Donnarumma ni suala la muda tu kusaini Manchester City
Muktasari:
- Kipa huyo Mtaliano ameshindwa kusaini dili jipya kwenye klabu yake ya Paris Saint-Germain na hivyo yupo tayari kuachana na miamba hiyo ya Paris.
GIANLUIGI Donnarumma ameripotiwa kufikia makubaliano na klabu ya Manchester City.
Kipa huyo Mtaliano ameshindwa kusaini dili jipya kwenye klabu yake ya Paris Saint-Germain na hivyo yupo tayari kuachana na miamba hiyo ya Paris.
Donnarumma, 26, amebakiza mwaka mmoja tu kwenye mkataba wake kwenye kikosi hicho cha miamba ya Ligue 1, ambayo ipo tayari kumuuza ili kupata pesa kuliko kusubiri mwakani aondoke bure.
Kwa mujibu wa Fabrizio Romano, kipa huyo amefika makubaliano ya kujiunga na Man City na sasa kinachosubiriwa ni makubaliano ya klabu juu ya ada ya uhamisho. Uhamisho wa Donnarumma kwenda Etihad unategemea na hatima ya kipa namba moja wa Man City, Ederson, ambaye amekuwa akiwindwa na Galatasaray. PSG tayari imeshapata kipa wa kuchukua mikoba ya Donnarumma, ilipomsajili Lucas Chevalier kutoka Lille. Mashabiki wa Man City watakuwa kwenye furaha kubwa watakapofanikisha usajili wa kipa Donnarumma hasa baada ya James Trafford kuonyesha kiwango cha hovyo.
Rasmus Hojlund
NAPOLI imapanga kukamilisha dili la kumsajili Rasmus Hojlund mwenye umri wa miaka 22, ndani ya wiki hii baada yakuwa katika mazungumzo kwa muda mrefu. Napoli inataka kuharakisha mchakato huo baada ya mshambuliaji wao Romelu Lukaku, 32, kupata jeraha. Hojlund ambaye alisajiliwa na Man United kwa Pauni 72 milioni kutoka Atalanta mwaka 2023, amepewa ruhusa ya kuondoka na kocha Ruben Amorim kwa sababu hayupo kwenye mipango yake.
Soungoutou Magassa
ATALANTA, West Ham na Nottighan Forest zipo katika vita kali ya kuiwania saini ya kiungo wa AS Monaco, Soungoutou Magassa katika dirisha hilj.
Soungoutou mwenye umri wa miaka miaka 21, mwenyewe anaonekana kuwa na uhitaji zaidi wa kutua England kuliko sehemu nyingine yoyote.
Mabosi wa Monaco wanataka zaidi ya Pauni 20 milioni ili kumuuza staa huyu.
Timu zote zinatarajiwa kutuma ofa ndani ya wiki hii.
Lorenzo Pellegrini
WEST Ham inaangalia uwezekano wa kumsajili staa wa AS Roma, Lorenzo Pellegrini mwenye umri wa miaka 29, ambaye amevuliwa kitambaa cha unahodha baada ya kutofautiana na kocha wa timu hiyo.
Inaelezwa Lorenzo haitaji kuendelea kusalia Roma ambayo hadi sasa ameichezea zaidi ya mechi 250 za Serie A. West Ham inataka kutoa takribani Pauni 30 milioni ili kuvunja mkataba wake.
Bilal El Khannouss
BAADA ya kuikosa saini ya Eberechi Eze aliyetimkia Arsenal, mabosi wa Tottenham wameenda kuanzisha mazungumzo na Leicester City ili kuipata saini ya kiungo wa timu hiyo na Morocco, Bilal El Khannouss. Hata hivyo, ili kuipata huduma yake itatakiwa kwanza kushinda vita dhidi ya Crystal Palace ambayo pia inahitaji huduma ya staa huyu mwenye umri wa miaka 20. Bilal ni miongoni mwa wachezaji waliong’ara katika michuano ya AFCON 2023.
Alexander Isak
KOCHA wa Newcastle, Eddie Howe ameweka wazi kuwa watapambana kusajili mshambuliaji mwingine katika dirisha hili ikiwa Alexander Isak ataondoka.
Isak ambaye anahusishwa kuwa huenda akatimkia Liverpool iliyoweka mezani Pauni 130 milioni kama ofa ya ada yake ya uhamisho, ameshindwa kujumuika katika mazoezi ya pamoja na wenzake baada ya sintofahamu iliyoibuka kati yake na viongozi.
Carney Chukwuemeka
BORUSSIA Dortmund ipo katika hatua za mwisho kumsajili kiungo wa Chelsea, Carney Chukwuemeka, 21, kwa ada ya Euro 25 milioni katika dirisha hili pamoja na beki Aaron Anselmino naye kutoka Chelsea lakini atajiunga kwa mkopo wa msimu mmoja.
Chukwuemeka aliomba mwenyewe kuondoka ili muda zaidi wa kucheza.
Antony
REAL Betis bado inajadiliana na Manchester United juu ya uwezekano wa kuipata saini ya winga wa timu hiyo na Brazil, Antony, 25, baada ya kuvutiwa na kiwango bora alichoonyesha msimu uliopita alipokuwa kwa mkopo.
Antony ambaye alisajiliwa na Man United mwaka 2022 chini ya kocha Erik Ten Hag kwa Pauni 85 milioni akitokea Ajax hakuwa na wakati mzuri Man United.