Faulo ya Gabriel Magalhaes yaacha gumzo
Muktasari:
- Arsenal ililazimika kutoka nyuma baada ya Morgan Rogers kuifungia Chelsea bao la mapema katika dakika ya pili, kabla ya Kai Havertz na Martin Odegaard hajawaifungia Arsenal na kuipa ushindi katika mchezo huo wa Ligi Kuu England.
LONDON, ENGLAND: BEKI wa Arsenal, Gabriel Magalhaes, ameambiwa ni mtu mwenye bahati baada ya kuepuka kadi nyekundu kufuatia tukio la kumpiga teke kichwani kipa wa Chelsea, Emiliano Martinez, katika ushindi wa mabao 2-1 wa Arsenal dhidi ya Chelsea.
Arsenal ililazimika kutoka nyuma baada ya Morgan Rogers kuifungia Chelsea bao la mapema katika dakika ya pili, kabla ya Kai Havertz na Martin Odegaard hajawaifungia Arsenal na kuipa ushindi katika mchezo huo wa Ligi Kuu England.
Hata hivyo, tukio lililomhusisha Gabriel limeendelea kuwa gumzo kubwa baada ya mchezo huo, huku mshambuliaji wa zamani wa Manchester United, Wayne Rooney, akisema beki huyo alistahili kuonyeshwa kadi nyekundu.
Tukio hilo lilitokea dakika ya sita wakati wa vurugu kwenye mpira wa kona. Gabriel alikuwa chini akigombea mpira na beki wa Chelsea, Jorrel Hato, ndipo mguu wake ulipomkuta Martinez usoni.
Martinez, ambaye alikuwa tayari ameudaka mpira kwa mikono yake, alilazimika kupewa matibabu, lakini mwamuzi Chris Kavanagh hakuchukua hatua dhidi ya Gabriel.
Uamuzi huo pia uliungwa mkono na waamuzi wa VAR, jambo ambalo limezua mjadala mkubwa miongoni mwa wachambuzi na mashabiki.
Akizungumza katika kipindi cha Match of the Day, Rooney amesema Gabriel alikuwa na bahati kubwa kuendelea na mchezo.
“Kwa mara ya kwanza huwezi kuona vizuri, lakini ukiangalia marudio na kupunguza kasi, Martinez alikuwa ameshika mpira kwa mikono yote miwili, kisha Gabriel akampiga teke kichwani,” amesema Rooney.
“Alikuwa ameshika mpira kwa mikono yote miwili na Gabriel alikuwa juu sana ya mpira. Kwa hiyo, nafikiri ana bahati sana kuendelea kuwa uwanjani.”
Mchezaji wa zamani wa Manchester United na mchambuzi mwenzake, Ashley Young, alikubaliana na Rooney, akisema VAR ilipaswa kulichunguza kwa kina tukio hilo.
“Nilikuwa na mtazamo huohuo. Tulizungumza kuhusu tukio hilo wakati huo na tukasema hakuna kilichotokea, lakini unapoliona tena, Martinez alikuwa ameshika mpira kwa mikono yake na Gabriel akapandisha mguu juu na kumpiga kichwani,” amesema Young.
“Siwezi kuelewa kwa nini VAR haikuliangalia vizuri, kwa sababu Gabriel alikuwa mbali na mpira. Nafikiri amepona hapo.”
ANATETEWA
Licha ya ukosoaji huo, aliyewahi kuwa mkuu wa waamuzi England, Keith Hackett, alitetea uamuzi wa kutomtoa Gabriel.
Akizungumza na Football Insider, Hackett amesema mwamuzi huenda hakuwa na mtazamo mzuri wa tukio hilo na kwamba kitendo cha Gabriel hakikuonyesha nia ya kumdhuru Martinez.
“Ni wazi mwamuzi hakuwa na mtazamo wa tukio. Kwa maoni yangu, kitendo cha mchezaji wa Arsenal hakikuonyesha nia mbaya na hivyo nakiona kama tukio la bahati mbaya. VAR pia, kwa busara kwa maoni yangu, iliamua kutuingilia,” amesema.
Gabriel hakupata adhabu yoyote na aliendelea kucheza hadi mwisho, akitoa mchango mkubwa katika kuwadhibiti washambuliaji wa Chelsea, Rogers, Joao Pedro na Cole Palmer.
Beki huyo pia alihusika katika tukio lingine baadaye katika mchezo, ambapo alionekana kumzuia Pedro Neto kwa mwili nje ya mpira karibu na kibendera cha kona, lakini hakuchukuliwa hatua.