Kisa Trump barabara kufungwa, ulinzi mkali fainali NBA
Muktasari:
- Knicks wamewashangaza wengi kwa kushinda michezo miwili ya kwanza katika mfululizo wa michezo saba, wakishinda michezo miwili ugenini huku nyota wa Spurs, Mfaransa Victor Wembanyama akishindwa kufikia matarajio katika fainali hizo.
NEW YORK, MAREKANI: BARABARA zitafungwa, hakutaruhusiwa kuingia na mabegi au mifuko, pamoja na hatua kali za kiusalama zitawakabili mashabiki watakaoingia kwenye Ukumbi wa Madison Square Garden usiku wa leo, wakati Rais wa Marekani, Donald Trump, atakapowasili katikati ya Manhattan kushuhudia fainali ya tatu ya NBA kati New York Knicks dhidi ya San Antonio Spurs.
Knicks wamewashangaza wengi kwa kushinda michezo miwili ya kwanza katika mfululizo wa michezo saba, wakishinda michezo miwili ugenini huku nyota wa Spurs, Mfaransa Victor Wembanyama akishindwa kufikia matarajio katika fainali hizo.
Wakati huo huo, uwanja wa MetLife Stadium unatarajiwa kuandaa mchezo wake wa kwanza kati ya michezo minane ya Kombe la Dunia ndani ya wiki moja, lakini kwa sasa Fainali za NBA zimechukua umaarufu mkubwa jijini New York kuliko mashindano hayo ya kimataifa. Kufikia usiku wa Juni 6, hata tiketi za bei ya chini kabisa katika jukwaa la mauzo ya tiketi la StubHub zilikuwa zimefikia zaidi ya dola 9,000 za Marekani.
Kamati ya usalama imewasihi mashabiki wenye tiketi kufika mapema kwenye “Ukumbi Maarufu Zaidi Duniani”, ambao umejengwa juu ya kituo cha usafiri chenye shughuli nyingi zaidi nchini Marekani, Penn Station. Ukumbi huo utaandaa Fainali za NBA kwa mara ya kwanza baada ya zaidi ya miaka 25 huku Trump akihudhuria.
Mkuu wa usalama na Mawasiliano, Anthony Guglielmi, amesema katika taarifa kwa barua pepe: “Wahudhuriaji wanapaswa kujua baadhi ya barabara katika maeneo yanayozunguka Madison Square Garden zitafungwa kabisa.”
Ameongeza kuwa: “Sheria kali ya kutoruhusu mifuko yoyote kuingia ukumbini itawekwa, na tunataka kuwajulisha mashabiki mapema ili waweze kujipanga ipasavyo. Pia wahudhuriaji wanapaswa kutarajia ukaguzi wa usalama wa kiwango cha juu, unaofanana na taratibu za ukaguzi wa viwanja vya ndege.”
Huduma za treni za metro ya New York na reli ya abiria ya Long Island Rail Road zinatarajiwa kuendelea kawaida kupitia Penn Station bila usumbufu.
Kwa upande wa Knicks walitoa taarifa wakisema: “Mashabiki wanapaswa kujitahidi kupunguza vitu binafsi wanavyobeba hadi kiwango cha chini kabisa kinachowezekana.”
Trump ameendelea kutumia umaarufu wa matukio ya michezo katika muhula wake wa pili wa urais. Alikuwa rais wa kwanza madarakani kuhudhuria Super Bowl mwaka 2025, kabla ya kuhudhuria matukio mengine makubwa kama Ryder Cup na fainali ya Kombe la Dunia la Klabu.
Maelfu ya mashabiki walikosa mwanzo wa fainali ya tenisi kwa wanaume ya US Open mwezi Septemba baada ya ukaguzi wa usalama unaohusiana na uwepo wa Trump kusababisha mkanganyiko na kuchelewesha watu kuingia ukumbini.
Guglielmi amesema:“Ili kuhakikisha mashabiki wanaingia kwa wakati na kuepuka ucheleweshaji, tunawahimiza wafike angalau saa mbili kabla ya mchezo kuanza. Ingawa mipango ya mwisho bado inaendelea kuratibiwa, huu ndio mfumo wa maandalizi tunaotarajia kwa sasa.”
Knicks hawajashinda ubingwa wa NBA tangu mwaka 1973, na safari yao ya kwanza kufika fainali tangu mwaka 1999 imeamsha msisimko mkubwa katika wilaya zote tano za Jiji la New York.
Takribani mashabiki 6,500 walijazana nje ya Madison Square Garden Ijumaa usiku kwa ajili ya tamasha la kutazama mchezo, ambapo Knicks walipata ushindi wa kusisimua wa pointi 105-104 dhidi ya Spurs na kuongoza mfululizo huo kwa michezo 2-0.
Polisi wa Jiji la New York wamesema waliwakamata watu 17 katika tukio hilo, akiwemo mtu mmoja aliyempiga usoni askari mwanamke mwenye umri wa miaka 23.
Meya wa Jiji la New York, Zohran Mamdani, aliwataka mashabiki kusherehekea kwa uwajibikaji.
“Wakazi wa New York wana sababu ya kufurahia safari hii ya kihistoria ya Knicks katika fainali, na tunataka mashabiki washerehekee pamoja. Hata hivyo, hakuna nafasi ya vurugu, wala uvumilivu kwa mashambulizi dhidi ya maafisa wa polisi.”
Mamdani, ambaye ni shabiki wa muda mrefu wa Knicks, amehudhuria matukio mbalimbali ya michezo tangu alipochaguliwa meya mwaka 2025, na aliiambia redio ya New York 1010 WINS kwamba anapanga kuhudhuria Mchezo wa Tatu wa fainali hizo.