Kane afichua siri ya mabao 73
Muktasari:
- Wengi hujiuliza kwa nini mshambuliaji ambaye jukumu lake kubwa ni kufunga mabao asikae muda mwingi karibu na lango la wapinzani. Lakini msimu uliopita, nahodha huyo wa England na mshambuliaji wa Bayern Munich alifunga mabao 73, idadi kubwa zaidi kuwahi kufunga katika msimu mmoja katika maisha yake ya soka, licha ya kucheza akiwa amerudi chini zaidi kuliko alivyowahi kufanya.
LONDON, England; KADIRI umri unavyosonga mbele, Harry Kane amekuwa akibeba jukumu pana zaidi uwanjani, kiasi cha kushuka hadi karibu na boksi lake mwenyewe kutafuta mpira.
Wengi hujiuliza kwa nini mshambuliaji ambaye jukumu lake kubwa ni kufunga mabao asikae muda mwingi karibu na lango la wapinzani. Lakini msimu uliopita, nahodha huyo wa England na mshambuliaji wa Bayern Munich alifunga mabao 73, idadi kubwa zaidi kuwahi kufunga katika msimu mmoja katika maisha yake ya soka, licha ya kucheza akiwa amerudi chini zaidi kuliko alivyowahi kufanya.
Nilipomtajia mkanganyiko huo, Kane alitabasamu.
“Mpaka uielewe vizuri soka na kile tunachozungumzia hapa, ni rahisi sana kusema, ‘kaa juu, utapata nafasi na kufunga’, lakini soka halifanyi kazi hivyo,” anasema Kane.
Nilikaa naye chini na kuzungumza kuhusu undani wa mchezo wake, huku akieleza kwa kina namna anavyotekeleza jukumu lake la kipekee uwanjani.
KANE: MFUNGAJI ANAYEJUA KUJENGA MASHAMBULIZI
Unapomtazama Kane akifanya mazoezi, utaona wazi kiwango chake cha weledi. Mfungaji bora wa muda wote wa England huwa miongoni mwa wachezaji wa kwanza kufika uwanjani.
Wakati wachezaji vijana wakifurahia kupiga piga mpira kwa ustadi, Kane huwa pembeni akizungumza na mmoja wa wafanyakazi wa timu.
Kwa kumtazama kwa mbali, unaweza kudhani ni kocha. Lakini ukizingatia jukumu analobeba uwanjani, si ajabu kufanya kosa hilo.
Mtindo wa Kane kucheza unaakisi pia aina ya mtu alivyo. Wanaomfahamu wanamuelezea kuwa mtu mwenye uwezo mpana, mnyenyekevu na anayejituma ndani na nje ya uwanja.
Msimu bado upo mwanzoni, lakini Kane hakuwa akipumzika kutokana na mafanikio aliyoyapata katika miezi 12 iliyopita.
Akiwa amefanya mazoezi ya maandalizi ya msimu kwa siku tano pekee, nahodha huyo wa England alicheza dakika zote 90 katika ushindi wa Bayern Munich wa mabao 2-1 dhidi ya Borussia Dortmund na kutwaa Kombe la Super Cup la Ujerumani.
Pamoja na kwamba jukumu lake la kuzunguka uwanja linahitaji nguvu nyingi, Kane ameweza kuhimili mahitaji hayo ya mwili.
Katika misimu sita iliyopita, takwimu za kampuni ya teknolojia ya michezo ya STATSports, ambayo Kane pia amewekeza, zinaonyesha umbali aliokimbia, mbio za kasi na kasi ya kuongeza mwendo viliongezeka kwa asilimia 8, 22 na 42, mtawalia.
Na kutokana na namna mbinu za soka zilivyobadilika katika kipindi hicho, uwezo wa Kane kuendelea kuendana na mabadiliko hayo na hata kuwa mbele yake unavutia.
“Katika miaka mitano au sita iliyopita, mfumo wa kuwabana wapinzani mtu kwa mtu umeongezeka sana,” anasema Kane.
“Soka la Ulaya ni la nguvu. Timu kubwa zinajaribu kuupata mpira juu zaidi, huku zikiwaamini mabeki na viungo wao kucheza mtu kwa mtu na kushinda mapambano yao.”
Kutokana na mabadiliko hayo, timu bora zimekuwa zikisajili wachezaji wenye nguvu za mwili na uwezo mkubwa wa kupiga chenga ili waweze kumzidi mpinzani wao katika mchezo unaogeuka kuwa wa mtu dhidi ya mtu.
