Henry: Gyokeres ana shida
Muktasari:
- Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Sweden ambaye amechukua jezi maarufu ya namba 14 iliyokuwa inavaliwa na Henry, alipata nafasi ya wazi akienda langoni mwa upinzani katikati ya kipindi cha kwanza cha mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya Jumanne usiku, lakini alisukumwa pembeni na kufyatua shuti lililokwenda moja kwa moja mikononi mwa kipa wa Bilbao, Unai Simon.
LONDON, ENGLAND: LEJENDI wa Arsenal, Thierry Henry ameonyesha kutokuridhishwa na namna straika wa timu hiyo, Viktor Gyokeres alivyocheza katika mechi dhidi ya Athletic Bilbao kutokana na kupoteza nafasi muhimu na kuweka wazi tatizo linalomkabili staa huyo.
Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Sweden ambaye amechukua jezi maarufu ya namba 14 iliyokuwa inavaliwa na Henry, alipata nafasi ya wazi akienda langoni mwa upinzani katikati ya kipindi cha kwanza cha mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya Jumanne usiku, lakini alisukumwa pembeni na kufyatua shuti lililokwenda moja kwa moja mikononi mwa kipa wa Bilbao, Unai Simon.
Ufanisi wa Gabriel Martinelli katika tukio sawa na hilo mwishoni mwa mchezo ulionyesha tofauti kubwa, jambo lililomfanya Henry amkosoe Gyokeres.
Akizungumza na kituo cha televisheni cha Marekani, CBS, baada ya mchezo, Henry alisema:
"Nilizungumza kuhusu Gyokeres na mnakumbuka, niliposimama kuonyesha picha, Martinelli alikuwa mbele ya mabeki na akafunga. Hicho ndicho ninachomaanisha ni lazima aongeze kipengele hicho kwenye uchezaji wake."
Gyokeres alikuwa na mchezo wa kawaida, akigusa mpira mara 19 pekee na kupiga pasi sita zilizofika, kabla ya kutolewa dakika ya 60 na nafasi yake kuchukuliwa na Leandro Trossard, aliyefunga bao la pili la Arsenal na kuihakikisha ushindi katika mchezo uliomalizika kwa washika mitutu hao kushinda mabao 2-0.
Mshambuliaji huyo alipigwa kichwani na kulazimika kucheza akiwa na bandeji kubwa usoni. Hata hivyo, alipiga mashuti manne licha ya kutohusika sana, lakini Henry alisisitiza anahitaji kuwa na umakini zaidi mbele ya lango na kujua namna anavyoweza akapishana na mabeki anapokuwa na mpira katika eneo la mwisho.
Henry aliendelea kusema: "Bila shaka atakuwa hana offside. Ninachojaribu kusema ni ili ufunge lazima umpite beki na sioni sababu ya beki kukupokonya mpira ikiwa unalinda mpira ipasavyo."
Mchambuzi mwingine wa masuala ya soka ambaye ni mchezaji wa zamani wa Manchester City, Michael Richards naye aliungana na Henry akisema: "Ndiyo, ndiyo. Tazama, sote tunajua amekuwa akifunga mabao, lakini ukiwa ugenini, nafasi kama ile lazima iwe bao. Martinelli aliibadilisha kuwa bao."
Aidha, Henry aliweka presha kwa timu yake ya zamani akisema ni lazima kushinda taji msimu huu.
"Sasa tuwe wakweli, ni lazima mwaka huu kushinda kitu. Ni lazima. Hatuwezi kujificha.
Ni lazima tushinde kitu. Ukizungumzia yaliyofanywa hivi karibuni, kumaliza nafasi ya pili hakukupi kombe. Ni jambo kubwa, lakini wakati fulani ni lazima uthibitishe ubora wako kwa taji."
Gyokeres ambaye amejiunga na Arsenal dirisha la majira ya kiangazi msimu uliopita, alicheza mechi nne za michuano yote na kufunga mabao matatu.
Alifunga mabao mawili katika ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya Leeds United, pia alifunga bao moja katika mchezo wa Nottingham Forest na Arsenal ilishinda mabao 3-0.
Mara kadhaa Kocha Mikel Arteta alipoulizwa juu ya maendeleo ya fundi huyu alisema kuna wakati anapata wakati mgumu kwa sababu eneo la kiungo huwa halimlishi vya kutosha.