana yenyewe ndiyo iliyomuua.”
Shabiki huyo raia wa Bulgaria, Marin alivutiwa na timu hiyo kiasi cha kumfanya kubadilisha jina lake la kuzaliwa wakati timu hiyo iliponyakua taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya 1999.
Hata hivyo, ilimchukua miaka 15 kushinda vita hiyo ya kubadilisha jina ili aitwe Manchester United.
Jumapili iliyopita, Man United iliichapa Liverpool 2-1 na kwamba timu ya Man United ilisononeshwa sana kwa taarifa za kwamba shabiki wao amefariki dunia.
Mrembo Elka amesema: “Kama Manchester angekuwa hai, angekuwa mwenye furaha sana kwa timu yake anayoshabiki kushinda.”