Kane, ambaye si maarufu kwa kupiga chenga na ambaye mwenyewe anakiri kuwa “si mtu mwenye kasi zaidi”, ameweza kufanikiwa kwa kutumia silaha zake mwenyewe.
AKILI BADALA YA KASI
Katika mchezo dhidi ya Dortmund, kulikuwa na tukio moja lililoonyesha kwa uwazi aina ya mchezo wa Kane.
Alishuka chini akitafuta nafasi ya kupokea mpira akiwa hajakabwa na mabeki. Kutambua hatari hiyo, wachezaji wawili wa Dortmund walimfuata.
Chenga za Kane zinaongozwa zaidi na akili kuliko kasi ya miguu. Kasi yake ya kufikiri humsaidia kupata suluhisho la tatizo ambalo wachezaji wengine wangejaribu kulitatua kwa kutumia miguu pekee.
Baada ya kushuka chini na kutumia nguvu zake kumtoa beki wa kati Waldemar Anton, Kane alisimama na kubadilisha kidogo mwelekeo wa mwili wake kuelekea kulia.
Mabadiliko hayo madogo ya mwili ni sehemu muhimu ya mchezo wake. Kupitia hatua hizo ndogo, anaweza kubadilisha mwelekeo wa mashambulizi ya timu nzima.
Daniel Svensson na Jobe Bellingham walidanganywa na mabadiliko hayo ya mwelekeo. Kane akairudisha mipira upande mwingine, akifungua uwanja mzima akiwa ndani ya nusu ya Bayern.
ASILIMIA 50 KANUNI, ASILIMIA 50 KANE
Mapema mwaka huu, kocha wa Bayern, Vincent Kompany aliwahi kueleza siri ya jukumu la Kane, akisema asilimia 50 yake inaongozwa na maelekezo ya kiufundi na asilimia 50 nyingine ni Kane mwenyewe kuamua nini afanye.
Kane anakubaliana na hilo.
“Kwa sehemu ni hisia, kutumia akili yangu ya soka na kuhisi kinachoendelea uwanjani,” anasema.
“Kwa mfano, nikitaka kushuka chini kuona kama beki wa kati atanitoka na kunifuata, anaweza kunifuata hadi kwenye kiungo. Lakini je, atafanya hivyo nikishuka mpaka kwenye boksi langu?”
“Baada ya dakika tano au 10 za kwanza, huwa unaanza kuelewa jinsi wapinzani watakavyocheza, na hilo ndilo linaloamua namna nitakavyocheza.”
Bayern kuna uelewano mkubwa kuhusu mfumo huo, unaowaruhusu wachezaji kuelewa mabadiliko ya nafasi ambayo kwa mtazamaji wa kawaida yanaweza kuonekana kama hayana mpangilio.
Kane, ambaye amepewa uhuru mkubwa kuliko wachezaji wengi, ndiye kiini cha mfumo huo.
“Nahisi sasa nafasi yangu ni kama mmoja wa viungo wawili namba 10, na tunafanya kazi pamoja,” anasema.
“Unaweza kujikusanya upande mmoja na kuongeza idadi ya wachezaji, jambo linalowaweka mabeki wa kati wa wapinzani kwenye tatizo la kuamua nani wamfuate.”
“Kama wanataka kuwafuata wote, watalazimika kucheza mtu kwa mtu, na hapo ndipo nafasi inafunguka kwa mawinga au mabeki wetu wa pembeni kukimbilia.”
“Unawauliza wapinzani maswali mengi, lakini binafsi napenda kuwa na mchezaji aliye karibu nami ambaye tunaweza kuunganisha naye mchezo.”
KUTOKA NAMBA 9 HADI NAMBA 10
Kane alijenga jina lake kubwa akiwa mshambuliaji wa kati, namba tisa, anayebaki mbele peke yake.
Ndiyo maana inashangaza kumsikia akijitambulisha sasa kama namba 10 anayefanya kazi ndani ya mfumo wa washambuliaji wawili.
“Unapokuwa namba tisa peke yako, unaweza kuwekwa chini ya ulinzi wa mabeki wawili wa kati na ukapata shida kugusa mpira,” anasema.
“Unategemea wachezaji wengine wakutafutie mpira.”
Nilimwonyesha Kane video mbili kutoka msimu uliopita na kumuomba kueleza kilichokuwa kikimpita akilini wakati wa matukio hayo.
“Kitu kuhusu mfumo wetu ni kwamba, mradi tu kuna mtu katika kila nafasi, si muhimu sana ni nani anayekuwa hapo. Katika kipande hiki, Lucho (Luis Diaz) anacheza kama mmoja wa hao namba 10.”
“Mimi nimesogea pembeni ili kujaribu kutengeneza nafasi kidogo, wakati Lucho ameingia katikati.”
Harakati za Kane za kushuka chini zilimfanya mmoja wa viungo wa wapinzani kumfuata. Hilo likafungua nafasi na kumruhusu Joshua Kimmich kupenyeza mpira hadi kwa Diaz.
“Nadhani ni Serge (Gnabry) anayekimbia nyuma ya mabeki, jambo linalowafanya mabeki warudi nyuma na kutupa mimi na Lucho nafasi katikati.”
“Lucho anaurudisha mpira kwangu na ninapokuwa katika eneo lile, takribani yadi 20 hadi 25 kutoka langoni, huwa natazama kama ninaweza kupiga shuti.”
Ni moja ya mifano mingi ambayo Kane huanza kwa kushuka chini kabla ya kuibuka na kufunga.
“Kwa kucheza chini wakati shambulizi linajengwa, mwisho wa yote naingia kwenye nafasi ya namba 10 wakati kila mtu ameshuka,” anasema.
“Naweza kupiga shuti kutoka ukingoni mwa boksi, ambalo ni moja ya nguvu zangu kubwa, au nakimbia nyuma ya wachezaji ambako hakuna anayenifuatilia kwa sababu kiungo huwa anapata ugumu kunifuatilia.”
HATA ASIPOGUSA MPIRA, KANE ANAHUSIKA
Video ya pili ilikuwa kutoka katika mchezo wa Bayern wa Ligi ya Mabingwa dhidi ya Club Brugge.
Kwa kawaida Kane hupewa ulinzi na beki wa kati wa wapinzani, lakini Club Brugge ilimkabidhi jukumu hilo kiungo wao mkabaji.
Kane alilitambua hilo na kulitumia.
Lennart Karl alifunga bila Kane hata kuugusa mpira, lakini mchango wa mshambuliaji huyo katika bao hilo ulikuwa wazi.
“Hizi ndizo zile harakati ndogo ambazo si kila mtu huziona,” Kane anaeleza.
“Jamal Musiala na Lenny ni wazuri sana wanapopokea mpira na kupiga chenga, kwa hiyo wakati mwingine mimi hubaki juu zaidi na kuwaacha wao wapokee mpira chini, huku mimi nikifanya mbio za kuingia nyuma ya mabeki.”
“Bila kubadilisha sana mchezo wangu, huwa najitahidi kuendana na wachezaji wanaonizunguka.”
“Najua Lenny ni mzuri sana katika zile nafasi za kati. Anapokuwa huko, mimi nafikiria zaidi kukimbia nyuma ya mabeki kwa sababu, kwanza, anaweza kunipa pasi nikatokeana na kipa, au pili, anaweza kupiga chenga na kufanya kile kilichotokea hapa.”
“Mara tu Lenny anapoingia kwenye nafasi hiyo, mimi nakimbia. Si kila wakati kwa ajili ya kupokea mpira; wakati mwingine ni kumtoa beki kwenye eneo lake.”
“Sasa Lenny anabaki kwenye hali ya mtu mmoja dhidi ya beki mmoja katikati ya uwanja, na hilo ni hatari kwa beki yeyote wa kati.”
ZAIDI YA MABAO 73
Wakati mjadala wa tuzo ya Ballon d’Or ukiwa ukikaribia, jina la Kane limekuwa likitajwa kutokana hasa na idadi kubwa ya mabao aliyofunga.
Lakini jambo ambalo linaweza kupuuzwa katika mjadala huo ni ukubwa wa mchango wake katika maeneo mengine ya mchezo.
Kane huichezea timu katika kila hatua ya mchezo na katika kila sehemu ya uwanja, huku akiendelea kutengeneza takwimu binafsi za kiwango cha juu zinazomweka kwenye kundi moja na nyota kama Cristiano Ronaldo, Lionel Messi na Erling Haaland.
Wakati mwingine amejielezea kama mchezaji anayecheza nafasi ya namba 10, namba 9 na hata namba 6.
Katika dunia ya soka ambayo majukumu ya wachezaji yamekuwa yakigawanywa kwa usahihi mkubwa na kufundishwa kwa maelekezo maalumu, uwezo wa Kane kucheza nafasi hizo mbalimbali kwa ufanisi ni jambo kubwa.
Na pengine hapo ndipo siri ya mabao yake 73 ilipo: Kane haishii kuwa mshambuliaji anayesubiri mpira ufike kwake yeye mwenyewe huenda kuutafuta mpira, hujenga mashambulizi, huvuta mabeki kutoka kwenye nafasi zao na, hatimaye, hujitengenezea mazingira ya kufunga.